Mezali 14 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Mwanamuke mwenye hekima anajenga nyumba yake, lakini mupumbafu anaibomoa kwa mikono yake mwenyewe. 2 Mwenye mwenendo sawa anamwogopa Yawe, lakini mupotovu anamuzarau Mungu. 3 Ndani ya kinywa cha mupumbafu kunatokea maneno ya kiburi, lakini mwenye hekima analindwa na maneno yake. 4 Bila ngombe wa kulima gala za mutu ni tupu. Mavuno mengi yanapatikana kwa nguvu ya ngombe wa kulima. 5 Mushuhuda mwaminifu hasemi uongo, lakini asiyeaminiwa anabubujika uongo. 6 Mwenye mazarau anatafuta hekima naye haipati, lakini mwenye akili anapata maarifa kwepesi. 7 Ondoka pahali mupumbafu anapokuwa, maana pale anapokuwa hakuna maneno ya hekima. 8 Hekima ya mwenye akili inamwonyesha njia yake, lakini upumbafu wa wapumbafu unawadanganya wenyewe. 9 Wapumbafu wanafurahia zambi, lakini watu wa usawa wanapata rehema kwa Mungu. 10 Moyo unajua uchungu wake wenyewe, wala mugeni hawezi kushiriki furaha yake. 11 Nyumba ya mutu mwovu itabomolewa, lakini hema ya watu wa usawa itaimarishwa. 12 Kuna njia inayozaniwa kuwa sawa, lakini kwa mwisho inaongoza kwenye kifo. 13 Huzuni inaweza kufichwa katika kicheko; nyuma ya furaha kunakuja huzuni. 14 Mutu mupotovu atavuna matunda ya mwenendo wake, naye mutu muzuri atapata malipo ya matendo yake. 15 Mujinga anaamini kila kitu anachoambiwa, lakini mwenye akili anachunguza hatua zake zote. 16 Mwenye hekima ni mwangalifu na anaepuka uovu, lakini mupumbafu hajizuizi wala hana uangalifu. 17 Mwenye kuwaka hasira haraka anatenda kipumbafu, lakini mwenye akili ana uvumilivu. 18 Wajinga wanarizi upumbafu, lakini wenye akili wanalipwa taji ya maarifa. 19 Waovu watapiga magoti mbele ya watu wazuri, watu wabaya kwenye mulango wa wenye haki. 20 Masikini anachukiwa hata na jirani yake, lakini tajiri ana warafiki wengi. 21 Anayemuzarau jirani yake ni mwenye zambi, lakini ana heri yule anayekuwa mwema kwa masikini. 22 Anayepanga kutenda maovu kweli anakosa! Wanaopanga kutenda mazuri watapata mema na uaminifu. 23 Bidii katika kila kazi inaleta faida, lakini maneno matupu yanaleta umasikini. 24 Mali ni taji ya utukufu wa wenye hekima, lakini ujinga ni kitambaa cha wapumbafu. 25 Mushuhuda wa kweli anaokoa maisha, lakini musema uongo ni mudanganyifu. 26 Anayemwogopa Yawe ana tumaini imara, na watoto wake watapata kimbilio salama. 27 Kumwogopa Yawe ni chemichemi ya uzima inayowezesha mutu kuepuka mitego ya kifo. 28 Utukufu wa mufalme ni wingi wa watu wake, lakini bila watu mutawala anaangamia. 29 Mutu asiyekuwa mwepesi wa hasira ana akili nyingi, lakini anayekasirika upesi anaongeza upumbafu. 30 Amani ndani ya roho inamupa mutu afya, lakini wivu inaozesha mifupa. 31 Anayemutesa muzaifu anamutukana Muumba wake, lakini anayemwonea huruma mukosefu anamutukuza Mungu. 32 Mwovu anaangamizwa kwa matendo yake maovu, lakini mwenye haki atapata usalama kwa uaminifu wake. 33 Hekima iko ndani ya moyo wa mutu mwenye akili, lakini haipatikani hata kidogo ndani ya moyo wa mupumbafu. 34 Haki inainua taifa, lakini zambi ni haya kwa taifa lote. 35 Mufalme anapendezwa na mutumishi anayetenda kwa hekima, lakini hasira yake inawapata wanaotenda mambo yasiyofaa. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo