Maombolezo 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Azabu, kugeuka na tumaini 1 Mimi ni mutu niliyepata mateso kwa fimbo ya kasirani ya Mungu. 2 Amenikamata na kunitembeza katika giza ambako hakuna mwangaza. 3 Amenyoosha mukono wake juu yangu mimi tu, akiniazibu tena na tena muchana kutwa. 4 Amenichakalisha ngozi na nyama, ameivunja mifupa yangu. 5 Amenikusanyia na kunizungushia uchungu na mateso. 6 Amenikalisha katika giza kama watu waliokufa zamani. 7 Amenizungushiia ukuta na siwezi kutoka, amenifunga kwa minyororo mizito. 8 Ingawa ninaita na kuomba musaada anazuiza maombi yangu yasimufikie. 9 Amezifunga njia zangu kwa mawe makubwa, amepotosha mapito yangu. 10 Alikuwa kwangu kama dubu anayevizia, kama simba katika maficho. 11 Alinifukuza katika njia yangu, akanirarua na kuniacha ukiwa. 12 Aliuvuta upinde wake, akanielekezea mushale wake. 13 Alinichoma ndani ya moyo kwa mishale, kutoka katika kifuko chake. 14 Nimekuwa kitu cha kuchekelewa kwa watu wote, muchana kutwa nimekuwa mutu wa kuzomewa. 15 Amenijaza taabu, akanishibisha uchungu. 16 Amenisagisha meno katika mawe, akanifanya nigaegae katika majivu. 17 Moyo wangu haujui tena amani, nimesahau furaha. 18 Nimewaza: Nimekata tamaa kabisa, tumaini langu kwa Yawe limetoweka. 19 Kukumbuka taabu na kutangatanga kwangu kunanipa uchungu na sumu. 20 Ninafikiri juu ya hayo siku zote, nayo roho yangu imejaa huzuni. 21 Lakini ninakumbuka jambo hili moja, nami ninakuwa na tumaini: 22 Wema wa Yawe haukomi, huruma zake hazina mwisho. 23 Uaminifu wake ni mukubwa sana, kila mara kunapokucha ni mupya kabisa. 24 Yawe ndiye sehemu yangu, hivyo nitamuwekea tumaini langu. 25 Yawe ni muzuri kwa wanaomutegemea, kwa wote wanaomutafuta. 26 Ni vizuri kwa mutu kungojea kwa utulivu wokovu unaotoka kwa Yawe. 27 Ni vizuri kwa mutu kujifunza uvumilivu tangu wakati wa ujana wake. 28 Heri kwa mutu kukaa peke yake na kimya, mambo mazito yanapomupata kutoka kwa Mungu. 29 Inamupasa kuinama na kujinyenyekeza, labda tumaini litakuwa likingali. 30 Inamupasa kumugeuzia shavu mwenye kumupiga, na kuwa tayari kupokea matusi yake. 31 Yawe hatatutupilia milele. 32 Ingawa atatufanya tuhuzunike, atakuwa na huruma tena, kadiri ya wingi wa wema wake. 33 Yeye hapendelei kuwatesa wala kuwahuzunisha wanadamu. 34 Wafungwa wote katika inchi wanapoteswa na kupondwa, 35 haki za wanadamu zinapopotoshwa mbele ya Mungu Mukubwa, 36 wanapomunyima mutu haki katika tribinali, basi, Yawe haoni hayo? 37 Nani anayeweza kusema kusudi kitu kifanyike ikiwa Yawe asipoamuru ikuwe hivyo? 38 Maovu na mema yanatokea tu kwa amri ya Mungu Mukubwa. 39 Kwa nini mutu anungunike ikiwa ameazibiwa kwa ajili ya zambi zake? 40 Tupime na kuchunguza mwenendo wetu tupate kumurudilia Yawe. 41 Tumufungulie Mungu mioyo yetu na kumwomba kule juu mbinguni: 42 Tulikukosea na kukuasi, nawe haujatusamehe bado. 43 Umejifunika hasira yako na kutufuatilia, ukatuua bila huruma. 44 Umejifunika wingu kusudi maombi yoyote yasipite. 45 Umetufanya kuwa takataka na uchafu kati ya mataifa. 46 Waadui zetu wote wanatuzomea. 47 Woga na hofu vimetuandama tumepatwa na uharibifu na maangamizi. 48 Macho yangu yanabubujika mito ya machozi kwa sababu ya kuangamizwa kwa watu wangu. 49 Macho yangu yanatelemusha machozi bila kukoma, 50 mpaka Yawe kutoka kule mbinguni aangalie chini na kuona. 51 Ninahuzini sana kuona yale yaliyowapata wabinti wa muji wangu. 52 Nimewindwa kama ndege na hao wanaonichukia bila sababu. 53 Walinitupa ndani ya shimo nikiwa muzima na juu yangu wakalundika mawe. 54 Maji yalianza kunifunika kichwa, nami nikafikiri: Huu ni mwisho wangu. 55 Kutoka chini ndani ya shimo, nilikulilia ee Yawe. 56 Wewe umenisikia nikikulilia: Usiache kusikiliza maombi yangu ya musaada. 57 Nilipokuita ulifika karibu nami ukaniambia: Usiogope! 58 Ulinitetea katika maneno yangu, ee Yawe, uliyakomboa maisha yangu. 59 Uliuona uovu niliotendewa, ee Yawe; uniamulie kwa wema maneno yangu. 60 Umeuona uovu wa waadui zangu, na mipango yao yote juu yangu. 61 Umesikia matukano yao, ee Yawe, na mipango yao yote juu yangu. 62 Maneno na mawazo ya waadui zangu siku nzima, ni juu ya kuniangamiza mimi. 63 Wakiikaa au wakienda, ni mimi ndiye wanayemuzomea. 64 Uwalipize, ee Yawe, sawasawa na matendo yao, sawasawa na kazi ya mikono yao. 65 Uifanye mioyo yao kuwa migumu, na laana yako iwashukie. 66 Uwafuatilie kwa hasira na kuwaangamiza toka katika dunia. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo