Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Matayo 24 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yesu anatangaza uharibifu wa hekalu
( Mk 13.1-2 ; Lk 21.5-6 )

1 Yesu akatoka ndani ya hekalu, na alipokuwa akienda, wanafunzi wake wakamufikia na kumwonyesha majengo ya hekalu.

2 Lakini Yesu akawaambia: “Munaona haya yote? Kweli ninawaambia: hapa hakutabaki hata jiwe moja juu ya lingine; yote yatabomolewa.”

3 Basi Yesu alipokuwa akiikaa kwa mulima wa Mizeituni, wanafunzi wake wakamwendea peke yao na kumwuliza: “Utuambie, mambo hayo uliyotoka kusema yatakuwa wakati gani? Na kitambulisho cha kurudi kwako nao wakati wa mwisho wa dunia ni nini?”

4 Yesu akawajibu: “Muangalie vizuri, mutu asiwadanganye.

5 Watu wengi watakuja wakijiita kwa jina langu, wakisema: ‘Mimi ni Kristo!’ Nao watawadanganya wengi.

6 Mutasikia habari za matokeo au utetezi wa vita, lakini musiogope. Sherti mambo hayo yatukie, lakini hayaonyeshi kama mwisho umefika.

7 Kwa maana taifa litapigana na taifa, na ufalme utapigana na ufalme. Kutakuwa njaa na tetemeko ya inchi katika pahali mbalimbali.

8 Na haya yote ni kama mwanzo wa maumivu ya kuzaa tu.

9 “Halafu watu watawatoa kusudi muteswe na kuuawa, na watu wa mataifa yote watawachukia ninyi kwa ajili yangu.

10 Kwa wakati ule watu wengi wataanguka katika imani yao; watatoana wao kwa wao na kuchukiana.

11 Manabii wengi wa uongo watatokea, nao watawadanganya watu wengi.

12 Na kwa sababu ya kuongezeka kwa maovu, upendo wa watu wengi utapunguka.

13 Lakini atakayevumilia mpaka mwisho ataokolewa.

14 Na hii Habari Njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia nzima kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; na halafu mwisho wa dunia utatimia.


Mateso makubwa
( Mk 13.14-23 ; Lk 21.20-24 )

15 “Mutamwona yeye anayeitwa ‘Chukizo Linaloleta Uharibifu,’ yule aliyetajwa na nabii Danieli, akisimamishwa katika hekalu. (Anayesoma maneno haya aelewe maana yake.)

16 Basi watakaokuwa Yudea, wakimbilie kwa milima.

17 Atakayekutiwa juu ya paa la nyumba asishuke ndani yake kwa kutwaa kitu.

18 Na mutu atakayekutiwa katika shamba, asirudi kwake kwa kutwaa nguo yake.

19 Wanawake wenye mimba na wenye kunyonyesha watapata hasara katika siku zile!

20 Mumwombe Mungu kusudi kukimbia kwenu kusikuwe wakati wa mvua au kwa siku ya Sabato!

21 Kwa maana katika siku zile kutakuwa mateso makubwa yasiyotokea tangia kuumbwa kwa dunia mpaka sasa, wala hakutatokea tena mateso kama yale.

22 Na kama Mungu asingepunguza siku zile za mateso, hakuna hata mutu mumoja angeponyoka kufa. Lakini kwa ajili ya watu wake aliowachagua, yeye atazipunguza.

23 “Kwa wakati ule mutu akiwaambia ninyi: ‘Angalia, Kristo yuko hapa!’ au ‘Yuko kule!’, musimusadiki

24 kwa maana kutatokea watu wanaojiita kwa uongo ‘Kristo’ pamoja na manabii wa uongo, nao wataonyesha vitambulisho vikubwa na maajabu, hata ikiwezekana, wawadanganye hata watu waliochaguliwa na Mungu.

25 Angalia, nimewaambia haya yote mbele.

26 “Basi kama watu wakiwaambia: ‘Angalia, Kristo yuko katika jangwa!’, musiende kule. Au wakiwaambia: ‘Angalia, yuko katika chumba cha ndani!’, musiwasadiki.

27 Kwa maana kama vile umeme unavyoangaza na kuonekana katika mbingu yote, ni vile Mwana wa Mutu atakavyoonekana siku atakapokuja.

28 “Nafasi yoyote kunapokuwa muzoga, ndipo tai wanapokusanyika.


Kuja kwa Mwana wa Mutu
( Mk 13.24-27 ; Lk 21.25-28 )

29 “Mara moja kisha mateso ya siku zile, jua litatiwa giza, mwezi hautaangaza, nyota zitaanguka toka mbinguni na vyote vyenye nguvu katika mbingu vitatikiswa.

30 Kisha kitambulisho cha kurudi kwa Mwana wa Mutu kitaonekana katika mbingu. Nayo mataifa yote ya dunia yatakuwa katika malalamiko, na yatamwona Mwana wa Mutu akikuja katikati ya mawingu toka mbinguni, kwa uwezo na utukufu mukubwa.

31 Baragumu kubwa itapigwa, halafu atawatuma wamalaika wake katika pande ine za dunia, kusudi wawakusanye watu wake aliowachagua, kutoka katika dunia nzima.


Mafundisho toka muti wa matunda ya tini
( Mk 13.28-31 ; Lk 21.29-33 )

32 “Muangalilie mufano juu ya muti wa tini. Wakati matawi yake yanapochipuka, nayo majani yao yanapochipuka, ninyi munatambua kwamba wakati wa jua kali unakaribia.

33 Vilevile, wakati mutakapoona mambo haya yote niliyotoka kutaja yanatokea, mujue kwamba yeye yuko karibu, na amekuwa kwa mulango.

34 Maana kweli ninawaambia: hiki kizazi hakitapita mbele ya kutimia kwa mambo hayo yote.

35 Mbingu na dunia vitatoweka, lakini maneno yangu hayatabadilika hata kidogo.


Mungu pekee anajua wakati wa mwisho
( Mk 13.32-37 ; Lk 17.26-30 , 34-36 )

36 “Lakini hakuna mutu anayejua siku ile na saa, hata wamalaika wa mbinguni, hata Mwana, isipokuwa Baba peke yake tu.

37 Kama ilivyokuwa katika siku za Noa, ndivyo itakavyokuwa wakati Mwana wa Mutu atakaporudi.

38 Kwa maana katika siku zile mbele ya kunyesha kwa mvua kubwa, watu walikuwa wakikula na kunywa, wakioa na kuolewa, mpaka ilipotimia siku ile Noa alipoingia ndani ya chombo.

39 Nao hawakutambua kitu mpaka mvua kubwa sana ilipotokea, na kuwaua wote. Na ni hivi itakavyokuwa wakati Mwana wa Mutu atakaporudi.

40 Wakati ule, watu wawili watakutiwa katika shamba moja; mumoja atapelekwa na mwingine ataachwa.

41 Wanawake wawili watakutiwa wakisaga pamoja, mumoja atapelekwa na mwingine ataachwa.

42 Basi mukeshe, kwa sababu hamujui siku Bwana wenu atakaporudi.

43 Munajua vema kwamba mwenye nyumba angalijua wakati gani mwizi atakapokuja kuiba, angalikesha na kuchunga nyumba yake isibomolewe.

44 Kwa hiyo, ninyi vilevile mukuwe tayari, kwa sababu Mwana wa Mutu atarudi saa musiyozania.


Mutumishi mwaminifu na mutumishi mubaya
( Lk 12.41-48 )

45 “Basi ni nani anayekuwa mutumishi mwaminifu na mwenye akili? Ni yule bwana wake aliyemuweka kuwa musimamizi wa watumishi wake wengine na kumwamuru kuwapatia posho yao kwa wakati uliopangwa.

46 Heri mutumishi yule ikiwa saa bwana wake anaporudi, anamukuta akifanya kazi ile.

47 Kweli ninawaambia: bwana wake atamuweka mutumishi yule kuwa musimamizi wa mali yake yote.

48 Lakini kama mutumishi yule ni mutu mubaya, atajisemesha yeye mwenyewe kwamba bwana wake anakawia,

49 naye ataanza kuwapiga watumishi wenzake, na kula na kunywa pamoja na walevi.

50 Basi bwana wa mutumishi yule atakuja siku asiyozania na saa asiyojua.

51 Naye atamupiga vikali na atamwazibu sawa na watu wanafiki, akimuweka kwenye nafasi atakapolia na kusaga meno.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan