Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mezali 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002

1 Mwana wangu, ushike maneno yangu, uchunge amri zangu.

2 Ufuate amri zangu nawe utaishi; ulinde mafundisho yangu kama mboni ya jicho lako.

3 Uyafunge kwenye vidole vyako; uyaandike ndani ya moyo wako.

4 Uambie Hekima: “Wewe ni dada yangu”, na Akili: “Wewe ni rafiki yangu”.

5 Vitakulinda mbali na mwanamuke mubaya, vitakuepusha na maneno matamu ya mwanamuke mugeni.

6 Siku moja katika dirisha ya nyumba yangu, nilichungulia inje kupitia nyavu za dirisha,

7 nikawaona vijana wengi wajinga, na hasa mumoja aliyekuwa mupumbafu.

8 Huyo alikuwa akitembea kwenye barabara ile, karibu na pahali mwanamuke mumoja alipoishi. Basi akashika njia inayokwenda kwa mwanamuke yule.

9 Ilikuwa karibu wakati wa magaribi, giza na usiku vilikuwa vimeanza kuingia.

10 Kijana akakutana na yule mwanamuke; alivaa kama kahaba, mwenye ukorofi.

11 Alikuwa mwanamuke wa makelele na mwenye kiburi; miguu yake haitulii ndani ya nyumba:

12 mara katika barabara, mara katika soko, pembeni ya njia hakosekani akivizia.

13 Alimukumbatia kijana yule na kumubusu, na kwa maneno matamu, akamwambia:

14 “Ilinipasa kutoa sadaka zangu; leo hii nimekamilisha naziri yangu.

15 Ndio maana nimetoka kwa kukupokea, nimekutafuta kwa hamu nikakupata.

16 Nimetandika kitanda changu vizuri, kwa blanketi za rangi za kitani kutoka Misri.

17 Nimekinyuzia marasi, manemane, udi na mudalasini.

18 Kuja! Tufanye mapenzi mpaka asubui; kuja tujifurahishe kwa mapenzi.

19 Mume wangu hayuko ndani ya nyumba, amekwenda safari ya mbali.

20 Amepeleka mufuko wa feza, hatarudi mbele ya mwandamo wa mwezi.”

21 Alimushawishi kwa maneno mengi ya kubembeleza; kijana akashawishiwa kwa maneno yake matamu.

22 Naye akamufuata yule mwanamuke moja kwa moja, kama ngombe anayekwenda kuchinjwa, kama mupambafu anayefungwa na kwenda kuazibiwa.

23 Hakutambua kwamba maisha yake yako katika hatari, mpaka alipojikuta amekuwa kama amechomwa mushale ndani ya moyo, amekuwa kama ndege aliyerukia ndani ya wavu.

24 Sasa wana wangu, munisikilize; mutege sikio kwa maneno ya kinywa changu.

25 Musikubali kuongozwa na mwanamuke kama yule, wala musipitepite katika mapito yake.

26 Maana amewaangusha wanaume wengi; ni wengi sana wale aliowachinja.

27 Nyumba yake ni njia ya kwenda kuzimu, ni pahali pa kuteremukia katika mauti.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan