Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Marko 12 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mufano wa walimaji wabaya
( Mat 21.33-46 ; Lk 20.9-19 )

1 Kisha Yesu akaanza kusema maneno haya kwa wale wakubwa kwa njia ya mifano: “Mutu mumoja alipanda shamba la mizabibu, akalizungusha na upango, akatengeneza nafasi ya kukamulia matunda ya mizabibu na kujenga munara kwa ajili ya walinzi wa shamba. Kisha akalipangisha kwa walimaji, akaenda safari katika inchi ingine.

2 Siku za mavuno zilipotimia, akamutuma mutumishi wake mumoja kwa wale walimaji kusudi wamupatie sehemu yake ya mavuno.

3 Lakini wale walimaji wakamukamata yule mutumishi, wakamupiga na kumurudisha mikono mitupu.

4 Mwenye shamba akatuma tena kwao mutumishi mwingine. Yule naye, wakamwumiza kwenye kichwa na kumutukana.

5 Mwenye shamba akatuma tena kwao mutumishi mwingine, nao wakamwua. Na kisha akatuma wengine wengi, nao wale walimaji wakawapiga wamoja na kuwaua wengine.

6 Mwenye shamba alibaki tu na mutu mumoja, naye alikuwa mwana wake mupendwa. Mwisho akamutuma kwao, akisema: ‘Ninajua kwamba watamuheshimu mwana wangu.’

7 Lakini wale walimaji walipomwona akikuja, wakasemezana: ‘Musimame! Huyu ndiye atakayerizi shamba hili. Basi tumwue, na shamba hili litakuwa urizi wetu!’

8 Basi wakamukamata yule mwana, wakamwua na kutupa maiti yake inje ya shamba.”

9 Kisha Yesu akauliza: “Basi yule mwenye shamba la mizabibu atafanya nini? Yeye atakuja na kuwaua wale walimaji. Na kisha atawapatia walimaji wengine shamba lile.

10 Hamujasoma bado Maandiko Matakatifu yanayosema: ‘Jiwe lililokataliwa na wajengaji limekuwa sasa jiwe kubwa la musingi.

11 Ni Bwana aliyefanya jambo hili, nalo ni ajabu sana kwetu.’ ”

12 Basi hao wakubwa wakatafuta kumukamata Yesu, kwa sababu walitambua kwamba alisema mufano huo juu yao. Lakini kwa sababu waliogopa kundi la watu, wakamwacha ajiendee.


Ulizo juu ya kulipa kodi
( Mat 22.15-22 ; Lk 20.20-26 )

13 Wafarisayo wamoja na watu wamoja waliojiunga na Herode walitumwa kwa Yesu kusudi wamunase katika masemi.

14 Walipomufikia, wakamwuliza: “Mwalimu, tunajua kwamba wewe ni mutu wa kweli. Vilevile haushuguliki na mafikiri ya mutu lakini unafundisha kwa ukweli njia Mungu anayoamuru kufuata. Utuambie basi, Sheria inaturuhusu kulipa kodi kwa Mufalme wa Roma au hapana? Ni sherti tulipe au hapana?”

15 Lakini kwa kuwa Yesu alitambua kwamba wao ni wanafiki, akawaambia: “Sababu gani munanipima? Muniletee kikoroti kimoja cha feza hapa kusudi nikione.”

16 Wakakileta kwake. Yesu akawauliza: “Sura hii na jina hili linaloandikwa hapa ni vya nani?” Wakamujibu: “Ni vya Mufalme wa Roma.”

17 Halafu Yesu akawaambia: “Mumupe Mufalme wa Roma vinavyokuwa vyake, na Mungu vinavyokuwa vyake.” Nao wakashangaa sana juu ya jibu lake.


Ulizo juu ya ufufuko
( Mat 22.23-33 ; Lk 20.27-40 )

18 Wasadukayo wamoja, ndio wale watu wanaosema kwamba wafu hawatafufuka, wakamufikia Yesu na kumwuliza:

19 “Mwalimu, Musa alituamuru: ‘Mutu akiwa na ndugu yake, naye akikufa na kuacha muke wake bila mutoto, yule ndugu yake anapaswa kumwoa yule mujane na kumuzalia ndugu yake marehemu watoto.’

20 Basi kulikuwa wandugu saba. Wa kwanza alioa mwanamuke, lakini mutu yule akakufa bila kuacha mutoto.

21 Ndugu wa pili akamwoa yule mwanamuke, naye akakufa vilevile bila kuacha mutoto. Na ikakuwa vile kwa ndugu wa tatu

22 na hata kwa wote saba. Wote walimwoa yule mwanamuke, kila mumoja kisha kufa kwa mwenzake, lakini wakakufa bila kuacha watoto. Na kwa mwisho yule mwanamuke akakufa vilevile.

23 Sasa, siku wafu watakapofufuka, muke yule atakuwa wa nani; kwa maana wote saba walikuwa wamemwoa?”

24 Yesu akawajibu: “Mumedanganyika kwa sababu ya kutojua Maandiko Matakatifu wala uwezo wa Mungu.

25 Kwa maana wafu watakapofufuka, wataishi kama vile wamalaika wanavyoishi katika mbingu; hawataoa wala kuolewa.

26 Na juu ya kufufuka kwa wafu, hamujasoma katika kitabu cha Sheria ya Musa, yale maandiko yanayosema juu ya kichaka kilichowaka moto? Mungu alimwambia Musa: ‘Mimi ni Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo.’ ”

27 Na Yesu akaendelea kuwaambia: “Mungu si Mungu wa waliokufa, lakini ni Mungu wa wanaokuwa wazima. Hivi ninyi munadanganyika kabisa.”


Amri kubwa
( Mat 22.34-40 ; Lk 10.25-28 )

28 Mwalimu mumoja wa Sheria alikuwa pale Yesu alipobishana na Wasadukayo. Yeye alitambua kwamba Yesu aliwajibu vizuri. Basi akamujongelea na kumwuliza: “Ni amri gani inayokuwa ya kwanza katikati ya amri zote?”

29 Yesu akamujibu: “Amri ya kwanza katikati ya zote ni hii: ‘Sikia, wewe taifa la Waisraeli! Bwana Mungu wetu ndiye Bwana peke yake.

30 Umupende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa roho yako yote, kwa akili yako yote na kwa nguvu yako yote.’

31 Na amri ya pili ni hii: ‘Umupende mwenzako kama vile unavyojipenda mwenyewe.’ Hakuna amri zingine kubwa kupita hizi.”

32 Yule mwalimu wa Sheria akamwambia Yesu: “Ni vizuri, Ee Mwalimu! Umesema kweli kwamba Mungu ni mumoja peke yake wala hakuna mungu mwingine isipokuwa yeye.

33 Na mutu anapaswa kumupenda Mungu kwa moyo wake wote, kwa akili yake yote na kwa nguvu yake yote, naye anapaswa kumupenda mwenzake kama vile anavyojipenda mwenyewe. Mambo hayo ni bora zaidi kuliko kumutolea Mungu nyama za kuteketezwa kwa moto na sadaka zingine zote.”

34 Yesu alipoona kwamba amejibu kwa akili, akamwambia: “Si mbali kwako kuingia katika Ufalme wa Mungu.” Kisha maneno hayo hakuna mutu aliyesubutu tena kumwuliza Yesu neno.


Ukoo na ukubwa wa Kristo
( Mat 22.41-46 ; Lk 20.41-44 )

35 Yesu alipokuwa akifundisha katika hekalu akauliza: “Namna gani walimu wa Sheria wanaweza kusema kwamba Kristo ni Mwana wa Daudi?

36 Daudi yeye mwenyewe, akiongozwa na Roho Mutakatifu, alisema: ‘Bwana wetu Mungu alimwambia Bwana wangu: Ikaa na mamlaka kwa kuume kwangu, mpaka nitakapoweka waadui zako chini ya miguu yako.’

37 Daudi mwenyewe anamwita Kristo ‘Bwana’; namna gani basi Kristo anaweza kuwa Mwana wake?” Kundi kubwa la watu walimusikiliza Yesu kwa furaha.


Maonyo juu ya walimu wa Sheria
( Mat 23.1-36 ; Lk 20.45-47 )

38 Katika mafundisho yake aliwaambia: “Mujiepushe na walimu wa Sheria, wanaopenda kujitembeza wakivaa kanzu ndefu, na kusalimiwa kwa heshima kwenye nafasi ya makutano.

39 Wanapenda vilevile kuikaa katika viti vya mbele ndani ya nyumba za kuabudia na kwenye nafasi za heshima katika karamu.

40 Wananyanganya mali ya wajane na kuomba maombi marefu kusudi waonekane mbele ya watu. Kwa sababu hii watahukumiwa vikali sana!”


Sadaka ya mujane masikini
( Lk 21.1-4 )

41 Yesu akaikaa akielekea kwenye sanduku ya kutilia sadaka za hekalu. Akaangalia jinsi watu walivyotia feza ndani ya sanduku ile. Watajiri wengi walitia feza nyingi ndani yake.

42 Na kukakuja mujane mumoja masikini, akatoa vikoroti viwili vidogo sana vinavyolingana na sengi mbili.

43 Basi Yesu akawaita wanafunzi wake na kuwaambia: “Kweli ninawaambia kwamba mujane huyu masikini ametoa mingi zaidi kuliko wote wanaotia feza ndani ya sanduku ya sadaka.

44 Kwa maana wengine wote walitoa sehemu ya mali wasiyokuwa nayo lazima. Lakini yeye ametoa kwa umasikini wake, mali yote aliyokuwa nayo kwa kuishi.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan