Matayo 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Musiwahukumu wengine ( Lk 6.37-38 , 41-42 ) 1 “Musiwahukumu wengine kusudi Mungu asiwahukumu ninyi vilevile. 2 Kwa maana mutahukumiwa kufuatana na namna munavyowahukumu wengine, na kipimo kile munachowapimia wengine ndicho kitakachotumiwa kwenu vilevile. 3 Namna gani unaona vumbi inayokuwa ndani ya jicho la ndugu yako, lakini haufikiri juu ya nguzo inayokuwa ndani ya jicho lako? 4 Au namna gani unaweza kumwambia ndugu yako kwamba aache umwondoe vumbi inayokuwa ndani ya jicho lake, wakati ndani ya jicho lako mwenyewe mungali ile nguzo? 5 Wewe munafiki, ondosha kwanza nguzo kutoka ndani ya jicho lako, kisha utaweza kuona waziwazi na kuweza kuondoa ile vumbi inayokuwa ndani ya jicho la ndugu yako. 6 “Musiwape imbwa vitu vitakatifu, kusudi wasiwageukie na kuwararua, wala musiwatupie nguruwe ushanga zenu za bei kusudi wasizikanyagekanyage. Kuomba na kupewa ( Lk 11.9-13 ) 7 “Muombe, nanyi mutapewa; mutafute, nanyi mutapata; mupige hodi, nanyi mutafunguliwa mulango. 8 Kwa maana kila mutu anayeomba, anapewa; naye anayetafuta, anapata, naye anayepiga hodi, anafunguliwa. 9 Ni nani kati yenu anayeweza kumupa mutoto wake jiwe kama akimwomba mukate? 10 Au nani anaweza kumupa nyoka kama akimwomba samaki? 11 Basi ikiwa ninyi munaokuwa waovu munajua kuwapa watoto wenu vitu vizuri, zaidi sana Baba yenu anayekuwa mbinguni atawapa wale wanaomwomba vitu vizuri zaidi. 12 “Basi jambo lolote munalotaka wengine wawatendee, ninyi mulitende kwao vilevile, kwa maana kile ndicho kifungo cha Sheria ya Musa na mafundisho ya manabii. Milango miwili ( Lk 13.24 ) 13 “Muingie kwa kupitia mulango unaokuwa mwembamba. Kwa maana njia inayoongoza kufikia kwenye lufu ni kubwa, nao mulango unaoiingilia ni mupana, nao watu wanaoipitia ni wengi. 14 Lakini njia inayoongoza kufikia kwenye uzima ni yenye kusongamana na mulango unaoiingilia ni mwembamba, nao watu wanaoifuata ni wachache tu. Muti unajulikana kwa njia ya matunda yake ( Lk 6.43-44 ) 15 “Mufanye angalisho na manabii wa uongo; kwa maana wanakuja kwenu wakionekana kwa inje kama vile kondoo, lakini ndani, wao ni kama imbwa wakali wa pori. 16 Mutawatambua kwa matendo yao. Watu hawachumi matunda ya mizabibu au ya tini toka juu ya miti ya miiba. 17 Na ni vile inavyokuwa: kila muti muzuri unazaa matunda mazuri, lakini kila muti mubaya unazaa matunda mabaya. 18 Muti muzuri hauwezi kutoa matunda mabaya, wala muti mubaya hauwezi kutoa matunda mazuri. 19 Kila muti usiozaa matunda mazuri unakatwa na kutupwa katika moto. 20 Basi kwa hiyo, mutawatambua manabii wa uongo kwa njia ya matendo yao. Wafusi wa kweli wa Yesu ( Lk 13.25-27 ) 21 “Si kila mutu anayeniita ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika Ufalme wa mbinguni, lakini yule tu anayefanya mapenzi ya Baba yangu anayekuwa mbinguni. 22 Siku ile ya hukumu itakapotimia, wengi wataniambia: ‘Bwana, Bwana, sisi hatukutangaza ujumbe wa Mungu? Nasi hatukufukuza pepo kwa jina lako na kufanya maajabu mengi kwa jina lako?’ 23 Halafu mimi nitawaambia hivi waziwazi: ‘Sikuwajua ninyi hata siku moja. Mutoke karibu nami, ninyi watenda maovu.’ Mufano wa wajengaji wawili ( Lk 6.47-49 ) 24 “Basi kila mutu anayesikia hayo maneno yangu na kuyashika, anafananishwa na mutu mwenye akili aliyejenga nyumba yake juu ya jiwe. 25 Mvua ikanyesha, mito ikajaa, nao upepo ukavuma na kuishambulia nyumba ile, lakini haikuanguka, kwa sababu musingi wake ulikuwa umejengwa juu ya jiwe. 26 “Lakini kila mutu anayesikia maneno ninayotoka kusema bila kuyashika, anafananishwa na mutu mupumbafu aliyejenga nyumba yake juu ya udongo wenye kichanga. 27 Mvua ikanyesha, mito ikajaa, upepo ukavuma na kupiga nyumba ile, nayo ikaanguka na kubomoka kabisa.” Mamlaka ya Yesu 28 Yesu alipomaliza kusema maneno hayo, makundi ya watu wakashangaa sana kwa kuona namna alivyowafundisha; 29 kwa maana hakuwafundisha sawa vile walimu wao wa Sheria, lakini kama vile mutu mwenye mamlaka. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo