Marko 8 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yesu anakulisha watu elfu ine ( Mat 15.32-39 ) 1 Katika siku zile kundi kubwa la watu walikusanyika tena. Nao walipokosa chakula, Yesu akawaita wanafunzi wake, na kuwaambia: 2 “Ninawasikilia watu hawa huruma, kwa sababu wamekaa nami sasa muda wa siku tatu, nao hawana chakula tena. 3 Kama nikiwaambia waende kwao pasipo kula wataregea katika njia, kwa maana wamoja kati yao wametoka mbali.” 4 Wanafunzi wake wakamujibu: “Hapa katika pori mutu ataweza kupata wapi chakula cha kuwashibisha?” 5 Yesu akawauliza: “Muko na mikate ngapi?” Nao wakamujibu: “Tuko na mikate saba.” 6 Basi Yesu akawaamuru watu waikae chini. Kisha akakamata ile mikate saba, akamushukuru Mungu, akaimega na kuwapa wanafunzi wake waigawanye kwa watu; nao wanafunzi wakaigawanya. 7 Walikuwa vilevile na samaki ndogo chache. Yesu akamushukuru Mungu na kuwaambia wanafunzi wazigawanye vilevile. 8 Wote walikula na kushiba. Kisha wanafunzi wakaokota vipande vya mikate na vya samaki vilivyobaki, wakajaza vitunga saba. 9 Watu waliokula walikuwa yapata elfu ine. Kisha kuagana nao, 10 mara moja Yesu akaingia ndani ya chombo pamoja na wanafunzi wake, akaenda katika jimbo la Dalmanuta. Wafarisayo wanataka kitambulisho ( Mat 16.1-4 ) 11 Wafarisayo wakamufikia Yesu na kuanza kubishana naye. Wakamupima wakimwomba awaonyeshe kitambulisho kinachohakikisha kwamba uwezo wake umetoka kwa Mungu. 12 Yesu akaugua sana kwa huzuni, na kusema: “Sababu gani ninyi watu wa kizazi hiki munataka kuona kitambulisho? Kweli ninawaambia, hamutaonyeshwa kitambulisho!” 13 Kisha akawaacha, akaingia tena ndani ya chombo, akaanza kuvuka ziwa. Chachu ya Wafarisayo na ya Herode ( Mat 16.5-12 ) 14 Wanafunzi walikuwa wamesahau kupeleka mikate, isipokuwa walikuwa na mukate mumoja tu ndani ya chombo. 15 Yesu akawaagiza: “Mujiangalie vizuri, mujiepushe na chachu ya Wafarisayo na ya Herode.” 16 Wanafunzi wakaanza kusemezana: “Anasema hivi kwa sababu hatuna mikate.” 17 Yesu akatambua maneno waliyosema, basi akawauliza: “Sababu gani munasemezana juu ya kukosa mikate? Hamujafahamu wala kuelewa? Mioyo yenu ingali migumu? 18 Muko na macho, lakini hamwoni? Muko na masikio, lakini hamusikii? Hamukumbuki 19 wakati nilipomega mikate mitano na kulisha watu elfu tano? Wakati ule mulijaza vitunga ngapi na vipande vya mikate?” Wakajibu: “Kumi na viwili.” 20 Naye akawauliza tena: “Na wakati nilipomega mikate saba na kulisha watu elfu ine, mulijaza vitunga ngapi na vipande vya mikate?” Wakamujibu: “Saba.” 21 Basi Yesu akawauliza: “Na hata sasa hamujaelewa kitu?” Yesu anaponyesha kipofu wa Betesaida 22 Yesu na wanafunzi wake wakafika Betesaida. Kule wakamuletea Yesu mutu mumoja kipofu na kumwomba amuguse kusudi apate kupona. 23 Yesu akashika mukono wa yule kipofu na kumupeleka inje ya kijiji. Yesu alipokwisha kupakaa mate kwa macho ya mutu yule na kuweka mikono juu yake, akamwuliza: “Unaona kitu?” 24 Kipofu akainua macho yake na kusema: “Ninaona watu wakitembea, lakini wanaonekana kama miti.” 25 Yesu akagusa tena macho ya yule kipofu, naye akapata kuona vizuri. Macho yake yakapona, na kupata kuona vitu vyote waziwazi. 26 Kisha Yesu akamwomba arudie kwake, akimwagiza asirudi katika kijiji. Petro anajulisha kwamba Yesu ni Kristo ( Mat 16.13-20 ; Lk 9.18-21 ) 27 Yesu na wanafunzi wake wakaenda pande za vijiji vilivyokuwa karibu na muji Kaisaria Filipi. Walipokuwa katika njia yeye akawauliza: “Watu wanasema kwamba mimi ni nani?” 28 Nao wakamujibu: “Wamoja wanasema kwamba wewe ni Yoane Mubatizaji; wengine wanasema kwamba wewe ni nabii Elia na wengine wanasema kwamba wewe ni mumoja wa manabii wengine.” 29 Halafu Yesu akawauliza: “Na ninyi munasema kwamba mimi ni nani?” Petro akamujibu: “Wewe ni Kristo.” 30 Basi Yesu akawaagiza wasimwambie mutu neno lile. Yesu anajulisha habari za kufa na kufufuka kwake ( Mat 16.21-28 ; Lk 9.22-27 ) 31 Kisha Yesu akaanza kuwafundisha wanafunzi wake, akisema: “Sherti Mwana wa Mutu ateswe na kukataliwa na wasimamizi wa watu, wakubwa wa makuhani pamoja na walimu wa Sheria. Atauawa na kwa siku ya tatu kisha kufa kwake atafufuka.” 32 Yeye aliwaambia maneno hayo waziwazi. Basi Petro akamwita Yesu pembeni na kuanza kumukaripia. 33 Lakini Yesu akawageukia wanafunzi wake na kumukaripia Petro akisema: “Ondoka hapa karibu nami wewe Shetani, kwa maana mawazo yako si ya Mungu lakini ni ya kimutu.” Namna ya kufuata Yesu 34 Kisha Yesu akaita kundi la watu pamoja na wanafunzi wake, na kuwaambia: “Kama mutu akitaka kunifuata, asijishugulikie mwenyewe, lakini ajitolee kwa kubeba musalaba wake na kunifuata. 35 Kwa maana mutu anayetaka kulinda uzima wake, ataupoteza; lakini yule atakayetoa uzima wake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Habari Njema, ataulinda. 36 Ni faida gani kwa mutu kupata utajiri wote wa dunia, lakini anapoteza uzima wake? 37 Hakuna kitu chochote mutu anachoweza kutoa kwa kukomboa uzima wake. 38 Kwa hiyo mutu yeyote anayesikia haya juu yangu na juu ya mafundisho yangu kati ya watu wa kizazi hiki kisichokuwa na uaminifu mbele ya Mungu na chenye zambi, Mwana wa Mutu atasikia haya juu yake vilevile. Itakuwa vile, atakapokuja pamoja na wamalaika watakatifu, akitukuzwa na Baba yake.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo