Mezali 8 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Wito wa Hekima 1 Musikilize! Hekima inaita! Akili inapiga kelele yake! 2 Juu kwenye vilima karibu na njia na katika masanganjia ndipo ilipojiweka. 3 Karibu na milango ya kuingilia katika muji, pahali wanapoingilia watu inaita kwa sauti: 4 “Enyi watu wote, ninawaita ninyi! Wito wangu ni kwa ajili ya wanadamu. 5 Enyi wajinga, mujifunze kuwa na akili; musikilize kwa uangalifu, enyi wapumbafu. 6 Musikilize maana nitakachosema ni jambo la lazima; katika midomo yangu mutatoka mambo ya haki. 7 Kinywa changu kitasema kweli mutupu; uovu ni chukizo katika midomo yangu. 8 Kinywa changu kitasema maneno ya haki, hakuna udanganyifu wala upotevu katika midomo yangu. 9 Kwa mutu mwenye ufahamu kila kitu ni wazi, kwa mwenye maarifa yote imesawanishwa. 10 Chagua mafundisho yangu pahali pa feza; na maarifa pahali pa zahabu safi. 11 “Hekima ina maana sana kuliko mawe ya bei kali; kitu chochote unachotamani hakiwezi kulingana nayo. 12 Mimi Hekima nina ujuzi; nina maarifa na akili. 13 Kumwogopa Yawe ni kuchukia uovu. Ninachukia kiburi, majivuno maisha mabaya, na luga mbaya. 14 Nina uwezo wa kushauri na kuamua vizuri. Nina ufahamu na nina nguvu. 15 Kwa musaada wangu watawala wanatawala na wakubwa wanaagiza kwa haki. 16 Kwa musaada wangu viongozi wanaongoza na wakubwa wanaamua. 17 Ninawapenda wale wanaonipenda; wanaonitafuta kwa bidii wananipata. 18 Utajiri na heshima viko kwangu, mali ya kudumu na fanaka. 19 Matunda yangu ni mazuri kuliko zahabu safi, na faida yangu inashinda ya feza bora. 20 Ninatembea katika njia ya haki; ninafuata sheria ya Mungu. 21 Ninawatajirisha wale wanaonipenda, ninajaza tele hazina za wanaonipenda. 22 “Yawe aliniumba kwa mwanzo wa kazi yake, zamani za kale mbele ya kuumbwa kwa kitu chochote. 23 Nilifanywa kwa mwanzo wa nyakati, nilikuwa niko mbele ya dunia kuanza. 24 Nilizaliwa mbele ya vilindi vya bahari, mbele ya chemichemi zinazobubujika maji. 25 Nilizaliwa mbele milima na vilima havijaumbwa, 26 mbele Mungu hajaumba dunia na mashamba yake, wala chembe za kwanza za mavumbi ya dunia. 27 Nilikuwa niko wakati alipoweka mbingu, wakati alipofanya muviringo juu ya bahari; 28 wakati alipoimarisha mawingu mbinguni, alipofanya imara chemichemi za bahari, 29 wakati alipowekea bahari mupaka wake kusudi maji yake yasipate kuvunja amri yake, wakati alipoweka misingi ya dunia. 30 Nilikuwa pamoja naye kama fundi wa kazi, nilikuwa furaha yake kila siku, nikishangilia mbele yake siku zote, 31 nikifurahia dunia na wakaaji wake, na kupendezwa kuwa pamoja na wanadamu. 32 “Sasa basi, wana wangu, munisikilize: heri wale wanaofuata njia zangu. 33 Musikilize mafundisho mupate hekima, wala musiyakatae. 34 Heri mutu anayenisikiliza, anayeikaa kila siku kwenye mulango wangu, anayekesha karibu na milango yangu. 35 Anayenipata mimi amepata uzima, na upendeleo kutoka kwa Yawe. 36 Asiyenipata anajizuru mwenyewe; wote wanaonichukia wanapenda kifo.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo