Maombolezo 5 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kuomba huruma 1 Ukumbuke, ee Yawe, mambo yaliyotupata! Utuangalie, uone haya yetu! 2 Inchi yetu imepewa kwa wageni, nyumba zetu kwa watu wengine. 3 Tumekuwa wayatima, bila baba, wamama zetu ni kama wajane. 4 Maji yetu tunayapata kwa feza, kuni zetu kwa kuzinunua. 5 Tunalazimishwa kufanya kazi kama punda, tumechoka, lakini haturuhusiwi kupumzika. 6 Tumewanyooshea Wamisri na Waasuria mikono, kusudi tupate chakula cha kutosha. 7 Babu zetu walitenda zambi na sasa hawako tena; nasi tunabeba makosa yao. 8 Watumwa wanatutawala, wala hakuna wa kutuokoa toka katika mikono yao. 9 Chakula chetu tunakipata kwa kuhatarisha maisha yetu, maana wauaji wanazungukazunguka katika jangwa. 10 Ngozi zetu zinawaka moto kama furu, kwa sababu ya njaa inayotuchoma. 11 Wanawake wetu wanatendewa kwa kinguvu katika Sayuni, na wabinti wetu katika miji ya Yuda. 12 Wakubwa wetu wametundikwa kwa mikono yao; wazee wetu hawapewi heshima yoyote. 13 Vijana wanalazimishwa kusaga ngano kwa mawe, watoto wanayumbayumba kwa mizigo ya kuni. 14 Wazee wameacha kutoa mashauri yao, vijana wameacha kuimba. 15 Furaha ya mioyo yetu imetoweka, michezo yetu imegeuzwa kuwa maombolezo. 16 Taji tuliojivunia imeanguka. Ole kwetu maana tumetenda zambi! 17 Kwa ajili ya hiyo tumeugua ndani ya moyo, kwa ajili ya hiyo macho yetu yamefifia. 18 Maana mulima Sayuni umeachwa utupu, mbweha wanazungukazunguka humo. 19 Lakini wewe Yawe unatawala milele, kiti chako cha kifalme kinadumu kwa vizazi vyote. 20 Sababu gani umetusahau kwa muda murefu hivyo na kutuacha siku nyingi hivyo? 21 Utugeuze, ee Yawe, kusudi tukurudilie. Uturudishie hali ya zamani. 22 Au, umetukataa kabisa? Umetukasirikia sana? |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo