Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mezali 25 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mezali zingine za Solomono

1 Hizi nazo ni mezali nyingine za mufalme Solomono zilizoandikwa na watu wa Hezekia, mufalme wa Yuda.

2 Mungu anatukuzwa kwa kuficha mambo, lakini wafalme wanatukuzwa kwa kuchunguza mambo.

3 Kama vile mbingu zinavyokuwa mbali juu na dunia mbali chini, ndivyo inavyokuwa vigumu kuelewa akili za mufalme.

4 Toa takataka katika feza, na mufuaji wa vyuma atakutengenezea chombo kizuri.

5 Uwaondoe waovu mbele ya mufalme, na utawala wake utaimarika katika haki.

6 Usijipendekeze kwa mufalme, wala usijifanye mutu mukubwa,

7 maana ni heri kuambiwa: “Kuja huku mbele”, kuliko kuporomoshwa mbele ya mukubwa.

8 Mambo uliyoona kwa macho yako, usiharakishe kuyapeleka katika tribinali; maana utafanya nini kwa mwisho, kama jirani yako anakupatisha haya?

9 Utengeneze ugomvi na mwenzako peke yake, na kila mumoja wenu asitoe siri ya mwenzake;

10 watu wanaokusikia wasikuzarau, nawe usijiharibishie heshima kwa siku zote.

11 Neno linalosemwa kwa wakati unaofaa, ni kama michoro ya zahabu juu ya feza.

12 Onyo la mwenye hekima kwa mutu musikilivu ni bora kuliko pete au ushanga wa zahabu safi.

13 Mujumbe mwaminifu anamufurahia yule aliyemutuma, kama maji ya baridi wakati wa joto la mavuno.

14 Kama vile mawingu na upepo bila mvua, ndivyo anavyokuwa mutu anayeahidi zawadi na haitoi.

15 Kwa uvumilivu mutawala anaweza kusadikishwa; ulimi laini unavunja mifupa.

16 Unapopata asali, kula sehemu ya kukutoshelea, kusudi usishibe na kuitapika.

17 Usimutembelee jirani yako mara kwa mara, kusudi asichoke nawe na kukuchukia.

18 Mutu anayetoa ushuhuda wa uongo juu ya mwenzake, ni hatari kama nyundo, upanga au mushale mukali.

19 Kumutegemea mutu asiyeaminiwa wakati wa taabu, ni kama kutegemea jino zaifu au muguu ulioteguka.

20 Kumwimbia mutu mwenye huzuni ni kama kumuvua nguo wakati wa baridi, au kutia siki katika kidonda.

21 Adui yako akiwa na njaa, umupe chakula; akiwa na kiu, umupe maji ya kunywa.

22 Hivyo utamufezehesha, kama vile kumwanga makaa ya moto juu ya kichwa chake. Yawe atakupa zawadi.

23 Upepo wa kaskazini unaleta mvua; vilevile mwenye kusingiziana analeta chuki.

24 Afazali kuishi pembeni juu ya paa, kuliko kuishi ndani ya nyumba pamoja na mwanamuke mugomvi.

25 Kama vile maji baridi kwa mwenye kiu, ndivyo habari njema kutoka mbali inavyokuwa.

26 Mwenye haki anayekubali kufuata mambo ya mwovu ni chemichemi iliyochafuliwa au kisima kinachotofuliwa.

27 Si vizuri kula asali nyingi sana; vilevile haifai kujipendekeza sana.

28 Mutu asiyeweza kuzuia hasira yake ni kama muji usiokuwa na ulinzi unaposhambuliwa.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan