Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Matayo 11 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Wajumbe wa Yoane Mubatizaji
( Lk 7.18-35 )

1 Yesu alipomaliza kutoa maagizo hayo kwa wanafunzi wake kumi na wawili, akaondoka kule, akaenda kufundisha na kuhubiri katika miji ya inchi ile.

2 Yoane Mubatizaji, akiwa katika kifungo, akapata habari za mambo Kristo aliyokuwa akifanya. Basi akawatuma wanafunzi wake

3 kumwuliza Yesu: “Wewe ndiwe yule aliyepaswa kuja kutuokoa au tumungojee mwingine?”

4 Yesu akawajibu: “Mwende kumwelezea Yoane mambo munayosikia na kuyaona:

5 vipofu wanapata kuona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanapata kusikia, wafu wanafufuliwa na Habari Njema inahubiriwa kwa wamasikini.

6 Heri mutu yule mimi sitakayekuwa kikwazo kwake!”

7 Wale wanafunzi wa Yoane walipoondoka, Yesu akaanza kuwaambia makundi ya watu habari za Yoane: “Mulienda katika jangwa kwa kuangalia nini? Tete linalotikiswa na upepo? Hapana!

8 Basi mulienda kuona nini? Mutu aliyevaa nguo nzuri? Hapana! Wale wanaovaa nguo nzuri wanakaa katika nyumba za wafalme.

9 Basi mulikwenda kuona nini? Nabii? Ndiyo, ninawaambia, yeye ni mukubwa kupita hata nabii.

10 Huyu ndiye maneno haya yameandikwa juu yake katika Maandiko Matakatifu: ‘Ninamutuma mujumbe wangu akutangulie, kusudi akutengenezee njia utakayopitia!’

11 “Kweli ninawaambia: kati ya watu wanaoishi katika dunia, hakuna mutu anayekuwa mukubwa kuliko Yoane Mubatizaji. Lakini yeyote anayeonekana kuwa mudogo katika Ufalme wa mbinguni anahesabiwa kuwa mukubwa kuliko yeye.

12 Tangia wakati Yoane Mubatizaji alipohubiri mpaka sasa, watu wanapinga Ufalme wa mbinguni, nao watu wakali wanajaribu kuukamata kwa kinguvu.

13 Kwa maana mambo hayo yalitangazwa na manabii wote na Sheria ya Musa mpaka wakati wa Yoane.

14 Na ikiwa munasadiki, Yoane ndiye nabii Elia aliyepaswa kuja.

15 Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!

16 “Nitawafananisha watu wa kizazi hiki na nini? Wanafanana na watoto wanaoikaa kwenye nafasi ya makutano na kuita wenzao wakisema:

17 ‘Tuliwapigia ngoma, lakini hamukucheza! Tuliimba wimbo wa kilio, lakini hamukulia!’

18 Kwa maana Yoane alikuja, alifunga kula chakula na kunywa, nao wakasema: ‘Yuko na pepo!’

19 Mwana wa Mutu alikuja, yeye anakula na kunywa, nao wanasema: ‘Angalia huyu mulafi na mulevi, rafiki wa walipishaji wa kodi na watenda maovu wenzao.’ Lakini hekima ya Mungu ilionyeshwa kuwa ya haki kwa njia ya matendo yake.”


Azabu ya miji iliyokataa kumwamini Yesu
( Lk 10.13-15 )

20 Kisha Yesu akaanza kuonya miji ambamo alifanya miujiza mingi zaidi, kwa sababu wakaaji wa kule hawakugeuka toka zambi zao. Akasema:

21 “Ole kwako, muji Korazini! Ole kwako, muji Betesaida! Kwa maana miujiza iliyofanyika ndani yenu ingalifanyika katika muji wa Tiro na muji wa Sidona, wakaaji wa kule wangekwisha zamani kuvaa magunia na kujipakaa majivu, kwa kuonyesha kwamba wamegeuka toka zambi zao.

22 Kwa hiyo ninawaambia kwamba kwa Siku ya hukumu, ninyi mutaazibiwa zaidi kuliko muji wa Tiro na wa Sidona.

23 Nawe, muji Kapernaumu, unafikiri kwamba utapandishwa mpaka juu mbinguni? Utashushwa mpaka chini katika kuzimu. Kwa maana miujiza iliyofanyika ndani yako ingalifanyika katika Sodoma, muji ule ungekuwa ungali hata leo.

24 Kwa hiyo ninawaambia kwamba kwa Siku ya hukumu, wewe utaazibiwa zaidi kuliko watu wa Sodoma!”


Yesu anamushukuru Mungu
( Lk 10.21-22 )

25 Katika siku zile Yesu akasema: “Ee Baba, Mwenyeji wa mbingu na dunia, ninakushukuru kwa maana mambo uliyoyaficha kwa watu wenye hekima na elimu, umeyafunua kwa wanaokuwa wadogo.

26 Ndiyo, Baba, hayo yote ni kutokana na mapenzi yako.

27 “Baba yangu ameweka vitu vyote katika mikono yangu. Hakuna mutu anayemujua Mwana isipokuwa Baba, wala hakuna anayemujua Baba isipokuwa Mwana, na yeyote Mwana anayetaka kumujulisha kwake.


Maonyo kwa wenye kusumbuka

28 “Mukuje kwangu ninyi wote munaosumbuka na kulemewa na mizigo mizito, nami nitawapumzisha.

29 Mukubali kuongozwa nami kama vile ngombe dume anayefungiwa nira, nanyi mufuate mafundisho yangu maana mimi ni mupole na munyenyekevu. Kwa hiyo mutapumzika.

30 Nira yangu si nzito, nao muzigo nitakaowabebesha ni mwepesi.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan