Maombolezo 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yerusalema kisha kuangamizwa 1 Namna gani zahabu yetu ilivyochakaa, zahabu safi kabisa ilivyobadilika! Mawe ya bei kali yamesambazwa kwa barabara zote. 2 Watoto wa Sayuni waliosifiwa sana, waliokuwa na bei kama zahabu safi, namna gani sasa wamekuwa kama vyombo vya udongo, kazi ya mikono ya mufinyanzi! 3 Hata mbweha wanatoa maziwa, na kuwanyonyesha watoto wao; lakini watu wangu wamekuwa wabaya, wanafanya kama mbuni katika jangwa. 4 Midomo ya watoto wachanga imekauka kwa kiu, watoto wanaomba chakula, lakini hakuna anayewapa. 5 Wale waliokula vyakula vinono wanakufa na njaa katika barabara. Waliolelewa na kuvalishwa namna ya kifalme wanafukua kwa mikono kwenye yalala. 6 Kosa la watu wangu lilikuwa kubwa kuliko zambi za watu wa Sodoma, muji ambao uliteketezwa kwa rafla bila kuwa na muda wa kunyoosha mukono. 7 Vijana wa Sayuni walikuwa safi kuliko teluji, walikuwa weupe kuliko maziwa. Miili yao ilikuwa myekundu kuliko mawe ya matumbawe, uso wao kama jiwe la rangi ya samawi. 8 Sasa sura zao ni nyeusi kuliko makaa, wanapita katika barabara bila kujulikana; ngozi yao imebanana na mifupa yao, imekauka, imekuwa kama kuni. 9 Afazali waliouawa kwa upanga kuliko waliokufa kwa njaa, ambao walikufa polepole kwa kukosa mazao ya shamba. 10 Wamama ambao wanakuwa na huruma kubwa, waliwapika watoto wao wenyewe, wakawafanya kuwa chakula chao, wakati watu wangu walipoangamizwa. 11 Yawe ameonyesha kabisa kasirani yake, aliimwanga hasira yake kali, aliwasha moto huko katika Sayuni ambao uliteketeza misingi yake. 12 Wafalme katika dunia hawakuamini wala wakaaji wowote wa ulimwengu, kwamba mwangamizaji na adui wangeweza kuingia katika milango ya Yerusalema. 13 Ni kwa sababu ya zambi za manabii wake na makosa ya makuhani wake, ambao walimwanga damu ya watu wa haki katika muji wake. 14 Walitangatanga katika barabara kama vipofu, walikuwa wamejichafua kwa damu, hata mutu yeyote hangeweza kugusa nguo zao. 15 Watu waliwapigia kelele wakisema: Mutoke, enyi munaokuwa wachafu! Mutoke! Mutoke! Musiguse kitu chochote. Hivyo wakakuwa wakimbizi na kutangatanga; watu wa mataifa walisema: Hawa hawatakaribishwa kukaa kwetu! 16 Yawe mwenyewe aliwatawanya, wala hatawajali tena. Makuhani hawaheshimiwi tena, wazee hawapendelewi tena. 17 Tulichoka kukaa macho kungojea musaada; tulikesha na kungojea kwa hamu taifa ambalo halikuweza kutuokoa. 18 Watu walifuatilia hatua zetu, tukashindwa kupita katika barabara zetu. Mwisho wetu ulikaribia, siku zetu zilitimia, mwisho wetu ulifika. 19 Waliotufuatilia walikuwa wepesi kuliko tai, walitukimbiza kwenye milima walituvizia katika jangwa. 20 Walimunasa yule ambaye maisha yetu yalimutegemea, yule mufalme aliyechaguliwa na Yawe yule ambaye tulisema juu yake: Chini ya ulinzi wake tutaishi kati ya mataifa. 21 Wakaaji wa Edomu, ile inchi ya Uzi, mushangilie na kufurahi kwa sasa. Lakini kikombe hiki cha azabu kitawafikia vilevile. Mutakikunywa na kulewa, hata mutavaa uchi! 22 Azabu ya uovu wako, ewe Sayuni imekamilika; Yawe hatawaacha zaidi katika uhamisho. Lakini ninyi Waedomu atawaazibu kwa uovu wenu, atazifichua zambi zenu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo