Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mezali 13 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002

1 Mutoto mwenye hekima anasikia maagizo ya baba yake, lakini mwenye kiburi hasikilizi maonyo.

2 Mutu muzuri anapata uzuri kutokana na maneno yake, lakini mudanganyifu anaishi kwa kutesa kwa ukali.

3 Anayechunga kinywa chake analinda maisha yake, mwenye midomo mirefu anajiletea maangamizi.

4 Muvivu anatamani lakini hapati kitu chochote, wakati mwenye bidii anajaliwa kwa wingi.

5 Mwenye haki anachukia uongo, lakini mwovu anatenda kwa kupatisha haya na mazarau.

6 Haki inalinda wenye mwenendo sawa, lakini zambi inaangusha waovu.

7 Kuna mutu anayejidai kuwa tajiri, kumbe hana kitu. Mwengine anajiona kuwa masikini wakati ana mali tele.

8 Ukombozi wa uzima wa mutu ni mali yake, lakini masikini hana njia ya kujikomboa.

9 Mwenye haki anaangaa kama vile taa inayowaka vizuri, lakini waovu ni kama taa inayozimika.

10 Kiburi kinasababisha tu ugomvi, lakini kwa wanaokubali shauri jema kuna hekima.

11 Mali ya harakaharaka inatoweka, lakini anayekusanya kidogokidogo ataiongeza.

12 Tumaini la kungojangoja linaumiza moyo, lakini tazamio linalotimia ni musingi wa uzima.

13 Anayezarau mashauri anajiletea maangamizi, lakini anayetii amri atapewa zawadi.

14 Mafundisho ya wenye hekima ni chemichemi ya uzima; inamwezesha mutu kuepuka mitego ya kifo.

15 Kuwa na akili kunaleta ukubali, lakini njia ya waovu ni ya taabu.

16 Mwenye akili anatenda kila kitu kwa kufikiri, lakini mupumbafu anatembeza upumbafu wake.

17 Mujumbe mubaya anawatumbukiza watu katika taabu, lakini mujumbe mwaminifu analeta amani.

18 Umasikini na mazarau vinamupata yule asiyejali mafundisho, lakini mwenye kusikia maonyo anaheshimiwa.

19 Ni jambo la kufurahisha unapopata kile unachotaka, kwa hiyo wapumbafu wanachukia kuepuka uovu.

20 Anayeandamana na wenye hekima anapata hekima, lakini anayejiunga na wapumbafu atapata hasara.

21 Wanaotenda zambi wanapatwa na hasara, lakini wenye haki wanafanikiwa.

22 Mutu muzuri anawaachia wazao wake urizi, lakini mali ya mwenye zambi imelundikiwa wenye haki.

23 Shamba la masikini linatoa mazao mengi, lakini linanyanganywa juu ya wale wanaopotosha haki.

24 Asiyemwazibu mutoto wake hamupendi; lakini anayemupenda mwana wake atamwazibu kwa wakati.

25 Mwenye haki yuko na chakula cha kumutoshelea, lakini tumbo la waovu linataabika kwa njaa.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan