Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Marko 6 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Watu wa Nazareti wanamukataa Yesu
( Mat 13.53-58 ; Lk 4.16-30 )

1 Yesu akatoka kule, akaenda katika muji wake wa kuzaliwa, nao wanafunzi wake wakamufuata.

2 Siku ya Sabato ilipotimia, akaanza kufundisha katika nyumba ya kuabudia. Watu wengi waliomusikiliza, wakashangaa sana na kuulizana: “Huyu amepata maneno haya yote kutoka wapi? Ni hekima ya namna gani aliyopata? Ni kwa uwezo wa namna gani anafanya miujiza kama hii?

3 Huyu si yule museremala, mwana wa Maria, ndugu ya Yakobo, Yose, Yuda na Simoni? Nao wadada zake, si wanaishi hapa kati yetu?” Na kwa hiyo wakakosa kumwaminia.

4 Lakini Yesu akawaambia: “Nabii hakosewi heshima fasi zote, isipokuwa tu katika muji wake, katikati ya wandugu zake na katika jamaa yake.”

5 Kwa hiyo Yesu hakuweza kufanya muujiza wowote kule, isipokuwa aliweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache na kuwaponyesha.

6 Naye alishangaa sana kwa sababu ya kutokuamini kwa watu wale. Kisha Yesu akazunguka katika vijiji vya kandokando akiwafundisha watu.


Yesu anawatuma wanafunzi kumi na wawili
( Mat 10.5-15 ; Lk 9.1-6 )

7 Aliwaita wanafunzi wake kumi na wawili, akaanza kuwatuma wawili wawili na kuwapatia uwezo wa kufukuza pepo.

8 Akawaagiza: “Musibebe kitu chochote kwa safari yenu isipokuwa fimbo tu. Musibebe chakula, mufuko, wala feza ndani ya mikaba yenu.

9 Muvae viatu lakini musivae kanzu mbili.”

10 Akawaambia tena: “Nafasi yoyote watakapowakaribisha ndani ya nyumba, mubakie mule mpaka mutakapotoka kule.

11 Na nafasi yoyote watu watakapokataa kuwakaribisha na kuwasikiliza, mutoke kule na mukungute mavumbi toka juu ya miguu yenu. Jambo hili litakuwa ushuhuda juu yao.”

12 Basi wanafunzi wakaondoka, wakahubiri watu kwamba wageuke toka zambi zao.

13 Wakafukuza pepo wengi, na wakapakaa wagonjwa wengi mafuta na kuwaponyesha.


Kufa kwa Yoane Mubatizaji
( Mat 14.1-12 ; Lk 9.7-9 )

14 Mufalme Herode alisikia habari za Yesu, kwa maana jina lake lilikuwa limevuma fasi zote. Watu wamoja walisema: “Huyu ni Yoane Mubatizaji aliyefufuka! Ni kwa sababu hii amepata uwezo wa kufanya miujiza.”

15 Lakini wengine walisema: “Huyu ni nabii Elia.” Wengine walisema: “Yeye ni nabii sawa na mumoja wa wale manabii wa zamani.”

16 Lakini Herode aliposikia habari zile, akasema: “Ni yule Yoane Mubatizaji niliyemukata kichwa ndiye amefufuka!”

17 Ni Herode mwenyewe aliyeamuru kwamba Yoane akamatwe na kutiwa katika kifungo. Ilitokea vile kwa sababu Herode alimwoa Herodia, muke wa ndugu yake Filipo.

18 Yoane alikuwa amemwambia kwamba hana sheria ya kumwoa yule muke wa mudogo wake.

19 Kwa hiyo Herodia akamuwekea Yoane chuki na kutaka kumwua, lakini hakuweza kwa sababu ya Herode.

20 Herode alimwogopa Yoane, kwa sababu alijua kwamba Yoane ni mwenye haki na mutakatifu. Kwa hivi alimulinda. Alipenda kumusikiliza, ijapokuwa alifazaika sana kila mara alipomusikia.

21 Siku moja Herodia alipata wakati wa kumwua Yoane. Ilikuwa sikukuu ya kuzaliwa kwa Herode, wakati alipofanya karamu kwa wasimamizi wa serikali yake, wakubwa wa waaskari na waheshimiwa wa Galilaya.

22 Binti ya Herodia aliingia na kucheza hata Herode na waalikwa wake wakapendezwa. Halafu mufalme akamwambia yule binti: “Uniombe kitu chochote unachotaka, nami nitakupa.”

23 Kisha akamwapia, akisema: “Nitakupa chochote utakachoniomba, hata ikiwa nusu ya ufalme wangu.”

24 Basi yule binti akatoka na kwenda kumwuliza mama yake: “Niombe nini?” Mama yake akamujibu: “Omba kichwa cha Yoane Mubatizaji.”

25 Mara moja yule binti akarudi upesi kwa mufalme na kumwomba: “Ninataka unipe sasa hivi kichwa cha Yoane Mubatizaji katika sahani.”

26 Mufalme akahuzunika sana, lakini hakumukatalia kwa sababu ya viapo alivyovitoa na kwa sababu ya waalikwa wake.

27 Mara moja mufalme akamutuma mumoja wa waaskari wake walinzi na kumwamuru aende kuleta kichwa cha Yoane Mubatizaji. Yule askari akaenda ndani ya kifungo na kumukata Yoane kichwa.

28 Kisha akakileta katika sahani, akamupa yule binti, naye akakipatia mama yake.

29 Wakati wanafunzi wa Yoane walipopata habari ile, wakaenda kubeba maiti yake na kuizika.


Yesu anakulisha watu elfu tano
( Mat 14.13-21 ; Lk 9.10-17 ; Yn 6.1-14 )

30 Mitume wakarudi kwa Yesu, na kumwelezea mambo yote waliyofanya na yote waliyofundisha.

31 Watu waliomufikia Yesu na kuondoka walikuwa wengi sana hata yeye na wanafunzi wake hawakupata wakati wa kula. Kwa sababu hii aliwaambia wanafunzi: “Twende peke yetu kwa pahali penye ukiwa kusudi mupumzike kidogo.”

32 Basi wakaenda peke yao ndani ya chombo kwa pahali penye ukiwa.

33 Lakini watu wengi waliwaona wakiondoka, wakawatambua. Kwa hiyo wakaenda kule mbio kwa miguu toka miji yote, wakawatangulia kule walipokuwa wakienda.

34 Wakati Yesu alipotoka ndani ya chombo, akaona kundi kubwa la watu, akawasikilia huruma, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasiokuwa na muchungaji. Basi akaanza kuwafundisha maneno mengi.

35 Ilipofika saa za magaribi, wanafunzi wa Yesu wakamufikia na kumwambia: “Hapa ni pori na sasa ni magaribi.

36 Uwaage watu hawa kusudi waende kwenye nyumba kule katika mbuga na katika vijiji vya hapa karibu wapate kujinunulia chakula.”

37 Yesu akawajibu: “Ninyi wenyewe muwape chakula.” Lakini wakamwuliza: “Unataka tuende kununua mikate kwa bei ya vikoroti mia mbili vya feza?”

38 Naye Yesu akawauliza: “Muko na mikate ngapi? Muende kwanza kuangalia.” Walipokwisha kujua, wakamwambia: “Tuko na mikate mitano na samaki mbili.”

39 Basi Yesu akawaamuru wanafunzi wake wawaambie watu wote waikae chini kwenye majani kwa makundi mbalimbali.

40 Wakaikaa kwa makundi ya watu mia moja mia moja, na makumi tano tano.

41 Kisha Yesu akatwaa ile mikate mitano na samaki mbili, akainua macho mbinguni, akamushukuru Mungu. Akamega ile mikate, akawapa wanafunzi wake pamoja na zile samaki mbili kusudi waigawanyie watu wote.

42 Wote wakakula na kushiba.

43 Kisha wanafunzi wakaokota vipande vya mikate na vya samaki vilivyobaki, wakajaza vitunga kumi na viwili.

44 Hesabu ya wanaume tu waliokula ilikuwa elfu tano.


Yesu anatembea juu ya maji
( Mat 14.22-33 ; Yn 6.15-21 )

45 Pale pale Yesu akawalazimisha wanafunzi wake waingie ndani ya chombo na kumutangulia ngambo ingine ya ziwa la Galilaya kuelekea muji Betesaida. Kwa wakati ule alibaki akiaga lile kundi la watu.

46 Kisha kuwaaga, akaenda kwenye kilima kwa kuomba.

47 Giza lilipoingia, chombo kilikuwa katikati ya ziwa, na Yesu alikuwa peke yake inchi kavu.

48 Aliwaona wanafunzi wake wakitaabika kwa kuendesha chombo sababu upepo ulikuwa ukiwarudisha nyuma. Basi ilipokuwa karibu na mapambazuko, Yesu akawafikia akitembea juu ya maji, akitaka kuwapita.

49 Nao walipomwona akitembea juu ya maji, wakawaza kwamba ni muzimu, wakaanza kulalamika,

50 kwa maana wote walimwona na kuogopa sana. Lakini mara moja Yesu akasema nao na kuwaambia: “Mujipe moyo, ni mimi! Musiogope!”

51 Kisha akaingia ndani ya chombo walimokuwa, na upepo ukakoma. Kwa hiyo wanafunzi wakashangaa sana,

52 kwa maana hawakuelewa maana ya ule muujiza wa kuzidisha mikate; kwa kuwa mioyo yao ilikuwa migumu.


Yesu anaponyesha wagonjwa katika inchi ya Genezareti
( Mat 14.34-36 )

53 Walipovuka ziwa, wakafika katika inchi ya Genezareti, wakaezeka chombo kwenye kivuko.

54 Walipotoka ndani ya chombo, mara moja watu wakamutambua Yesu.

55 Basi wakaenda mbio wakipita katika inchi ile yote, wakaanza kumuletea wagonjwa wakibebwa juu ya vipoyi, wakamufikia Yesu popote waliposikia yuko.

56 Na kila pahali Yesu alipokwenda, katika vijiji, miji, au kwenye mbuga, watu waliweka wagonjwa katika viwanja vya makutano na kumusihi awaache wagonjwa waguse hata upindo wa kanzu yake tu. Nao wote waliougusa, walipona.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan