Mezali 16 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Mwanadamu anapanga mipango yake, lakini neno la mwisho ni la Yawe. 2 Matendo yote ya mutu yanaonekana kwake kuwa sawa lakini Yawe anapima nia ya mutu. 3 Tegemea Yawe katika kazi yako, nayo mipango yako itafanikiwa. 4 Yawe ameumba kila kitu kwa kusudi lake, hata waovu kwa ajili ya siku ya maangamizi. 5 Kila mwenye kiburi ni chukizo kwa Yawe. Hakika mutu wa namna hiyo hatakosa kuazibiwa. 6 Kwa wema na uaminifu mutu anaondoa uovu. Kwa kumwogopa Yawe anaepuka ubaya. 7 Yawe akipendezwa na mwenendo wa mutu, anawageuza hata waadui zake kuwa warafiki. 8 Afazali mali kidogo kwa njia ya haki, kuliko mapato mengi kwa njia isiyofuatana na sheria ya Mungu. 9 Mutu anaweza kufanya mipango yake, lakini Yawe anaongoza hatua zake. 10 Mufalme anaamua kwa maongozi toka kwa Mungu. Anapotoa hukumu hapotoki. 11 Mizani na vipimo vya kweli ni vya Yawe. Mawe yote ya kupimia katika mufuko ni kazi yake. 12 Ni chukizo kubwa kwa wafalme kutenda uovu, maana musingi wa mamlaka yao ni haki. 13 Mufalme anapendelea mutu anayesema maneno ya haki. Anamupenda mutu anayesema kwa usawa. 14 Hasira ya mufalme ni kama mujumbe wa kifo; mutu mwenye hekima ataituliza. 15 Uso wa mufalme ukiangaa, kuna uzima; kupendwa naye ni kama wingu la mvua kwa shamba. 16 Kupata hekima ni bora kuliko zahabu; kupata akili ni chaguo bora kuliko feza. 17 Njia ya watu wa usawa ni kujiepusha na uovu; anayechunga njia yake anachunga maisha yake. 18 Kiburi kinatangulia maangamizi; majivuno yanatangulia maanguko. 19 Afazali kuwa munyenyekevu pamoja na masikini, kuliko kugawanyana vitu vya unyanganyi pamoja na wenye kiburi. 20 Anayefikiri sana juu ya neno atafanikiwa. Heri mutu yule anayemutumainia Yawe. 21 Mwenye hekima ndani ya moyo anaitwa mwenye akili; neno la kupendeza linawavuta watu. 22 Hekima ni chemichemi ya uzima kwa yule anayekuwa nayo, lakini upumbafu ni azabu ya wapumbafu. 23 Moyo wa mwenye hekima unamwezesha kusema kwa hekima; unayafanya maneno yake yakuwe ya kuvutia. 24 Maneno mazuri ni kama asali. Ni matamu kwa nafsi na yenye kuupatia mwili afya. 25 Kuna njia mutu anayoona kuwa sawa, lakini kwa mwisho inaongoza kwenye kifo. 26 Njaa inamusukuma mutu kufanya kazi, maana tamaa ya kinywa chake inamupa bidii. 27 Mutu mwovu anapanga kutenda uovu. Maneno yake ni kama moto mukali. 28 Mutu mupotovu anatawanya ugomvi, na muchonganishi anatenganisha warafiki. 29 Mutesaji mukali anamushawishi jirani yake na kumwongoza katika njia mbaya. 30 Anayekonyeza jicho amepanga kutenda maovu; anayekaza midomo amekwisha kutenda mabaya. 31 Kuwa na imvi za uzee ni taji la utukufu; zinapatikana kwa maisha ya haki. 32 Asiyekuwa mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwenye nguvu. Anayetawala nafsi yake ni bora kuliko anayetaka muji. 33 Kura inapigwa kwa kujua yatakayotukia, lakini uamuzi ni wa Yawe. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo