Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Marko 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Desturi za babu
( Mat 15.1-9 )

1 Wafarisayo na walimu wamoja wa Sheria waliotoka Yerusalema wakakusanyika mbele ya Yesu.

2 Wakawaona wanafunzi wake wamoja wakikula chakula na mikono michafu, maana yake, mikono waliyokosa kunawa kufuatana na desturi ya dini yao.

3 Ilikuwa vile kwa maana Wafarisayo na Wayuda wote wanashika desturi za babu zao; zinazokataza kula pasipo kunawa mikono kama inavyostahili.

4 Tena, wanapotoka kwa soko, hawakuli pasipo kuoga kwanza. Na zaidi ya hii wanashika desturi zingine nyingi kama vile namna ya kusafisha vikombe, mitungi na vyungu vilivyotengenezwa na shaba.

5 Basi Wafarisayo na walimu wa Sheria wakamwuliza Yesu: “Sababu gani wanafunzi wako hawafuati desturi za babu zetu, lakini wanakula chakula na mikono michafu?”

6 Yesu akawajibu: “Isaya alitabiri vema wakati alipoandika maneno haya juu yenu ninyi wanafiki: ‘Mungu anasema: Watu hawa wananiheshimu kwa midomo yao, lakini mioyo yao ni mbali nami.

7 Ibada wanayonifanyia ni ya bure, sababu mafundisho yao yanalingana na kanuni za watu tu.’ ”

8 Yesu akaendelea kuwaambia: “Munaacha amri za Mungu pembeni na kushika desturi za watu.

9 Munajua vizuri namna ya kutupilia amri za Mungu kusudi mushike desturi zenu!

10 Maana Musa alisema: ‘Uwaheshimu baba yako na mama yako,’ na, ‘Anayemutukana baba yake au mama yake, anapaswa kuuawa.’

11 Lakini ninyi munasema kwamba mutu akiwa na kitu cha kumusaidia baba au mama yake, lakini akimwambia kwamba kitu kile ni Korbane, (maana yake, kimetolewa kuwa sadaka takatifu kwa Mungu),

12 munamuruhusu asiwasaidie wazazi wake.

13 Hivi munazarau Neno la Mungu kwa ajili ya desturi zenu munazopokezana. Nanyi munafanya mambo mengine mengi ya namna ile.”


Mambo yanayomuchafua mutu
( Mat 15.10-20 )

14 Kisha Yesu akaita tena kundi la watu na kuwaambia: “Ninyi wote munisikilize na kuelewa maneno haya.

15 Hakuna kitu kinachoingia ndani ya mutu kutoka inje kinachoweza kumuchafua. Lakini kitu kinachotoka ndani yake ndicho kinachomuchafua. [

16 Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie.]”

17 Wakati Yesu alipoachana na kundi na kuingia ndani ya nyumba, wanafunzi wake wakamwuliza maana ya mufano ule.

18 Naye akawaambia: “Hata ninyi vilevile hamuwezi kuelewa? Hamufahamu kwamba kila kitu kinachoingia ndani ya mutu kutoka inje hakiwezi kumuchafua?

19 Kitu kile hakiingii ndani ya moyo wake, lakini kinaingia tu ndani ya tumbo na kisha kinatoka na kwenda katika choo.” (Kwa kusema hivi Yesu alionyesha kwamba vyakula vyote vinaruhusiwa kukuliwa.)

20 Yesu akaongeza kusema: “Ni kile kinachotoka ndani ya mutu ndicho kinachomuchafua.

21 Kwa maana ni ndani ya mutu, ni kusema ndani ya moyo wake, ndimo munamotoka mawazo mabaya yanayoleta: uzinzi, wizi, uuaji,

22 uasherati, tamaa mbaya, matendo mabaya, ukorofi, maisha ya ovyo, wivu, matukano, majivuno na upumbafu.

23 Maovu haya yote yanatoka ndani ya mutu, nayo yanamufanya kuwa muchafu.”


Imani ya mwanamuke Musuria
( Mat 15.21-28 )

24 Kisha Yesu akaondoka pale, na kwenda katika jimbo lililokuwa karibu na muji Tiro. Akaingia ndani ya nyumba, naye hakutaka mutu ajue kwamba yuko mule, lakini haikuwezekana kwake kujificha.

25 Mwanamuke mumoja, binti yake aliyeshikwa na pepo, akasikia habari za Yesu. Mara moja akamufikia Yesu na kujitupa kwa miguu yake.

26 Mwanamuke yule hakukuwa wa taifa la Wayuda. Alikuwa muzaliwa wa jimbo la Foinikia, katika inchi ya Suria. Yeye akamwomba Yesu afukuze yule pepo kutoka ndani ya binti yake.

27 Lakini Yesu akamujibu: “Uwaache kwanza watoto wa nyumba washibe, kwa sababu si vizuri kukamata chakula cha watoto na kukitupia imbwa.”

28 Mwanamuke yule akamujibu: “Bwana, unasema ukweli, lakini hata imbwa wanazoea kula makombo watoto wanayoyaangusha chini ya meza.”

29 Basi Yesu akamwambia: “Kwa sababu ya jibu hili, unaweza kurudi kwako, yule pepo ametoka ndani ya binti yako.”

30 Mwanamuke yule alipofika kwake, akamwona binti yake akilala katika kitanda; na yule pepo alikuwa amekwisha kutoka ndani yake.


Yesu anaponyesha kiziwi

31 Kisha Yesu akaondoka kule katika jimbo lililokuwa karibu na Tiro, akapita Sidona na katikati ya inchi ya Miji Kumi, hata akafika kwenye ziwa la Galilaya.

32 Wakamuletea mutu mumoja aliyekuwa kiziwi na mwenye kigugumizi vilevile. Wale waliomuleta wakamusihi Yesu amuponyeshe kwa kuweka mikono juu yake.

33 Basi Yesu akamwondoa yule mutu kati ya kundi, akaenda naye mbali kidogo, akamutia vidole ndani ya masikio, akatema mate na kumugusa ulimi kwa mate yale.

34 Kisha Yesu akaangalia juu mbinguni, akasisimua na kumwambia yule mutu: “Efata,” maana yake, “Funguka!”

35 Mara moja masikio yake yakafunguka, nao ulimi wake ukafunguliwa, akaanza kusema vizuri.

36 Yesu akawaagiza wasimwambie mutu habari ya tendo hili. Lakini kwa kadiri alivyowakataza, wao walizidi kutangaza habari.

37 Nao watu wakashangaa sana na kusema: “Mambo anayofanya ni mazuri kweli. Anawawezesha hata viziwi wasikie, nao wabubu wapate kusema.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan