Matayo 17 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yesu anageuzwa sura ( Mk 9.2-13 ; Lk 9.28-36 ) 1 Nyuma ya siku sita, Yesu aliwatwaa Petro, Yakobo na ndugu yake Yoane, na kuwapeleka kwenye mulima murefu. Nao walikuwa kule peke yao. 2 Na kule sura ya Yesu ikageuka wazi mbele yao. Uso wake ukangaa kama jua, nazo nguo zake zikametameta kama mwangaza. 3 Halafu Musa na Elia wakiwa wakisemezana na Yesu, wakawatokea wale wanafunzi. 4 Basi Petro akamwambia Yesu: “Bwana, ni vizuri kuona kwamba sisi tuko hapa. Ukitaka, nitajenga hapa vibanda vitatu, kimoja chako, kimoja cha Musa na kingine cha Elia.” 5 Naye alipokuwa angali akisema, wingu lenye kuangaza likawafunika, na sauti ikasikilika toka katikati ya lile wingu ikisema: “Huyu ni Mwana wangu mupendwa, ninapendezwa naye sana. Mumusikilize!” 6 Wanafunzi wale waliposikia sauti ile, wakaogopa sana, wakaanguka uso mpaka chini. 7 Lakini Yesu akawajongelea, akawagusa na kuwaambia: “Musimame, musiogope.” 8 Nao walipoinua macho yao, hawakumwona mutu mwingine, isipokuwa Yesu peke yake. 9 Walipokuwa wakishuka toka kwa mulima, Yesu akawaamuru: “Musimwelezee mutu mambo muliyoona mpaka Mwana wa Mutu atakapofufuka.” 10 Kisha wanafunzi wakamwuliza: “Kwa nini basi walimu wa Sheria wanasema kwamba sherti Elia arudi kwanza?” 11 Yesu akawajibu: “Hakika Elia anapaswa kurudi kwanza kutengeneza mambo yote. 12 Lakini ninawaambia kama Elia amekwisha kurudi, nao hawakumutambua, lakini walimutendea yote waliyotaka. Ni vile ndivyo Mwana wa Mutu atateswa nao vilevile.” 13 Halafu wanafunzi wakafahamu kwamba alisema nao juu ya Yoane Mubatizaji. Yesu anaponyesha mwenye kifafa ( Mk 9.14-29 ; Lk 9.37-43a ) 14 Yesu na wanafunzi wake waliendelea hata wakafika kwenye kundi la watu. Pale mutu mumoja akamwendea Yesu, akapiga magoti mbele yake, 15 na kusema: “Bwana, ninakuomba umusikilie mwana wangu huruma kwa maana anateswa sana na ugonjwa wa kifafa. Mara nyingi anaanguka katika moto na ndani ya maji. 16 Nilimuleta kwa wanafunzi wako, lakini hawakuweza kumuponyesha.” 17 Na Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Ee ninyi watu wa kizazi kisichoamini Mungu na chenye kupotoka. Nitakaa pamoja nanyi tena mpaka wakati gani? Nitawavumilia tena mpaka wakati gani? Muniletee mutoto hapa.” 18 Yesu akamukaripia yule pepo aliyekuwa ndani ya yule mutoto, naye akamwacha, na tangia saa ile ile yule mutoto akapona. 19 Kisha wanafunzi wakamufikia Yesu, wakiwa peke yao, na kumwuliza: “Kwa nini sisi hatukuweza kumufukuza yule pepo?” 20 Yesu akawajibu: “Kwa sababu imani yenu ni ndogo. Kweli ninawaambia kama mukiwa na imani, hata ikiwa tu kama punje ndogo sana ya mbegu ya haradali, mutaweza kuuambia mulima huu: ‘Toka hapa uende kule,’ nao utatoka pale. Hakuna kitu chochote kitakachokosa kuwezekana kwenu. [ 21 Lakini pepo wa namna hii hawawezi kufukuzwa isipokuwa tu kwa njia ya maombi na kufunga kula chakula.]” Yesu anajulisha tena habari za kufa na kufufuka kwake ( Mk 9.30-32 ; Lk 9.43b-45 ) 22 Wanafunzi walipokuwa pamoja katika jimbo la Galilaya, Yesu akawaambia: “Mwana wa Mutu atatolewa katika mikono ya watu, 23 nao watamwua, lakini kwa siku ya tatu kisha kufa kwake, atafufuka.” Halafu wanafunzi wakahuzunika sana. Kulipa kodi ya hekalu 24 Yesu na wanafunzi wake walipofika katika muji Kapernaumu, walipishaji wa kodi ya hekalu wakamwendea Petro na kumwuliza: “Si mwalimu wenu analipa kodi ya hekalu?” 25 Petro akawajibu: “Ndiyo, analipa.” Petro alipoingia ndani ya nyumba, mbele hajasema kitu Yesu akamwuliza: “Simoni, unafikiri nini? Wafalme wa dunia wanawalipisha watu gani kodi au malipo mengine mbalimbali? Ni watu wa jamaa zao wenyewe au watu wengine?” 26 Petro akamujibu: “Watu wengine.” Na Yesu akamwambia: “Basi ni kusema kwamba watu wa jamaa zao wako na ruhusa ya kutolipa. 27 Lakini haifai kuwakwaza. Kwa hiyo kwenda kwenye ziwa, na utupe ndoana ndani ya maji. Na samaki wa kwanza utakayemunasa, ufungue kinywa chake, nawe utaona kikoroti cha feza. Ukikamate na kukitoa kwa kulipa kodi kwa ajili yetu sisi wawili.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo