Mezali 30 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maneno ya Aguri 1 Maneno ya Aguri mwana wa Yake. Maneno ambayo mutu huyu alimwambia Itieli na Ukali. 2 Mimi ni mupumbafu sana, wala si mutu; sina akili ya mwanadamu. 3 Sijajifunza hekima, wala sijui kitu juu ya Mungu Mutakatifu. 4 Ni nani aliyepanda juu mbinguni na kushuka chini? Ni nani aliyekamata upepo katika mukono? Ni nani aliyefunga maji katika kitambaa? Ni nani aliyeweka mipaka yote ya dunia? Jina lake ni nani? Na ni nani jina la mwana wake? Uniambie kama unajua! 5 Maneno yote ya Mungu ni ya kuaminiwa. Yeye ni ngao yao wote wanaomukimbilia. 6 Usiongeze neno katika maneno yake, kusudi asikukaripie, nawe usionekane kuwa mwongo. 7 Ee Mungu, ninakuomba mambo haya mawili, wala usikatae kunitimizia nayo mbele ya kufa kwangu: 8 Uniondolee uongo na udanganyifu; usinipe umasikini wala utajiri; unipatie chakula ninachohitaji, 9 maana nikipata mali mengi nitakusahau; nikisema: “Yawe ni nani?” Au nikiwa masikini nitaiba, na kuzaraulisha jina lako ee Mungu wangu. 10 Usimuchongee mutumwa kwa bwana wake, kusudi asikulaani, na kuonekana kwamba uko na kosa. 11 Kuna watu ambao wanalaani baba zao, wala hawana shukrani kwa mama zao. 12 Kuna watu ambao wanajiona kuwa safi, kumbe bado hawajatakaswa uchafu wao. 13 Kuna watu ambao macho yao yanajaa kiburi. Wanazarau kila kitu wanachoona. 14 Kuna watu ambao meno yao ni kama upanga, na mataya yao ni kama visu. Wako tayari kuwatafuna wamasikini wa inchi, na wakosefu wanaokuwa kati ya watu! 15 Muruba ana wabinti wawili wanaosema: “Unipe, Unipe!” Kuna vitu vitatu ambavyo havishibi hata kidogo, hata vitu vine visivyosema: “Inatosha!” 16 Kuzimu, tumbo la mwanamuke tasa, udongo usioshiba maji, na moto usiosema: “Inatosha!” 17 Kama mutu akimuchekelea baba yake na kuzarau utii kwa mama yake, macho yake yataondolewa na kibombobombo wa pori na kuliwa na tai. 18 Kuna mambo matatu yanayokuwa ya ajabu kwangu, hata mambo mane nisiyoyaelewa: 19 njia ya tai katika anga, njia ya nyoka juu ya jiwe, njia ya mashua ndani ya bahari, na njia ya mwanaume kwa mwanamuke. 20 Mwenendo wa mwanamuke mwasherati ni hivi: yeye anakula, anajipanguza mudomo, na kusema: “Sijafanya kosa lolote!” 21 Kuna mambo matatu ambayo yanaitetemesha dunia, hata mambo mane ambayo haiwezi kuyavumilia: 22 mutumwa anayekuwa mufalme; mupumbafu anayeshiba chakula; 23 mwanamuke asiyependwa anayeolewa; na mujakazi anapotwaa nafasi ya bibi yake. 24 Kuna viumbe vine vidogo sana katika dunia, lakini vina akili sana: 25 siafu ni wadudu wasiokuwa na nguvu, lakini wanajiwekea chakula wakati wa kipwa; 26 sungura ni nyama wasiokuwa na uwezo, lakini wanajitengenezea makao chini ya mawe; 27 nzige hawana mufalme, lakini wote wanaenda pamoja kwa vikundi; 28 mujusi, unaweza kumushika katika mukono, lakini anaingia katika nyumba ya kifalme. 29 Kuna viumbe vitatu vyenye mwendo wa kupendeza, hata viumbe vine vyenye mwendo muzuri: 30 simba, ambaye ni nyama mwenye nguvu kuliko wote wala hamwogopi nyama mwingine yeyote, 31 jogoo anayetembea kwa maringo, beberu, na mufalme mbele ya watu wake. 32 Kama umekuwa mupumbafu hata ukajisifu, au kama umekuwa unapanga maovu, chunga mudomo wako. 33 Maana ukigandisha maziwa, utapata siagi; ukimupiga mutu kwenye pua, atatoka damu. Vilevile kuchochea hasira kunaleta ugomvi. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo