Mezali 26 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Heshima anayopewa mupumbafu haifai. Ni kama teluji ya wakati wa kipwa, au mvua ya wakati wa mavuno. 2 Kama vile ndege anavyorukaruka, vilevile laana isiyokuwa na sababu haimupati mutu. 3 Kiboko ni kwa farasi, lijamu ni kwa punda, na fimbo ni kwa mugongo wa mupumbafu. 4 Usimujibu mupumbafu kipumbafu, kusudi usifanane naye. 5 Umujibu mupumbafu kama kufuatana na upumbafu wake, kusudi asijione kuwa mwenye hekima zaidi. 6 Kutuma ujumbe kwa mukono wa mupumbafu ni kama kujikata miguu au kujitafutia mateso. 7 Mezali katika midomo ya mupumbafu ni kama miguu ya kiwete inayoninginia. 8 Kumupa mupumbafu heshima ni kama kufunga jiwe kwenye mujeledi. 9 Mezali katika kinywa cha mupumbafu ni kama tawi lenye miiba katika mukono wa mulevi. 10 Mutu anayemulipa mupumbafu au mulevi kusudi amutumikie, ni kama mupiga upinde anayeumiza kila mutu. 11 Mupumbafu anayerudiliarudilia upumbafu wake ni kama imbwa anayekula matapiko yake. 12 Unamwona mutu anayejiona kuwa mwenye hekima? Afazali kumutumainia mupumbafu kuliko yule. 13 Muvivu anasema: “Kuna simba kali inje. Kuna simba katika njia.” 14 Kama vile mulango unavyozunguka kwenye vyuma vya kuukamatia, ndivyo muvivu anavyogeuka juu ya kitanda chake. 15 Muvivu anatia mukono wake katika sahani, lakini anachoka kwa kuuinua mpaka kwenye mudomo. 16 Muvivu anajiona kuwa mwenye hekima kuliko watu saba wanaoweza kujibu kwa akili. 17 Anayejiingiza katika ugomvi usiomwelekea, ni kama mutu anayeshika masikio ya imbwa anayepita. 18 Kama vile mwenda-wazimu anavyotupa mienge ya moto, mishale, na kifo, 19 ndivyo mutu ambaye anadanganya jirani, kisha anasema: “Nilikuwa ninafanya muzaha tu!” 20 Bila kuni, moto unazimika; bila mwenye kuchochea, ugomvi unamalizika. 21 Kama vile makaa au kuni vinachochea moto, ndivyo mugomvi anachochea ugomvi. 22 Maneno ya muchongeaji ni kama chakula kitamu; yanashuka mpaka ndani kabisa ya tumbo. 23 Kama vile rangi yenye kungaa iliyopakwa juu ya chungu cha udongo, ndivyo maneno matamu yenye nia mbaya yanavyokuwa. 24 Mwenye chuki anaficha chuki yake kwa maneno mazuri, lakini uovu unajaa ndani ya moyo wake. 25 Akisema maneno mazuri usimwaminie. Ndani ya moyo wake kuna machukizo mengi. 26 Anaweza kuficha chuki yake, lakini nia zake mbaya zitajulikana kwa wote. 27 Anayechimbia mwenzake shimo, anatumbukia ndani mwenyewe; anayewaporomoshea wengine jiwe, litamurudilia mwenyewe. 28 Anayesema uongo anachukia wale anaowaumiza, naye anayebembeleza analeta maangamizi. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo