Mezali 17 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Afazali kula mukate wenye kukauka kwa amani kuliko karamu katika nyumba ya ugomvi. 2 Mutumwa mwenye hekima atatwaa nafasi ya mwana mupumbafu. Atapata sehemu ya urizi wa jamaa hiyo. 3 Zahabu na feza vinapimwa kwa moto, lakini Yawe ndiye anayepima mioyo ya watu. 4 Mutenda maovu anasikiliza maneno mabaya; mwongo anategea sikio ulimi mudanganyifu. 5 Anayechekelea masikini anamutukana Muumba wake; anayefurahia hasara hatakosa kuazibiwa. 6 Taji la sifa la wazee ni wajukuu wao. Heshima ya wana ni baba yao. 7 Maneno mazuri hayastahili katika kinywa cha mupumbafu, zaidi sana maneno ya uongo katika kinywa cha kiongozi! 8 Kwa anayetoa kituliro ni kama hirizi; kila kitu anachofanya yeye anafanikiwa. 9 Anayesamehe makosa anajenga urafiki, lakini anayekumbusha makosa anatenga warafiki. 10 Onyo kwa mwenye akili lina maana, kuliko mapigo mia moja kwa mupumbafu. 11 Nia ya mutu mwovu ni kuasi tu; mujumbe mubaya atatumwa juu yake. 12 Afazali kukutana na dubu dike aliyenyanganywa watoto wake, kuliko kukutana na mupumbafu katika upumbafu wake. 13 Mwenye kulipa mazuri kwa mabaya, mabaya hayataondoka katika nyumba yake. 14 Kuanzisha ugomvi ni kama kufungua maji ya kisima; achana na ugomvi mbele haujafurika. 15 Kumuhesabu mwovu kuwa na haki na kumwazibu asiyekuwa na kosa, yote mawili ni chukizo kwa Yawe. 16 Kwa nini mupumbafu kuwa na feza katika mukono kwa kununua hekima, wakati yeye mwenyewe hana akili? 17 Rafiki wa kweli ni rafiki siku zote. Ndugu anazaliwa kusudi asaidie wakati wa taabu. 18 Mutu asiyekuwa na akili anajitoa rehani kwa deni ya mutu mwingine. 19 Anayependa ugomvi anapenda zambi. Anayejivuna anajitafutia maangamizi. 20 Mwenye moyo mupotovu hafanikiwi, na musema uongo anapatwa na hasara. 21 Mutoto mupumbafu ni huzuni kwa baba yake, na baba wa mupumbafu hana furaha. 22 Moyo wenye furaha ni dawa, lakini moyo wenye huzuni unakondesha mwili. 23 Mutu mubaya anapokea kituliro kwa siri kusudi apate kupotosha haki. 24 Hekima ni mbele ya uso wa mwenye akili, lakini macho ya mupumbafu yanaangalia kwa miisho ya dunia. 25 Mutoto mupumbafu ni huzuni kwa baba yake, na uchungu kwa mama yake muzazi. 26 Si vizuri kumwazibu mutu asiyekuwa na kosa; ni kosa kuwapiga fimbo wenye heshima. 27 Asiyesema sana ana maarifa; mutu mutulivu ni mwenye ufahamu. 28 Hata mupumbafu akinyamaza, anaonekana kuwa na hekima; akifunga kinywa chake anaonekana kuwa mwenye akili. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo