Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Matayo 13 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mufano wa mupandaji wa mbegu
( Mk 4.1-9 ; Lk 8.4-8 )

1 Siku ile ile, Yesu akatoka ndani ya nyumba na kwenda kuikaa pembeni ya ziwa kwa kufundisha.

2 Na kuona kundi kubwa la watu waliokusanyika karibu naye, akapanda ndani ya chombo na kukaa humo, nao watu walibaki wakisimama inchi kavu.

3 Halafu akawafundisha mambo mengi akitumia mifano, akasema: “Mutu mumoja alikwenda kupanda mbegu.

4 Alipokuwa akipanda mbegu katika shamba lake, zimoja zikaanguka pembeni ya njia, nao ndege wakakuja na kuzikula.

5 Zingine zikaanguka pahali penye mawe, pasipokuwa udongo mwingi. Nazo zikaota upesi, kwa sababu hapakukuwa udongo mwingi.

6 Wakati jua lilipokuwa kali, likazichoma, na kwa sababu hazikukuwa na mizizi mikubwa, zikakauka.

7 Mbegu zingine zikaanguka katikati ya miiba. Ile miiba ikaota na kuzisonga.

8 Lakini mbegu zingine zikaanguka katika udongo muzuri na kutoa matunda: zimoja zikazaa punje mia moja, zingine makumi sita na zingine makumi tatu.

9 Basi mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!”


Kusudi la kutmia mifano
( Mk 4.10-12 ; Lk 8.9-10 )

10 Wanafunzi wa Yesu wakamwendea na kumwuliza: “Kwa sababu gani unasema na watu hawa ukitumia mifano?”

11 Akawajibu: “Ninyi mumefunuliwa kujua siri ya Ufalme wa mbinguni, lakini kwao si vile.

12 Kwa maana mutu anayekuwa na kitu ataongezewa kingine, naye atakuwa na vitu vingi. Lakini mutu asiyekuwa na kitu, ataondolewa hata kile kidogo anachokuwa nacho.

13 Ni kwa sababu hiyo ninasema nao kwa kutumia mifano: kwa kuwa wanaangalia, lakini hawaoni, nao wanasikiliza lakini hawasikii wala hawafahamu.

14 Hivi yametimia kwao maneno haya yaliyosemwa na Mungu kwa njia ya nabii Isaya: ‘kusikia, mutasikia, lakini hamutafahamu; kuangalia, mutaangalia, lakini hamutaona.

15 Maana mioyo ya watu hawa imegeuka migumu, wameziba masikio yao, nao wamefunga macho yao, kusudi wasipate kuona, nao wasipate kusikia, wala wasipate kunigeukia, nami ningewaponyesha.’

16 “Lakini heri kwenu, kwa sababu macho yenu yanaona na masikio yenu yanasikia!

17 Kweli ninawaambia: manabii wengi na wenye haki wengi walitamani kuona mambo munayoona, lakini hawakuyaona, na kusikia maneno munayosikia, lakini hawakuyasikia.


Yesu anaeleza mufano wa mupandaji
( Mk 4.13-20 ; Lk 8.11-15 )

18 “Basi musikilize maana ya ule mufano wa mupandaji wa mbegu.

19 Pahali zile mbegu zilipoanguka pembeni ya njia, ni mufano wa watu wanaosikia habari ya Ufalme na kukosa kuielewa. Na kisha yule mwovu Shetani anakuja na kuondoa mbegu zilizopandwa ndani ya mioyo yao.

20 Udongo wenye mawe pahali mbegu zilipoanguka ni mufano wa watu wanaosikia Neno la Mungu, na mara moja wanalipokea kwa furaha.

21 Lakini halizami ndani yao kama mizizi. Wanalishika kwa muda mufupi tu. Wakati taabu na mateso vinapowafikia kwa ajili ya Neno la Mungu, mara moja, wanaanguka.

22 Pahali zile mbegu zilipoanguka katika miiba, ni mufano wa wale wanaosikia Neno la Mungu, lakini masumbuko ya dunia hii na udanganyifu wa mali vinasonga lile neno linalokuwa ndani yao na kulizuiza kuzaa matunda.

23 Pahali zile mbegu zilipoanguka katika udongo muzuri ni mufano wa watu wanaosikia Neno la Mungu na kulielewa. Nao wanazaa matunda; wamoja matunda mia moja, wengine makumi sita na wengine makumi tatu.”


Mufano wa nyasi

24 Yesu akawaambia mufano mwingine, akisema: “Ufalme wa mbinguni unafanana na mutu mumoja aliyepanda mbegu nzuri ya ngano katika shamba lake.

25 Lakini siku moja usiku, wote walipokuwa wakilala usingizi, adui wa mutu yule akakuja na kupanda nyasi katikati ya ngano; kisha akajiendea.

26 Ngano ilipoota na kutoa masuke, nyasi zikaonekana vilevile.

27 Watumishi wa mwenye shamba wakamwendea na kumwuliza: ‘Ee Bwana, si ulipanda mbegu nzuri katika shamba lako? Basi nyasi hizi zimetoka wapi?’

28 Naye akawajibu: ‘Ni adui aliyefanya vile.’ Basi watumishi wakamwuliza: ‘Unataka tuende kuongoa zile nyasi?’

29 Lakini akajibu: ‘Hapana, mukiongoa nyasi, labda mutafikia kuongoa ngano pamoja nazo.

30 Muviache vyote viwili vikomae pamoja mpaka wakati wa mavuno. Wakati ule nitawaambia wavunaji: muongoe kwanza nyasi, nanyi muzilundike kwa mafungu mafungu kwa kuzichoma, na kisha mukusanye ngano na kuweka mavuno ndani ya gala yangu.’ ”


Mufano wa mbego ndogo sana ya haradi
( Mk 4.30-32 ; Lk 13.18-19 )

31 Yesu akawaambia mufano mwingine akisema: “Ufalme wa mbinguni unafanana na mbegu ya haradali mutu mumoja aliyoitwaa na kuipanda katika shamba lake.

32 Mbegu hii ni ndogo sana kuliko mbegu zote, lakini inapokwisha kuota, inakuwa kubwa zaidi kuliko mimea yote, hata ndege wanakuja na kujenga chicha zao katikati ya matawi yake.”


Mufano wa chachu
( Lk 13.20-21 )

33 Yesu akawaambia tena mufano mwingine, akisema: “Ufalme wa mbinguni unafanana na chachu mwanamuke mumoja aliyoitwaa na kuichanga na vipimo vitatu vya unga kwa kuponda mikate hata yote ikapata kuvimba.”


Kusudi la Yesu la kutumia mifano
( Mk 4.33-34 )

34 Yesu aliwaambia makundi ya watu maneno hayo yote akitumia mifano. Yeye hakusema nao pasipo kutumia mifano.

35 Ilitokea vile kusudi yatimie maneno yaliyosemwa kwa njia ya nabii: “Nitasema nao kwa mifano, nitawaambia maneno yaliyofichwa tangu kuumbwa kwa dunia.”


Yesu anaeleza mufano wa nyasi

36 Halafu Yesu akaagana na makundi ya watu na kurudi kwenye nyumba. Wanafunzi wake wakamwendea na kumwambia: “Utufasirie maana ya ule mufano wa nyasi katika shamba.”

37 Naye akawajibu: “Yule anayepanda mbegu nzuri ni Mwana wa Mutu.

38 Shamba ni dunia. Mbegu nzuri ni washiriki wa Ufalme. Nyasi ni washiriki wa yule Mwovu Shetani.

39 Adui aliyepanda nyasi ni Shetani. Mavuno ni mwisho wa dunia, nao wavunaji ni wamalaika.

40 Kama vile nyasi zinavyoongolewa kwa kuchomwa katika moto, ndivyo itakavyokuwa vilevile kwa mwisho wa dunia.

41 Mwana wa Mutu atawatuma wamalaika wake, nao watakusanya toka katika Ufalme wake watu wote wanaowaangusha wengine katika zambi pamoja na wote wanaofanya maovu.

42 Nao watawatupa ndani ya furu la moto, na mule watalia na kusaga meno.

43 Lakini wenye haki watametameta kama jua katika Ufalme wa Baba yao. Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!”


Mufano wa mali iliyofichwa katika shamba

44 “Ufalme wa mbinguni unafanana na mali iliyofichwa katika shamba moja. Mutu mumoja alipoiona, akaificha tena. Halafu kwa furaha kubwa akaenda kuuzisha vitu vyake vyote na kununua lile shamba.


Mufano wa ushanga wa bei kali

45 “Ufalme wa mbinguni unafanana vilevile na muchuuzi mumoja aliyetafuta kununua ushanga muzuri.

46 Alipoona ushanga mumoja muzuri sana, akaenda kuuzisha vitu vyake vyote na kuununua.


Mufano wa wavu

47 “Ufalme wa mbinguni unafanana vilevile na wavuvi wamoja waliotupa wavu ndani ya ziwa, nao ukakusanya samaki wa kila namna.

48 Wakati wavu ulipojaa, wavuvi wakaukokota inchi kavu. Halafu wakaikaa kwa kuchagua samaki: wakaweka samaki wazuri ndani ya vyombo na kutupa samaki wabaya.

49 Ni hivi itakavyokuwa kwa mwisho wa dunia. Wamalaika watakuja na kuwatenga watu wabaya na watu wazuri.

50 Na halafu watawatupa watu wabaya ndani ya furu la moto; na mule watalia na kusaga meno.”


Mufano wa vitu vipya na vya zamani

51 Yesu akawauliza watu: “Mumeelewa maneno hayo yote?” Nao wakamujibu: “Ndiyo.”

52 Kisha akawaambia: “Basi, kila mwalimu wa Sheria aliyefundishwa katika Ufalme wa mbinguni, anafanana na mwenye nyumba anayetwaa vitu vipya na vitu vya zamani pamoja toka katika akiba yake.”


Watu wa Nazareti wanamukataa Yesu
( Mk 6.1-6 ; Lk 4.16-30 )

53 Yesu alipomaliza kusema mifano hiyo, akaondoka kule

54 na kwenda katika muji wake mwenyewe. Kule akaanza kuwafundisha watu katika nyumba zao za kuabudia, nao walishangaa na kuuliza: “Huyu amepata hekima na miujiza hii kutoka wapi?

55 Huyu si mwana wa yule seremala? Mama yake si Maria? Nao Yakobo, Yosefu, Simoni na Yuda si wandugu zake?

56 Na wadada zake, si wanaishi hapa kati yetu? Basi amepata mambo haya yote kutoka wapi?”

57 Na kwa hiyo akakuwa kikwazo kwao. Lakini Yesu akawaambia: “Nabii hakosewi heshima fasi zote, isipokuwa tu katika muji wake na katika jamaa yake.”

58 Na hivi kwa sababu ya kutokuamini kwa watu hao, Yesu hakufanya miujiza mingi kule.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan