Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mwanzo 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Kuumbwa kwa ulimwengu

1 Hapo mwanzo, Mungu aliumba mbingu na dunia.

2 Dunia ilikuwa bila umbo na tupu. Giza lilikuwa limefunika vilindi vya maji na roho wa Mungu alikuwa akitanda juu ya maji.

3 Mungu akasema: “Mwangaza ukuwe.” Mwangaza ukakuwa.

4 Mungu akaona kwamba mwangaza ule ni muzuri. Kisha Mungu akatenganisha mwangaza na giza.

5 Mwangaza akauita “Muchana” na giza akaliita “Usiku”. Ikakuwa magaribi na kisha ikakuwa asubui, ndiyo siku ya kwanza.

6 Mungu akasema: “Anga likuwe katikati ya maji, litenge maji sehemu mbili.”

7 Ikakuwa hivyo. Mungu akafanya anga, akatenga maji yanayokuwa juu ya anga na yale yanayokuwa chini ya anga lile.

8 Mungu akaliita anga “Mbingu”. Ikakuwa magaribi na kisha ikakuwa asubui, ndiyo siku ya pili.

9 Mungu akasema: “Maji yanayokuwa chini ya mbingu yakusanyike pahali pamoja, inchi kavu itokee.” Ikakuwa hivyo.

10 Mungu akapaita pahali pakavu “Inchi” na kusanyiko la maji akaliita “Bahari”. Mungu akaona kwamba ni vizuri.

11 Kisha Mungu akasema: “Inchi ioteshe mimea: mimea inayozaa mbegu, na miti inayozaa matunda yenye mbegu za aina yake.” Ikakuwa hivyo.

12 Inchi ikaotesha mimea inayozaa mbegu za aina yake, na miti inayozaa matunda yenye mbegu za aina yake. Mungu akaona kwamba ni vizuri.

13 Ikakuwa magaribi na kisha ikakuwa asubui, ndiyo siku ya tatu.

14 Mungu akasema: “Miangaza ikuwe katika anga, itenge muchana na usiku. Ikuwe vitambulisho kwa kuonyesha nyakati, siku na miaka,

15 na iangae katika anga na kuangazia dunia.” Ikakuwa hivyo.

16 Mungu akafanya miangaza miwili mikubwa: ule mukubwa utawale muchana na ule mudogo utawale usiku. Akafanya nyota vilevile.

17 Mungu akaweka miangaza ile katika anga iangazie dunia,

18 ipate kutawala muchana na usiku, na kutenga mwangaza na giza. Mungu akaona kwamba ni vizuri.

19 Ikakuwa magaribi na kisha ikakuwa asubui, ndiyo siku ya ine.

20 Mungu akasema: “Maji yajae makundi ya viumbe vyenye uzima. Na ndege waruke katika anga.”

21 Mungu akaumba nyama wakubwa sana wa bahari na aina zote za viumbe vyenye uzima vinavyotembea ndani ya maji. Akaumba aina zote za ndege. Mungu akaona kwamba ni vizuri.

22 Mungu akavibariki, akasema: “Muzae, muongezeke, mujaze maji ya bahari, nao ndege waongezeke katika inchi.”

23 Ikakuwa magaribi na kisha ikakuwa asubui, ndiyo siku ya tano.

24 Mungu akasema: “Inchi itoe aina zote za viumbe vyenye uzima: nyama wa kufugwa, viumbe vinavyotambaa na nyama wa pori wa kila aina.” Ikakuwa hivyo.

25 Mungu akafanya aina zote za nyama wa pori, nyama wa kufugwa, na viumbe vinavyotambaa. Mungu akaona kwamba ni vizuri.

26 Kisha Mungu akasema: “Tumufanye mutu kwa mufano wetu, anayefanana nasi, atawale samaki wa bahari, ndege wa anga, nyama wa kufugwa, dunia yote na viumbe vyote vinavyotambaa.”

27 Mungu akaumba mutu kwa mufano wake. Ndiyo, kwa mufano wake Mungu alimwumba. Aliwaumba mwanaume na mwanamuke.

28 Mungu akawabariki na kuwaambia: “Muzae, muongezeke, na mujaze inchi na kuitawala. Mutawale samaki wa bahari, ndege wa anga, na kila kiumbe chenye uzima kinachotembea katika dunia.”

29 Kisha Mungu akasema: “Ninawapa kila mumea katika dunia unaozaa mbegu na kila muti unaozaa matunda yenye mbegu, kwa ajili ya chakula chenu.

30 Nao nyama wote katika dunia, ndege wote wa anga, viumbe vyote vinavyotambaa, kila kiumbe chenye uzima, chakula chao kitakuwa majani yote ya mimea.” Ikakuwa hivyo.

31 Mungu akaona kwamba kila kitu alichofanya ni kizuri kabisa. Ikakuwa magaribi na kisha ikakuwa asubui, ndiyo siku ya sita.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan