Mezali 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mafaa ya hekima 1 Wana wangu, musikilize maadibisho ya baba yenu, mutege sikio mupate kuwa na akili. 2 Maana ninawapa kanuni zuri, musikatae mafundisho yangu. 3 Mimi vilevile nilikuwa mutoto kwa baba yangu, nilikuwa mupole, kipenzi cha mama yangu. 4 Baba yangu alinifundisha hiki: “Shika kwa moyo maneno yangu, shika amri zangu nawe utaishi. 5 Ujipatie hekima, ujipatie ufahamu; usisahau wala kuzarau maneno yangu. 6 Usimwache hekima, nayo itakutunza; umupende, nayo itakulinda. 7 Jambo la musingi ni kujipatia hekima; toa vyote unavyokuwa navyo ujipatie akili. 8 Shikamana sana na hekima, nayo itakutukuza; ukiishikilia itakupa heshima. 9 Itavalisha kilemba cha neema kwenye kichwa chako, atakupa taji lenye utukufu.” 10 Mwana wangu, sikia na kupokea maneno yangu, kusudi upate kuwa na miaka mingi ya kuishi. 11 Nimekufundisha njia ya hekima, nimekuongoza katika njia ya usawa. 12 Ukitembea hatua zako hazitazuizwa, wala ukikimbia hautajikwaa. 13 Shika mafundisho ya hekima na usimwache iponyoke, uishike kwa uangalifu maana ni uzima wako. 14 Usijiingize katika njia ya waovu, wala usifuate mwenendo wa watu wabaya. 15 Epuka njia hiyo wala usiikaribie; ujiepushe nayo, uende zako. 16 Waovu hawalali hata kidogo wasipotenda uovu; hawapati usingizi wasipomukwaza mutu. 17 Maana uovu ndicho chakula chao, mateso makali ndiyo divai yao. 18 Njia ya wenye haki ni kama mwangaza wa asubui mapema, ambao unaangaza zaidi na zaidi hata muchana kamili. 19 Lakini njia ya waovu ni kama giza nene, hawajui kinachowafanya wajikwae. 20 Mwana wangu, sikia kwa uangalifu maneno yangu, utegee sikio masemi yangu. 21 Usiyaache yatoweke mbele ya macho, uyafunge ndani ya moyo wako. 22 Maana hayo ni uzima kwa mutu anayeyapata, ni dawa kwa mwili wake wote. 23 Linda moyo wako kwa uangalifu wote, maana mule munatokea chemichemi za uzima. 24 Tenga mbali nawe luga potovu; wala midomo yako isiseme maneno madanganyifu. 25 Uyaelekeze macho yako mbele sawasawa, kope zako zipige sawasawa. 26 Chunguza sana njia utakayopitia, na hatua zako zote zitakuwa kamili. 27 Usigeukie kuume wala kushoto; epusha muguu wako mbali na uovu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo