Matayo 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mahubiri ya Yoane Mubatizaji ( Mk 1.1-8 ; Lk 3.1-18 ; Yn 1.19-28 ) 1 Katika siku zile Yoane Mubatizaji alitokea akihubiri katika jangwa la Yudea 2 akisema: “Mugeuke toka zambi zenu, kwa maana Ufalme wa mbinguni umekaribia!” 3 Yoane ndiye yule Mungu aliyemutaja kwa njia ya nabii Isaya akisema: “Sauti inatangaza katika jangwa: ‘Mutengeneze njia ya Bwana, munyooshe pahali atakapopita!’ ” 4 Yoane alikuwa akivaa nguo iliyotengenezwa na manyoya ya ngamia na mukaba wa ngozi katika kiuno. Naye alikuwa akikula nzige na asali ya pori. 5 Watu wa Yerusalema na wa jimbo lote la Yudea, nao waliokaa fasi zote pembeni ya muto Yordani walimufikia. 6 Waliungama zambi zao, naye Yoane aliwabatiza katika muto Yordani. 7 Yoane alipoona Wafarisayo wengi na Wasadukayo wakimufikia kwa kubatizwa, aliwaambia: “Ninyi kikundi cha nyoka! Ni nani aliyewaambia kwamba munaweza kuponyoka azabu ya Mungu inayokaribia? 8 Basi muonyeshe kwa njia ya matendo kwamba mumegeuka toka zambi zenu. 9 Musijifikiri kwamba munaweza kujidai tu kuwa Abrahamu ndiye babu yenu. Ninawaambia kwamba Mungu anaweza kugeuza mawe haya kuwa watoto wa Abrahamu! 10 Shoka limekwisha kuwekwa tayari kwenye mashina ya miti. Kila muti usiozaa matunda mazuri utakatwa na kutupwa katika moto. 11 Mimi ninawabatiza kwa maji kwa kuonyesha kwamba mumegeuka toka zambi zenu. Lakini yule atakayekuja nyuma yangu atawabatiza kwa Roho Mutakatifu na kwa moto. Yeye ni mwenye uwezo kunipita, nami sistahili hata kumuvua viatu. 12 Yeye anashika lungo katika mikono yake kwa kupepeta ngano. Atakusanya ngano na kuitia katika gala yake, lakini atateketeza maganda katika moto usiozimika.” Ubatizo wa Yesu ( Mk 1.9-11 ; Lk 3.21-22 ) 13 Wakati ule Yesu akatoka Galilaya na kufika kwenye muto Yordani, akamwendea Yoane kusudi abatizwe naye. 14 Lakini Yoane akamukatalia, akimwambia: “Ni mimi ninayepaswa kubatizwa nawe; namna gani unakuja kwangu?” 15 Lakini Yesu akamujibu: “Ukubali kufanya hivi sasa. Kwa maana ni kwa njia hii tutatimiza mambo yote yanayokuwa ya haki mbele ya Mungu.” Basi Yoane akakubali. 16 Yesu alipokwisha kubatizwa na kutoka ndani ya maji, mara moja mbingu zikafunguka, naye akamwona Roho wa Mungu akishuka kwa mufano wa njiwa na kukaa juu yake. 17 Na sauti ikasikilika toka mbinguni, ikisema: “Huyu ni Mwana wangu mupendwa; ninapendezwa naye sana.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo