Mezali 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Shabaha ya mezali 1 Hizi ni mezali za Solomono mwana wa Daudi mufalme wa Israeli. 2 Zitawawezesha watu kujua hekima na mafundisho, na kufahamu misemo yenye maana kubwa. 3 Zitawafundisha watu matendo ya hekima, haki, usawa, na sheria ya Mungu. 4 Zitawaerevusha wajinga, zitawapa vijana maarifa na akili. 5 Mwenye hekima akizisikiliza, zitamwongezea elimu; na mwenye ufahamu zitamupatia ujuzi. 6 Wataweza kuelewa mezali na maana iliyofichwa, watayaelewa maneno ya wenye hekima na vitendawili vyao. 7 Kumwogopa Yawe ni musingi wa maarifa, lakini wapumbafu wanazarau hekima na mafundisho. Maonyo kwa vijana 8 Mwana wangu, sikiliza mafundisho ya baba yako, wala usizarau mashauri ya mama yako; 9 hayo yatakupamba kilemba cha neema juu ya kichwa chako, kama mukufu katika shingo yako. 10 Mwana wangu, usikubali kushawishiwa na wenye zambi. 11 Wakisema: “Twende kuvizia mutu na kumwua; kuja tuwashambulie wasiokuwa na kosa! 12 Tutawameza wakiwa wazima kama kuzimu, watakuwa kama wale wanaoshuka katika shimo. 13 Tutajitwalia mali zote za bei kali, tutazijaza nyumba zetu vitu tulivyonyanganya. 14 Kuja na ushirikiane nasi, vyote tutakavyopata tutagawanyana.” 15 Wewe mwana wangu usiandamane nao, uzuie muguu wako usifuatane nao. 16 Maana wao wako mbio kutenda maovu, haraka zao zote ni za kumwanga damu. 17 Mutego unaotegwa na ndege akiona, mutego ule unategwa bure. 18 Wao wanavizia na kujiangamiza wao wenyewe, wanatega mutego wa kujinasa wao wenyewe. 19 Ndizo njia za wanyanganyi; maisha yao yananyanganywa. Hekima inaita 20 Hekima inapiga kelele katika barabara, inaita kwa sauti kubwa katika viwanja; 21 inaita kwenye masanganjia, inaita kwenye milango ya muji: 22 “Enyi wajinga! Mpaka wakati gani mutapenda kuwa wajinga? Mpaka wakati gani wenye kuzarau watafurahia mazarau yao, na wapumbafu kuchukia maarifa? 23 Musikilize maonyo yangu; nitawamiminia mawazo yangu, nitawajulisha maneno yangu. 24 “Nimewaita nanyi mumekataa kusikiliza, nimewanyooshea mukono mukuje nanyi hamukujali, 25 mumetupilia mashauri yangu yote, mumezarau maonyo yangu. 26-27 Kwa sababu hiyo, woga utakapowapata kama zoruba, hasara yenu itakapowatokea kama upepo mukali, taabu na huzuni vitakapowapata, nitachekelea hasara yenu na kuwasimanga. 28 Halafu mutaniita lakini sitaitika; mutanitafuta kwa bidii lakini hamutanipata. 29 “Muliyachukia maarifa, wala hamukuchagua kumwogopa Yawe, 30 mulikataa shauri langu, mukazarau maonyo yangu yote. 31 Basi, mutakula matunda ya mienendo yenu, mutageukiwa na mashauri yenu wenyewe. 32 Maana wajinga wanajiua kwa kiburi chao, wapumbafu wanajiangamiza kwa kufanikiwa kwao. 33 Lakini mutu anayenisikiliza atakaa salama, atatulia bila kuogopa mabaya.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo