Maombolezo 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Azabu ya Yerusalema 1 Kwa hasira yake, Yawe amewaweka watu wa Sayuni katika giza. Ametupa toka mbinguni mpaka katika dunia utukufu wa Israeli. Kwa siku ya hasira yake, alilitupilia mbali hata hekalu lake. 2 Yawe ameharibu bila huruma makao yote ya wazao wa Yakobo. Kwa kasirani yake amevibomoa vikingio vya watu wa Yuda. Ametupa chini na kuchafua ufalme wao na watawala wake. 3 Ameivunja kwa hasira nguvu yote ya Israeli. Hakunyoosha mukono kwa kuwasaidia walipokutana na adui; amewawakia watu wa Yakobo kama moto, akateketeza kila kitu. 4 Amevuta upinde wake kama adui, na kuuweka mukono wake wa kuume tayari, amewaua wote waliopendeza macho. Amemwanga hasira yake kama moto katika hema yetu watu wa Sayuni. 5 Yawe amekuwa kama adui, ameangamiza watu wa Israeli; ameharibu nyumba zake kubwa zote, amevibomoa vikingio vyake. Amewazidishia watu wa Yuda kilio na maombolezo. 6 Amelibomoa hekalu lake kama kibanda katika bustani, ameharibu pahali pake pa kusanyiko. Amefanya sikukuu na siku ya Sabato visahauliwe kule Sayuni, kwa hasira yake kubwa amewakataa mufalme na makuhani. 7 Yawe amechukia mazabahu yake na hekalu lake amelikataa. Amewaachilia waadui wazibomoe kuta za nyumba zake katika muji. Wakapiga kelele ndani ya nyumba ya Yawe kama kelele za wakati wa sikukuu. 8 Yawe alikusudia kuubomoa ukuta wa Sayuni; aliupima na kuhakikisha kila kitu kwamba kimeharibika; minara na kuta za inje ya muji akazifanya ukiwa, zote kwa pamoja zikaangamia. 9 Milango yake imezama ndani ya udongo, ameharibu na kuvunjavunja vifungio vyake. Mufalme na wakubwa wake wako katika uhamisho kati ya mataifa. Hakuna sheria tena, manabii wake hawapati tena maono kutoka kwa Yawe. 10 Wazee wa Sayuni wameikaa chini kimya, wamejitia mavumbi juu ya vichwa na kuvaa gunia. Wabinti wa Yerusalema wameinamisha vichwa chini. 11 Macho yangu yamevimba kwa kulia, roho yangu imechafuka, moyo wangu una huzuni nyingi, kwa sababu ya kuangamizwa kwa watu wangu, kwa sababu watoto wachanga na wale wanaonyonya wanazimia katika barabara za muji. 12 Wanawalilia wamama zao: Chakula kiko wapi, kinywaji kiko wapi? Wanazimia kama wale walioumizwa katika barabara za muji, na kukata roho katika mikono ya wamama zao. 13 Nikuambie nini, ee Yerusalema? Nikulinganishe na nini? Nikufananishe na kitu gani kusudi niweze kukufariji, ee Sayuni uliyekuwa muzuri? Maangamizi yako ni mengi kama bahari, ni nani atakayekuponyesha? 14 Manabii wako wamekuonea maono madanganyifu. Hawakufichua wazi uovu wako kusudi wapate kukurudishia hali yako ya mbele. Lakini walikuonea maono ya uongo na ya kupotosha. 15 Wapita njia wote wanakuchekelea; wanakupigia muunzi, ee Yerusalema, wakitikisa vichwa vyao kwa mazarau na kusema: Huu ndio ule muji uliofikia ukamilifu wa uzuri, muji uliokuwa furaha ya dunia nzima? 16 Waadui zako wote wanakuzomea, wanakupigia muunzi na kukusagia meno, nao wanasema: Tumemwangamiza! Kweli, siku ile tuliyoingojea kwa hamu sasa imefika na tumeiona! 17 Yawe amefanya yale aliyokusudia, ametimiza yale aliyoagiza. Kama alivyopanga tangu kale, ameangamiza bila huruma yoyote. Amewafanya waadui wafurahie azabu yako, amewatukuza mashujaa wa waadui zako. 18 Ee Sayuni, umulilie Yawe! Machozi yatiririke kama muto muchana na usiku! Lia na kuomboleza bila kupumzika! 19 Usiku kucha uamukeamuke na kulia. Umufungulie Yawe yanayokuwa ndani ya moyo wako. Umwinulie mikono yako kwa kuwaombea watoto wako, watoto wanazimia na njaa popote katika barabara. 20 Angalia, ee Yawe, uone! Kuna yeyote uliyemutendea kama ulivyotutendea sisi, hata wamama wawakule watoto wao nao makuhani wauawe ndani ya hekalu lako? 21 Maiti za vijana na wazee zimelala ndani ya mavumbi katika barabara, wabinti na vijana wangu wameuawa kwa upanga; umewaua bila huruma siku ya hasira yako. 22 Umewaalika kama kwenye sikukuu waadui zangu walionitisha kila upande. Katika siku ya hasira yako, ee Yawe, hakuna aliyetoroka au kubakia. Wale niliowazaa na kuwalea, waadui zangu wamewaangamiza. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo