Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mika 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002

1 Hili ni neno la Yawe lilomufikia Mika, wa muji wa Moreseti wakati Yotamu, Ahazi na Hezekia walipokuwa wafalme wa Yuda. Mika aliona mambo yote haya juu ya Samaria na Yerusalema.


Yawe anakuja kuhukumu

2 Musikilize enyi watu wote; sikiliza ewe dunia na vyote vinavyokuwa ndani yako. Bwana wetu Yawe anakuja kuwashitaki, Bwana wetu anasema kutoka hekalu lake takatifu.

3 Kweli, anakuja kutoka makao yake; atashuka na kutembea juu ya vilele vya dunia.

4 Milima itayeyuka chini ya miguu yake, kama inta karibu na moto; mabonde yatapasuka, kama vile maji yanayoporomoka kwenye muteremuko.

5 Haya yote yatatukia kwa sababu ya makosa ya wazao wa Yakobo, kwa sababu ya zambi za wazao wa Israeli. Kosa la Yakobo linaonekana wapi? Katika muji wake mukubwa Samaria! Kosa la Yuda linaonekana wapi? Katika Yerusalema kwenyewe!

6 Kwa hiyo, anasema hivi: Muji wa Samaria nitaufanya kuwa mabomoko katika mbuga, shamba ambalo watu watapanda mizabibu. Mawe yaliyoujenga nitayatupa ndani ya bonde, na misingi yake nitaichimbuachimbua.

7 Sanamu zake zote zitavunjwavunjwa, kila kitu kilichochumwa kitateketezwa kwa moto. Nitaharibu sanamu za miungu yake yote. Zililundikwa kutokana na mushahara wa ukahaba, nazo zitatumiwa tena kuwa mushahara wa ukahaba.

8 Kwa sababu hiyo, mimi nitalia na kuomboleza; nitatembea uchi na bila viatu. Nitaomboleza na kulia kama mbweha, nitasikitika na kulia kama mbuni.

9 Vidonda vya Samaria haviwezi kupona, navyo vimeipata vilevile inchi ya Yuda; vimefikia kwenye mulango wa Yerusalema, pahali watu wangu wanapokaa.

10 Musiitangaze habari hii kule Gati, wala musilie machozi! Kule Beti-Leafura mugaegae katika mavumbi kwa huzuni.

11 Enyi wakaaji wa Safiri, muende mukiwa uchi na wenye haya. Wakaaji wa Zanana musitoke inje ya muji wenu. Watu wa Beti-Ezeli wanalia; musaada wao kwenu umeondolewa.

12 Wakaaji wa Maroti wanangojea musaada kwa hamu kubwa, lakini maangamizi yanakuja kutoka kwa Yawe karibu kabisa na mulango wa Yerusalema.

13 Enyi wakaaji wa Lakisi, mufunge farasi wepesi na magari ya vita. Ninyi mulikuwa mumeiga zambi ya watu wa Sayuni, makosa ya Waisraeli yalikuwa kwenu.

14 Hivyo, munapaswa kuwaacha wakaaji wa Moreseti-Gati. Nao muji wa Akizibu hautawasaidia wafalme wa Israeli kwa kitu chochote.

15 Enyi wakaaji wa Maresa, Mungu atawaletea tena adui atakayewateka. Waongozi waheshimiwa wa Israeli watakimbilia ndani ya pango kule Adulamu.

16 Enyi watu wa Yuda, munyoe vichwa vyenu kwa kuwaomboleza watoto wenu wapenzi; mupanue upaa wenu ukuwe mupana kama wa tai, maana watoto wenu watawaacha kwenda katika uhamisho.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan