Matayo 20 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mufano wa watumishi waliotumika katika shamba la mizabibu 1 “Ufalme wa mbinguni unafanana na mutu mumoja mwenye shamba la mizabibu aliyetoka asubui mapema kwa kutafuta watu wa kutumika katika shamba lake. 2 Akapatana na watumishi wamoja kuwalipa kila mutu kikoroti kimoja cha feza sawa na kawaida, naye akawatuma katika shamba lake. 3 Ilipokuwa saa tatu za asubui, akatoka tena akawaona watu wengine wakisimama bure kwenye nafasi ya makutano. 4 Akawaambia: ‘Ninyi vilevile muende kutumika katika shamba langu la mizabibu, nami nitawalipa sawa na haki yenu.’ 5 Basi wakaenda. Mwenye shamba akatoka tena na saa sita, kisha na saa tisa, akafanya sawasawa mbele. 6 Karibu na saa kumi na moja akatoka tena, naye akakuta watu wengine wakisimama pale kwenye nafasi ile. Akawauliza: ‘Sababu gani munasimama bure hapa muchana kutwa?’ 7 Nao wakamujibu: ‘Kwa sababu hakuna mutu aliyetupatia kazi.’ Halafu akawaambia: ‘Ninyi vilevile muende kutumika katika shamba langu la mizabibu.’ 8 “Ilipokuwa magaribi, mwenye shamba akamwambia musimamizi wake: ‘Uwaite watumishi na uwalipe mushahara wao, ukianzia kwa wale wa mwisho mpaka kwa wale wa kwanza.’ 9 Wale walioanza kazi na saa kumi na moja ya magaribi wakakuja, na kila mutu akapokea kikoroti kimoja cha feza. 10 Na wale waliotangulia kuanza kazi wakakuja, wakizani kwamba watapewa zaidi. Lakini nao vilevile wakapokea kila mutu kikoroti kimoja cha feza. 11 Watu wale walipopokea mushahara ule, wakamunungunikia mwenye shamba. 12 Wakasema: ‘Watumishi hawa wa mwisho wametumika kazi kwa saa moja tu, nawe umewalipa sawasawa na sisi tuliovumilia muchoko na jua kali kwa muchana kutwa!’ 13 Lakini mwenye shamba akamujibu mumoja wao: ‘Rafiki, sikupunji kitu. Hatukupatana kwamba nitakulipa kikoroti kimoja cha feza kwa siku? 14 Basi kamata mushahara wako na uende. Ilinipendeza mimi peke kumupa mutu wa mwisho mushahara unaolingana na wako. 15 Sina haki ya kutumia mali yangu sawa ninavyotaka? Unapatwa na wivu kwa sababu mimi ni mwema?’ ” 16 Yesu akaongeza kusema: “Ni hivi inavyokuwa vilevile: wanaokuwa wa mwisho watakuwa wa kwanza, nao wanaokuwa wa kwanza watakuwa wa mwisho.” Yesu anajulisha mara ya tatu habari za kufa na kufufuka kwake ( Mk 10.32-34 ; Lk 18.31-34 ) 17 Yesu alipokuwa katika njia kwenda Yerusalema, akaita wanafunzi wake kumi na wawili pembeni, akawaambia: 18 “Angalia, tunapanda kwenda Yerusalema na kule Mwana wa Mutu atatolewa kwa wakubwa wa makuhani na kwa walimu wa Sheria. Nao watamuhukumu auawe 19 na kumutoa katika mikono ya watu wa mataifa mengine. Nao watamuchekelea, watamupiga fimbo na kumutundika juu ya musalaba. Lakini kwa siku ya tatu kisha kufa kwake, atafufuka.” Ombi la mama ya Yakobo na Yaone ( Mk 10.35-45 ) 20 Wana wa Zebedayo pamoja na mama yao wakamufikia Yesu. Yule mama akapiga magoti mbele yake, kwa kumwomba kitu kimoja. 21 Yesu akamwuliza: “Unataka nini?” Naye akamujibu: “Utakapokuwa katika Ufalme wako, uwaruhusu hawa wana wangu wawili kuikaa, mumoja kwa upande wako wa kuume na mwingine kwa upande wako wa kushoto.” 22 Yesu akawaambia: “Hamujui kitu munachoomba. Munaweza kubeba muzigo wa mateso nitakaoubeba?” Nao wakamujibu: “Tunaweza.” 23 Na Yesu akawaambia: “Hakika mutaubeba muzigo nitakaoubeba. Lakini kuikalisha mutu kwa upande wangu wa kuume au wa kushoto si kazi yangu. Ni Mungu peke yake atakayeweka watu aliowatayarisha kwenye nafasi zile.” 24 Wanafunzi wengine kumi waliposikia maneno yale, wakachukizwa na wale wandugu wawili. 25 Halafu Yesu akawaita wote pamoja na kuwaambia: “Munajua kwamba watawala wa mataifa wanayatawala kwa kinguvu, na wakubwa wao wanayagandamiza. 26 Lakini isikuwe hivi katikati yenu. Anayetaka kuwa mukubwa kati yenu, sherti akuwe mutumishi wenu. 27 Naye anayetaka kuwa wa kwanza, sherti akuwe mutumwa wenu. 28 Kwa maana Mwana wa Mutu hakukuja kutumikiwa, lakini kutumikiana na kutoa maisha yake kusudi awakomboe watu wengi.” Yesu anaponyesha vipofu wawili ( Mk 10.46-52 ; Lk 18.35-43 ) 29 Yesu na wanafunzi wake walipokuwa wakitoka Yeriko, kundi kubwa la watu wakamufuata. 30 Na kulikuwa vipofu wawili waliokuwa wakiikaa pembeni ya njia, nao wakasikia kwamba Yesu anapita. Kwa hiyo wakalalamika, wakisema: “Bwana, mwana wa Daudi, utusikilie huruma!” 31 Kundi la watu wakawakaripia na kuwaambia wanyamaze. Lakini wale vipofu wakaendelea kulalamika kwa nguvu, wakisema: “Mwana wa Daudi, utusikilie huruma!” 32 Yesu akasimama na kuwaita. Akawauliza: “Munataka niwafanyie nini?” 33 Nao wakamujibu: “Bwana, tunakuomba utuponyeshe macho.” 34 Yesu akawasikilia huruma. Akagusa macho yao, na mara moja wakapata kuona, nao wakamufuata. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo