Mwanzo 13 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Abramu na Loti wanatengana 1 Abramu akarudi kutoka Misri, akaingia upande wa Negebu. Alikuwa na muke wake na mali yake yote pamoja na Loti. 2 Wakati ule, Abramu alikuwa ametajirika sana. Alikuwa na makundi ya nyama, feza na zahabu. 3 Akaendelea kusafiri toka eneo la Negebu mpaka Beteli. Alifika pahali alipokuwa amepiga kambi ya hema mara ya kwanza kati ya Beteli na Ai, 4 pahali ambapo alikuwa amejenga mazabahu. Pale Abramu akamwomba Yawe kwa jina lake. 5 Na Loti, ambaye alikwenda pamoja na Abramu, alikuwa na kondoo, na makundi mengi ya nyama na hema. 6 Hesabu ya nyama wao ilikuwa kubwa sana hata inchi ile haikuweza kutosha kwa Abramu na Loti kuishi pamoja. 7 Basi, kukatokea ugomvi kati ya wachungaji wa Abramu na wachungaji wa Loti. Wakati ule, Wakanana na Waperizi ndio waliokuwa wenyeji wa inchi hiyo. 8 Basi, Abramu akamwambia Loti: “Kusikuwe ugomvi kati yetu wala kati ya wachungaji wako na wachungaji wangu, kwa sababu sisi ni jamaa moja. 9 Angalia inchi hii yote mbele yako. Na tutengane. Ukikwenda kushoto, mimi nitakwenda kuume. Ukikwenda kuume, mimi nitakwenda kushoto.” 10 Loti akainua macho yake, akaona bonde la muto Yordani, akaona kwamba lina maji ya kutosha kila pahali, kama vile bustani ya Yawe na kama vile inchi ya Misri upande wa Soari. (Hii ilikuwa mbele Yawe hajaiangamiza miji ya Sodoma na Gomora). 11 Kwa hiyo, Loti akajichagulia bonde lote la muto Yordani, akaelekea upande wa mashariki, na hivyo wakatengana. 12 Abramu akabaki katika inchi ya Kanana na Loti akakaa kati ya miji iliyokuwa katika bonde, akahamishia kambi yake Sodoma. 13 Watu wa Sodoma walikuwa waovu na watenda zambi wakubwa mbele ya Yawe. Abramu anaonyeshwa inchi 14 Nyuma ya Loti kujitenga na Abramu, Yawe akamwambia Abramu: “Inua macho yako toka pale unapokuwa, utazame pande zote: kaskazini, kusini, mashariki na magaribi. 15 Inchi hii yote unayoona nitakupa wewe na wazao wako ikuwe yenu milele. 16 Wazao wako nitawafanya wakuwe wengi wasihesabike, kama vile mavumbi ya inchi. Kama vile vumbi isivyoweza kuhesabika, ndivyo wazao wako hawataweza kuhesabika! 17 Basi, simama uitembelee inchi hii katika upana na urefu, maana nitakupa wewe inchi ile.” 18 Kwa hiyo, Abramu akaongoa hema, akakwenda kukaa karibu na mielo ya Mamure kule Hebroni. Kule akajengea Yawe mazabahu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo