Mezali 6 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maonyo mane 1 Mwana wangu, kama umejitolea kubeba deni ya mwenzako, ikiwa umetoa ahadi yako kwa ajili ya mutu yule, 2 ikiwa umejifunga kwa maneno yako mwenyewe, utajinasa kwa ahadi uliyofanya; 3 ujue kwamba uko chini ya mamlaka ya mwenzako, lakini mwana wangu, ukitaka kujiokoa, basi fanya hivi: umwendee mutu yule mara moja, umusihi akupe uhuru wako. 4 Usiache macho yako yapate usingizi, wala kope za macho yako zisinzie. 5 Ujiokoe kwa kujitoa katika mutego ule, ujiponyeshe kama vile paa au ndege anayemutoroka mwindaji. 6 Ewe muvivu! Kwenda kuchunguza siafu, fikiri juu ya namna yake ya kuishi upate hekima. 7 Siafu hana kiongozi, mukubwa, wala mutawala; 8 lakini anajiwekea chakula wakati wa kipwa, anajikusanyia akiba wakati wa mavuno. 9 Ewe muvivu, utalala pale mpaka wakati gani? Utaamuka wakati gani katika usingizi wako? 10 Unasema: “Acha nilale kidogo tu, acha nisinzie kidogo! Uniache nikunje mikono nipumzike kidogo!” 11 Wakati ule umasikini utakushambulia kama munyanganyi, ukosefu utakufuata kama mwizi mwenye silaha. 12 Mutu mwovu, mutu asiyefaa kitu, anatangatanga akisema maneno mapotovu. 13 Anakonyeza jicho kwa kuwakosesha wengine, anaparuza kwa miguu na kufanyia watu kitambulisho kwa vidole. 14 Akiwa amejaa mabaya ndani ya moyo, anatunga maovu. Anaamusha ugomvi kila pahali. 15 Kutokana na hayo hasara itamupata kwa rafla; kwa rafla atapondekana vibaya wala hatapata kupona. 16 Kuna vitu sita Yawe anavyochukia, hata saba ambavyo ni chukizo kwake: 17 Macho ya kiburi, ulimi mudanganyifu, mikono inayoua wasiokuwa na kosa, 18 moyo unaopanga mipango miovu, miguu inayokuwa mbio kutenda maovu, 19 mushuhuda wa uongo anayesema uongo, na mutu anayechochea fitina kati ya wandugu. Maonyo juu ya uasherati 20 Mwana wangu, shika amri za baba yako, wala usisahau mashauri ya mama yako; 21 uyaweke siku zote ndani ya moyo, uyafunge katika shingo lako. 22 Yatakuongoza katika njia yako, yatakulinda wakati unapolala, yatakushauria unapoamuka. 23 Maana amri hizi ni taa, na shauri hilo ni mwangaza. Maonyo hayo ya mafundisho ni njia ya uzima. 24 Yatakulinda mbali na mwanamuke mubaya, yatakuepusha na maneno matamu ya mwanamuke mugeni. 25 Usimutamani mwanamuke yule kwa uzuri wake, wala usikubali kunaswa kwa kope za macho yake. 26 Mutu anapoteza kipande cha mukate kwa kahaba, lakini mwanamuke muzinzi atapoteza uzima wako wote. 27 Mutu anaweza kuweka moto kwenye kifua chake na nguo zake zikose kuungua? 28 Mutu anaweza kukanyaga makaa ya moto na miguu yake ikose kuungua? 29 Ndivyo mwanaume anayelala na muke wa mwenzake anavyokuwa; yeyote anayemugusa mwanamuke yule hataacha kuazibiwa. 30 Watu hawamuzarau sana mutu akiiba kwa sababu ya njaa, 31 lakini akipatikana anapaswa kulipa mara saba, tena atatoa mali yote anayokuwa nayo. 32 Anayezini hana akili kabisa; anajiangamiza yeye mwenyewe. 33 Atapata vidonda na mazarau; haya atakayopata haitatoka juu yake. 34 Maana wivu wa mume unamufanya kuwa mukali kabisa; wakati atakapolipiza kisasi hana kitu cha kuhurumia. 35 Hatakubali malipo yoyote; wala kutulizwa na zawadi zako nyingi. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo