Marko 10 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mafundisho ya Yesu juu ya kuvunja ndoa ( Mat 19.1-12 ; Lk 16.18 ) 1 Yesu akaondoka kule, akaenda katika jimbo la Yudea na kuvuka ngambo ingine ya Yordani. Na makundi mengi ya watu wakakusanyika tena mbele yake, naye akaanza kuwafundisha, kama vile alivyozoea kufanya. 2 Wafarisayo wamoja wakamufikia kwa kumupima, wakamwuliza: “Sheria yetu inamuruhusu mutu kufukuza muke wake?” 3 Yesu akajibu: “Musa aliwaamuru nini?” 4 Nao wakamujibu: “Musa alitoa ruhusa kwa mutu kuandika barua ya kuachana na muke wake na kisha amufukuze.” 5 Yesu akawaambia: “Musa aliwaandikia amri ile kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu. 6 Lakini wakati Mungu alipowaumba watu wa kwanza, aliwaumba mwanaume na mwanamuke. 7 Kwa sababu hii, mutu atawaacha baba yake na mama yake na kuungana na muke wake, 8 nao wawili watakuwa mwili mumoja. Hivi wao si wawili tena, lakini wanakuwa mumoja. 9 Basi mutu asitenganishe kile Mungu alichokiunganisha.” 10 Walipokuwa ndani ya nyumba, wanafunzi wakamwuliza Yesu tena juu ya neno lile. 11 Yesu akawaambia: “Kila mutu anayemufukuza muke wake na kuoa mwingine, anazini na kumukosea yule muke wa kwanza. 12 Vile vile, kila muke anayemwacha mume wake na kuolewa na mwingine, anazini.” Yesu anabariki watoto wadogo ( Mat 19.13-15 ; Lk 18.15-17 ) 13 Watu wamoja wakamuletea Yesu watoto kusudi awawekee mikono, lakini wanafunzi wake wakawakaripia watu wale. 14 Yesu alipoona vile, akakasirika na kuwaambia wanafunzi wake: “Muwaache watoto wadogo wakuje kwangu wala musiwakataze, kwa maana Ufalme wa Mungu ni wa watu wanaokuwa sawasawa na wao. 15 Kweli ninawaambia ninyi: mutu yeyote asiyepokea Ufalme wa Mungu kama mutoto mudogo, hawezi kuingia ndani yake hata kidogo.” 16 Kisha akawakumbatia watoto wale, akaweka mikono juu yao na kuwabariki. Kijana mumoja tajiri ( Mat 19.16-30 ; Lk 18.18-30 ) 17 Yesu alipoondoka kwa kuendelea na safari yake, mutu mumoja akamufikia mbio akapiga magoti mbele yake na kumwuliza: “Mwalimu mwema, nifanye nini kusudi nipate kurizi uzima wa milele?” 18 Yesu akamwuliza: “Sababu gani unaniita mwema? Hakuna mutu anayekuwa mwema, isipokuwa Mungu peke yake. 19 Unajua jinsi amri zinavyosema kwamba: ‘Usiue, usizini, usiibe, usishuhudie uongo, usidanganye, uwaheshimu baba yako na mama yako.’ ” 20 Yule mutu akamujibu: “Mwalimu, nimetii amri zile zote tangu ujana wangu.” 21 Yesu akamwangalia kwa upendo, akamwambia: “Unakosewa na kitu kimoja tu: kwenda uuzishe vitu vyote unavyokuwa navyo, na uwape wamasikini mali zile, nawe utakuwa na akiba mbinguni. Kisha urudi, unifuate!” 22 Lakini kijana yule aliposikia maneno yale, alikunja uso, na kujiendea katika huzuni, kwa sababu alikuwa tajiri sana. 23 Yesu akaangalia pande zake zote na kuwaambia wanafunzi wake: “Kweli ni vigumu sana kwa watajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu!” 24 Wanafunzi wakashangaa sana kusikia maneno hayo. Lakini Yesu akawaambia tena: “Watoto wangu, ni vigumu kabisa kuingia katika Ufalme wa Mungu! 25 Ni kwepesi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.” 26 Wanafunzi waliposikia maneno hayo wakazidi kushangaa hata wakaulizana wao kwa wao: “Ni nani basi anayeweza kuokolewa?” 27 Yesu akawaangalia na kuwaambia: “Kwa mwanadamu haiwezekani, lakini kwa Mungu si vile, kwa maana mambo yote yanawezekana kwa Mungu.” 28 Petro akamwambia: “Angalia sisi tumeacha vyote na kukufuata wewe!” 29 Yesu akajibu: “Kweli ninawaambia: kama mutu akiacha nyumba yake, ndugu, dada, mama, baba, watoto wake au mashamba yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Habari Njema, 30 atapokea mara mia zaidi katika wakati wa sasa. Atapokea nyumba, ndugu, dada, mama, watoto na mashamba pamoja na mateso. Na katika wakati utakaokuja atapokea uzima wa milele. 31 Lakini wengi wanaokuwa wa kwanza watakuwa wa mwisho, na wengi wanaokuwa wa mwisho watakuwa wa kwanza.” Yesu anajulisha mara ya tatu habari za kufa na kufufuka kwake ( Mat 20.17-19 ; Lk 18.31-34 ) 32 Yesu na wanafunzi wake walipokuwa katika njia, wakipanda kwenda Yerusalema, yeye akatangulia mbele yao. Wanafunzi walishikwa na hofu, nao watu waliowafuata waliogopa. Yesu akawatwaa tena wanafunzi wake kumi na wawili, na kuanza kusemezana nao juu ya mambo yatakayomupata. 33 Akawaambia: “Tunapanda kwenda Yerusalema na kule Mwana wa Mutu atatolewa kwa wakubwa wa makuhani na kwa walimu wa Sheria. Nao watamuhukumu auawe na kumutoa katika mikono ya watu wa mataifa mengine. 34 Nao watamuchekelea, watamutemea mate, watamupiga fimbo na kumwua. Lakini kwa siku ya tatu kisha kufa kwake, atafufuka.” Yakobo na Yoane wanaomba ukubwa ( Mat 20.20-28 ) 35 Kisha wana wawili wa Zebedayo, Yakobo na Yoane, wakamufikia Yesu na kumwambia: “Mwalimu, tunataka utufanyie jambo tutakalokuomba.” 36 Yesu akawauliza: “Munataka niwafanyie nini?” 37 Nao wakamujibu: “Utakapokuwa katika utukufu wako, uturuhusu kuikaa pamoja nawe, mumoja kwa upande wako wa kuume na mwingine kwa upande wako wa kushoto.” 38 Lakini Yesu akawaambia: “Hamujui kitu munachoomba. Munaweza kunywa kikombe cha mateso nitakachokunywa? Au munaweza kubatizwa kwa namna ya ubatizo nitakaoupata?” 39 Nao wakamujibu: “Tunaweza.” Yesu akaongeza kuwaambia: “Hakika mutakunywa kikombe nitakachokunywa, na kubatizwa kama vile nitakavyobatizwa. 40 Lakini kuikalisha mutu kwa upande wangu wa kuume au wa kushoto si kazi yangu. Ni Mungu peke yake atakayeweka watu aliowatayarisha kwenye nafasi zile.” 41 Wanafunzi wengine kumi waliposikia maneno yale, wakachukizwa na Yakobo na Yoane. 42 Yesu akawaita wote na kuwaambia: “Munajua kwamba wale wanaohesabiwa kuwa watawala wa mataifa wanayatawala kwa kinguvu, na wakubwa yao wanayagandamiza. 43 Lakini isikuwe hivi katikati yenu. Anayetaka kuwa mukubwa kati yenu, sherti akuwe mutumishi wenu. 44 Naye anayetaka kuwa wa kwanza, sherti akuwe mutumwa wa wote. 45 Kwa maana hata Mwana wa Mutu hakuja kutumikiwa, lakini kutumika na kutoa maisha yake kusudi awakomboe watu wengi.” Yesu ananyesha kipofu Bartimayo ( Mat 20.29-34 ; Lk 18.35-43 ) 46 Wakafika Yeriko. Na wakati Yesu alipokuwa akitoka kule pamoja na wanafunzi wake na kundi kubwa la watu, mutu mumoja kipofu aliyeitwa Bartimayo mwana wa Timayo, alikuwa akiikaa pembeni ya njia akiombaomba. 47 Naye aliposikia kwamba Yesu wa Nazareti anapita katika njia ile, akalalamika, akisema: “Yesu Mwana wa Daudi, unisikilie huruma!” 48 Watu wengi walimukaripia na kumwambia anyamaze, lakini alizidi kulalamika akisema: “Yesu Mwana wa Daudi, unisikilie huruma!” 49 Yesu akasimama na kusema: “Mumwite.” Basi wakamwita yule kipofu na kumwambia: “Ujipe moyo! Simama, anakuita.” 50 Bartimayo akatupa koti yake, akaruka upesi na kumwendea Yesu. 51 Yesu akamwuliza: “Unataka nikufanyie nini?” Yule kipofu akamujibu: “Mwalimu, ninataka nipate kuona.” 52 Yesu akamwambia: “Ujiendee, imani yako imekuponyesha.” Na pale pale akapata kuona, na kumufuata Yesu katika njia. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo