Matayo 27 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yesu mbele ya Pilato ( Mk 15.1 ; Lk 23.1-2 ; Yn 18.28-32 ) 1 Kulipokucha, wakubwa wote wa makuhani na wasimamizi wa watu wakakata shauri la kumwua Yesu. 2 Wakamufunga, wakamupeleka na kwenda kumutoa kwa liwali Pilato. Kufa kwa Yuda ( Mdo 1.18-19 ) 3 Basi Yuda, aliyemutoa Yesu, alipoona kwamba Yesu amekwisha kuhukumiwa, akajuta, akawarudishia wakubwa wa makuhani na wasimamizi wa watu vile vikoroti makumi tatu vya feza. 4 Akawaambia: “Nimekosa kwa kumutoa mutu huyu asiyekuwa na kosa auawe.” Lakini wao wakamujibu: “Jambo hilo halituelekei. Ni kazi yako wewe mwenyewe!” 5 Yuda akatupa vile vikoroti ndani ya hekalu, naye akaondoka na kwenda kujitundika. 6 Wakubwa wa makuhani wakaokota zile feza na kusema: “Kufuatana na Sheria yetu hairuhusiwi kuweka feza kama hizi ndani ya sanduku ya hekalu kwa sababu feza hizi ni za damu.” 7 Basi walipokwisha kukata shauri, wakatumia zile feza kwa kununua shamba la Mufinyanzi, kusudi likuwe shamba la kuzikia wageni. 8 Ni kutokana na mambo hayo yote shamba lile linaitwa “Shamba la Damu” hata leo. 9 Halafu yakatimia maneno yaliyosemwa na nabii Yeremia: “Walitwaa vikoroti makumi tatu vya feza kufuatana na bei Waisraeli waliyoipanga juu yake, 10 wakazitumia kwa kununua shamba la Mufinyanzi, sawa vile Bwana alivyoniamuru.” Yesu mbele ya liwali Pilato ( Mk 15.2-5 ; Lk 23.3-5 ; Yn 18.33-38 ) 11 Yesu alipopelekwa mbele ya liwali, yeye akamwuliza: “Wewe ndiwe Mufalme wa Wayuda?” Yesu akamujibu: “Wewe umesema.” 12 Na kisha wakubwa wa makuhani na wasimamizi wa watu wakamushitaki, 13 lakini hakujibu neno. Halafu Pilato akamwuliza tena: “Hausikii mambo haya yote wanayokushitakia?” 14 Lakini Yesu hakumujibu hata juu ya neno moja, hata yule liwali akashangaa sana. Yesu anahukumiwa kufa ( Mk 15.6-15 ; Lk 23.15-25 ; Yn 16.39–19.16) 15 Kila sikukuu ya Pasaka, liwali alikuwa na desturi ya kuwafungulia watu mufungwa mumoja wanayemutaka. 16 Na katika siku zile kulikuwa mufungwa mumoja aliyejulikana sana, jina lake Baraba. 17 Nao watu walipokuwa wamekusanyika pamoja, Pilato akawauliza: “Munataka niwafungulie nani kati ya Baraba na Yesu anayeitwa Kristo?” 18 Alisema vile kwa maana alijua kwamba walimutoa Yesu kwake kwa sababu walimwonea wivu tu. 19 Pilato alipokuwa amekwisha kuikaa kwa kuamua maneno, muke wake akamutumia ujumbe huu: “Usijiingize katika maneno ya mutu huyo mwenye haki, kwa sababu usiku niliteseka sana katika ndoto kwa ajili yake.” 20 Lakini wakubwa wa makuhani na wasimamizi wa watu wakawashawishi wale waliokusanyika kwamba waombe Baraba afunguliwe, naye Yesu auawe. 21 Liwali akawauliza: “Munataka niwafungulie nani kati ya watu hawa wawili?” Nao wakamujibu: “Utufungulie Baraba.” 22 Pilato akawauliza tena: “Basi munataka nifanye nini na huyu Yesu anayeitwa Kristo?” Nao wote wakajibu: “Atundikwe juu ya musalaba!” 23 Pilato akawauliza tena: “Yeye alifanya ubaya gani?” Lakini wakazidi kupiga kelele wakisema: “Atundikwe juu ya musalaba!” 24 Basi Pilato alipoona kwamba hataweza kufanya kitu, isipokuwa tu kuongeza fujo, akatwaa maji na kunawa mikono yake mbele ya watu wote, akisema: “Lazima ya damu ya mutu huyu isikuwe juu ya kichwa changu! Maneno haya yanawaangukia.” 25 Nao watu wote wakajibu: “Lazima ya damu ya mutu huyu ikuwe juu ya kichwa chetu na juu ya kichwa cha watoto wetu!” 26 Basi Pilato akawafungulia Baraba, lakini akaamuru wamupige Yesu fimbo na kumutoa kusudi atundikwe juu ya musalaba. Waaskari wanamuchekelea Yesu ( Mk 15.16-20 ; Yn 19.2-3 ) 27 Kisha waaskari wa liwali Pilato wakamupeleka Yesu ndani ya upango wa nyumba ya liwali, nalo kundi lao lote wakakusanyika na kumuzunguka. 28 Wakamuvua nguo zake na kumuvalisha kanzu nyekundu. 29 Nao wakasokota taji na tawi lenye miiba na kumuvalisha nalo kwenye kichwa chake. Wakaweka tete katika mukono wake wa kuume, wakapiga magoti mbele yake na kumuchekelea, wakisema: “Jambo, Mufalme wa Wayuda!” 30 Wakamutemea mate, wakatwaa lile tete na kumupiga nalo juu ya kichwa. 31 Walipokwisha kumuchekelea, wakamuvua ile kanzu na kumuvalisha nguo zake. Kisha wakaondoka naye kwenda kumutundika juu ya musalaba. Yesu anatundikwa juu ya musalaba ( Mk 15.21-32 ; Lk 23.26-43 ; Yn 19.17-27 ) 32 Walipokuwa wakiondoka, wakamwona mutu mumoja wa Kurene, aliyeitwa Simoni; wakamushurutisha abebe musalaba wa Yesu. 33 Na walipofika kwenye pahali palipoitwa Golgota, maana yake, “Kilima cha Mufupa wa Kichwa,” 34 wakamupa Yesu divai iliyochanganywa na kinywaji chenye uchungu sana. Lakini alipoionja, akakataa kuikunywa. 35 Nao walipokwisha kumutundika juu ya musalaba, wakagawanya nguo zake kwa kuzipigia kura. 36 Kisha wakaikaa pale kwa kumuchunga. 37 Juu ya kichwa chake wakaweka tangazo hili kwa kuonyesha sababu ya kuhukumiwa kwake: “Huyu ndiye Yesu, Mufalme wa Wayuda.” 38 Vilevile wanyanganyi wawili walitundikwa juu ya misalaba pamoja na Yesu, mumoja kwa upande wake wa kuume na mwingine kwa upande wa kushoto. 39 Watu waliokuwa wakipita pale walimutukana, na kutikisatikisa vichwa vyao, 40 wakisema: “Wewe uliyetaka kubomoa hekalu na kujenga lingine katika siku tatu, ujiokoe sasa wewe mwenyewe! Kama wewe ni Mwana wa Mungu, ujishushe juu ya musalaba!” 41 Vilevile wakubwa wa makuhani walimuchekelea pamoja na walimu wa Sheria na wasimamizi wa watu, wakisemezana hivi: 42 “Aliokoa wengine, lakini sasa anashindwa kwa kujiokoa yeye mwenyewe! Yeye ni mufalme wa Waisraeli, sasa ajishushe pale juu ya musalaba kusudi nasi tupate kumwamini. 43 Yeye alimutumainia Mungu na alisema kwamba yeye ni Mwana wa Mungu. Ikiwa Mungu anapendezwa naye sasa amwokoe!” 44 Hata wale wanyanganyi waliotundikwa pamoja naye walimutukana vilevile. Kufa kwa Yesu ( Mk 15.33-41 ; Lk 23.44-49 ; Yn 19.28-30 ) 45 Tangia saa sita ya muchana, giza lilikuwa katika inchi yote mpaka saa tisa. 46 Ilipokuwa karibu saa tisa, Yesu akalalamika akisema: “Eli, Eli, lama sabaktani,” maana yake, “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?” 47 Na watu wamoja waliosimama pale walipomusikia wakasema: “Anamwita Elia.” 48 Mara moja, mumoja wao akaenda mbio akatwaa kikausho, akakichovya ndani ya divai yenye kuchacha. Akakifungia juu ya tete, akakipandishia Yesu, kusudi apate kunywa. 49 Lakini wengine wakasema: “Mwache, tuone kama Elia atakuja kumwokoa!” 50 Lakini Yesu, akalalamika tena kwa sauti kubwa na kukata roho. 51 Na saa ile ile pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu mpaka chini. Inchi ikatetemeka, mawe makubwa yakapasuka, 52 makaburi yakafunguka, na watakatifu wengi waliokufa zamani wakafufuliwa. 53 Wakatoka ndani ya makaburi, na nyuma ya kufufuka kwa Yesu, wakaingia katika muji mutakatifu Yerusalema, na watu wengi wakawaona. 54 Mukubwa wa waaskari na wale waliokuwa pamoja naye wakimuchunga Yesu walipoona tetemeko la inchi na mambo yote yaliyofanyika, wakaogopa sana, na kusema: “Hakika mutu huyu alikuwa Mwana wa Mungu.” 55 Pale kulikuwa vilevile wanawake wengi walioangalia kwa mbali; ndio wale waliomufuata Yesu tokea Galilaya, wakimushugulikia. 56 Kati yao kulikuwa Maria wa Magdala, Maria mama ya Yakobo na Yosefu, pamoja na mama ya wana wa Zebedayo. Kuzikwa kwa Yesu ( Mk 15.42-47 ; Lk 23.50-56 ; Yn 19.38-42 ) 57 Ilipokwisha kuwa magaribi, mutu mumoja tajiri aliyeitwa Yosefu wa Arimatea, akafika. Huyu naye alikuwa mwanafunzi wa Yesu. 58 Yeye akaenda kwa liwali Pilato kwa kumwomba maiti ya Yesu. Basi Pilato akaamuru aipewe. 59 Halafu Yosefu akatwaa maiti ile, akaifungafunga ndani ya vitambaa safi. 60 Akaiweka ndani ya kaburi lake jipya alilojichimbia katika jiwe. Kisha akasukumia jiwe kubwa kwenye kiingilio cha lile kaburi na kujiendea. 61 Maria wa Magdala na yule Maria mwingine walikuwa wakiikaa pale, kuelekea kwenye kaburi. Waaskari wanachunga kaburi 62 Kesho yake, maana yake siku iliyofuata ile ya matayarisho ya siku ya Sabato, wakubwa wa makuhani na Wafarisayo wakamwendea Pilato, 63 na kumwambia: “Bwana, tunakumbuka kwamba wakati yule mudanganyifu alipokuwa angali muzima, alisema: ‘Kwa siku tatu kisha kufa kwangu, nitafufuka.’ 64 Basi uamuru kaburi lichungwe mpaka zile siku tatu nyuma ya kufa kwake zitakapotimia, kusudi wanafunzi wake wasifike kuiba maiti yake na kuwaambia watu kwamba amefufuka.” 65 Pilato akawajibu: “Muko na waaskari walinzi. Muende kuchunga kaburi kwa kadiri munavyoweza.” 66 Basi wakaenda, wakatia muhuri juu ya lile jiwe, na wakaweka waaskari pale kwa kulichunga. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo