Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mezali 10 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mezali za Solomono Mwanamuke mwasherati

1 Hizi ni mezali za Solomono: Mutoto mwenye hekima ni furaha ya baba yake; lakini mutoto mupumbafu ni huzuni ya mama yake.

2 Mali iliyopatikana kwa njia mbaya haifai, lakini haki inaokoa mutu kutoka kifo.

3 Yawe hawaachi wenye haki wapate njaa, lakini anapinga tamaa za waovu.

4 Uvivu unasababisha umasikini, lakini mukono wa mutu wa bidii unajitajirisha.

5 Mwenye akili anakusanya wakati wa mavuno. Kulala wakati wa kuvuna ni haya.

6 Mwenye haki anajiletea baraka yeye mwenyewe, lakini kinywa cha mwovu kimesongwa na mateso makali.

7 Mwenye haki anakumbukwa kwa baraka, lakini waovu watasahauliwa kabisa.

8 Mwenye hekima anakubali maonyo, lakini mupumbafu anayesemasema mingi ataangamia.

9 Anayeishi kwa ukamilifu anaishi salama, lakini anayepotosha maisha yake atagunduliwa.

10 Anayekonyeza macho kwa nia mbaya analeta taabu, lakini anayeonya waziwazi analeta amani.

11 Kinywa cha mwenye haki ni chemichemi ya uzima, lakini kinywa cha mwovu kimesongwa na mateso makali.

12 Chuki inaleta ugomvi, lakini upendo unafunika makosa yote.

13 Katika kinywa cha mwenye ufahamu kuna hekima, lakini wasiokuwa na akili watapigwa fimbo katika mugongo.

14 Wenye hekima wanalinda maarifa, lakini kusemasema kwa mupumbafu kunaleta maangamizi haraka.

15 Mali ya tajiri ndiyo kikingio chake. Umasikini wa masikini unamuletea maangamizi.

16 Mushahara wa mutu wa haki ni uzima, lakini mapato ya mwovu ni katika zambi.

17 Anayekubali kufundishwa anaelekea kwenye uzima, lakini anayekataa kuonywa amepotoka.

18 Anayemuchukia mwingine kwa siri ni munafiki. Anayemusingizia mutu ni mupumbafu.

19 Kwenye kuwa maneno mengi hakukosekani makosa, lakini aneyezuia ulimi wake ana akili.

20 Maneno ya mwenye haki ni kama feza bora. Akili ya mutu mwovu haifai kwa kitu chochote.

21 Maneno ya mwenye haki yanawafalia watu wengi, lakini wapumbafu wanakufa kwa kukosa akili.

22 Baraka za Yawe ndizo zinazoleta utajiri. Juhudi za mutu haziongezi kitu.

23 Kwa mupumbafu, kutenda maovu ni kama muchezo, lakini watu wenye akili wanafurahia hekima.

24 Kitu mutu mwovu anachoogopa ndicho kitakachomupata, lakini kitu mwenye haki anachotamani ndicho atakachopewa.

25 Upepo mukali unapopita na mwovu anatoweka, lakini mwenye haki anaimarishwa milele.

26 Kama vile siki inavyokuwa kwa meno au moshi ndani ya macho, ndivyo muvivu anavyokuwa kwa bwana wake.

27 Kumwogopa Yawe kunarefusha maisha, lakini miaka ya waovu itakuwa mifupi.

28 Tumaini la mwenye haki linaleta furaha, lakini tazamio la mwovu linapotea bure.

29 Yawe ni kimbilio la watu wenye mwenendo sawa, lakini ataangamiza watenda maovu.

30 Wenye haki hawataondolewa katika inchi hata kidogo, lakini waovu hawatakaa katika inchi.

31 Kinywa cha mwenye haki kinatoa mambo ya hekima, lakini ulimi wa mutu mubaya utakatwa mbali.

32 Midomo ya wenye haki inajua mambo yatakayokubaliwa, lakini vinywa vya waovu vinasema tu maovu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan