Mika 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Malalamiko ya nabii 1 Ole wangu! Mimi ninakuwa kama muvunaji kisha wakati wa mavuno; hakuna tini za kwanzakwanza ninazotamani. Ni kama wakati wa kuchuma zabibu: hakuna hata fungu moja la zabibu la kula! 2 Hakuna mutu mwaminifu kwa Mungu aliyebaki katika inchi, hakuna mutu yeyote mwenye usawa kati ya watu. Kila mumoja anavizia kumwanga damu; kila mumoja anamwinda mwenzake kusudi amunase. 3 Wote ni wafundi wa kutenda maovu; waongozi na waamuzi wanaomba kituliro. Wakubwa wanaonyesha wazi nia zao mbaya, nao wanashirikiana pamoja kwa kuzitimiza. 4 Mutu muzuri zaidi kati yao ni kama michongoma, naye mwenye usawa zaidi ni hatari kama upango wa miiba. Siku iliyongojewa ya azabu yao imefika. Na sasa mahangaiko yamewapata. 5 Usimwaminie mwenzako, wala usimutumainie rafiki yako. Chunga mudomo wako, usimwambie kitu muke wako wewe mwenyewe. 6 Maana, mutoto mwanaume anamuzarau baba yake; mutoto mwanamuke anabishana na mama yake, muke wa mwana anapingana na mama mukwe wake. Waadui wa mutu ni watu wa nyumba yake. 7 Lakini mimi ninamutumainia Yawe, ninamutazamia Mungu mwenye kuniokoa; Mungu wangu atanisikiliza. Tumaini na maombi ya watu 8 Usifurahie hali yangu ewe adui yangu! Nikianguka, nitasimama tena; nikiwa katika giza, Yawe ni mwangaza wangu. 9 Kwa vile nimemukosea Yawe, nitavumilia kasirani yake, mpaka atakapotetea maneno yangu na kunijalia haki yangu. Atanileta inje kwenye mwangaza, nami nitaona akisimamisha haki. 10 Halafu adui yangu ataona hayo naye atafunikwa na haya; maana aliniambia: Basi Yawe, Mungu wako, yuko wapi? Mimi mwenyewe nitamwona adui akianguka; atakanyagwakanyagwa chini kama matope katika njia. 11 Siku inakuja ambapo kuta za muji wenu zitajengwa upya. Siku hiyo mipaka ya inchi yenu itapanuliwa. 12 Siku hiyo wandugu zenu watawarudilia, kutoka Asuria na vijiji vya Misri, kutoka inchi ya Misri na eneo la muto Furati; kutoka sehemu za maji na sehemu za milima. 13 Lakini inchi yote nyingine itakuwa jangwa, kwa sababu ya uovu wa wakaaji wake. Maombi 14 Ee Mungu, uwachunge watu wako kwa fimbo yako, uwachunge wale wanaokuwa kundi lako mwenyewe ambao wanaishi peke yao katika pori na kuzungukwa na inchi yenye mboleo. Uwachunge kama ulivyofanya pale zamani katika shamba la malisho ya Basani na Gileadi. 15 Kama wakati ulipotutoa toka katika inchi ya Misri, utuonyeshe tena maajabu yako. 16 Nao watu wa mataifa watakapoona hayo, watafezeheka hata kama wana nguvu. Watapigwa na bumbuazi na kukosa cha kusema na kuwa kama viziwi. 17 Watatambaa katika mavumbi kama nyoka, kama viumbe vinavyotambaa. Watatoka katika makimbilio yao wakitetemeka na kujaa hofu. Watakugeukia Yawe, Mungu wetu, kwa hofu, wataogopa kwa sababu yako. 18 Ee Mungu, ni nani anayekuwa kama wewe? Wewe unasemehe zambi za watu wako waliobaki, wala hauyaangalii makosa yao. Hasira yako haidumu milele, lakini unapendelea zaidi kutuonyesha wema wako. 19 Utatuhurumia tena; utatupilia mbali zambi zetu, utazitupa zote katika vilindi vya bahari. 20 Utatuonyesha uaminifu na wema wako sisi wazao wa Abrahamu na wa Yakobo, kama ulivyowaahidi babu zetu tangu zamani. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo