Malaki 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Ujumbe wa neno la Yawe lililowafikia Waisraeli kwa njia ya Malaki. Yawe anawapenda Waisraeli 2 Yawe anasema hivi: Nimewapenda ninyi siku zote. Lakini ninyi wazao wa Yakobo munaniuliza: Umetupenda namna gani? Yawe anasema hivi: Si Esau alikuwa ndugu wa Yakobo? Hata hivyo nilimupenda Yakobo 3 na kumuchukia Esau. Nimeiharibu inchi ya milima ya Esau ambayo ni urizi wake, nikawaachia imbwa wa pori wa jangwa. 4 Waedomu, wale wazao wa Esau, wanasema kwamba ingawa miji yao imeharibiwa, watajenga upya mabomoko yake. Lakini, Yawe wa majeshi anasema hivi: Wanaweza kuijenga upya, lakini mimi nitaibomoa tena. Watu watawaita: Taifa ovu ambalo Yawe amelikasirikia milele. 5 Nanyi mutakapoyaona mambo yale kwa macho yenu, mutatambua na kusema: Ukubwa wa Yawe unafika hata inje ya mipaka ya inchi ya Israeli. Yawe anawakaripia makuhani 6 Yawe wa majeshi anasema hivi: Mutoto anamuheshimu muzazi wake, na mutumishi anamuheshimu bwana wake. Ikiwa mimi ndiye Baba wenu, mbona munanivunjia heshima? Ikiwa mimi ni bwana wenu, mbona hamuniheshimu? Ninasema hivyo kwa ninyi makuhani munaozarau jina langu. Nanyi munauliza: Sisi tumezarau jina lako namna gani? 7 Munalizarau kwa kunitolea kwenye mazabahu yangu sadaka ya chakula kichafu. Lakini ninyi munauliza: Tumekichafua namna gani? Munakichafua kwa kuizarau mazabahu yangu. 8 Munaponitolea sadaka ya nyama anayekuwa kipofu, au kilema, au mugonjwa, huo si uovu? Mutawala atapendezwa au kukutendea mema ukimupa zawadi ya nyama kama yule? –Ni Yawe wa majeshi anayesema hivyo. 9 Kwa hiyo sasa enyi makuhani, mumwombe Mungu kusudi atuhurumie. Yawe wa majeshi anasema hivi: Ikiwa munamutolea matoleo ya aina hiyo, kweli atawakubali? 10 Heri kungepatikana mutu mumoja kati yenu ambaye angefunga milango ya hekalu kusudi musiwashe moto usiokubaliwa kwenye mazabahu yangu! Sipendezwi nanyi na sitaikubali sadaka yoyote munayonitolea. 11 Watu wa mataifa katika dunia yote tokea upande jua linapopanda mpaka upande jua linaposhuka wanalitukuza jina langu. Kila pahali wananifukizia ubani na kunitolea sadaka zinazokubaliwa; maana jina langu linatukuzwa kati yao. 12 Lakini ninyi munalizarau jina langu pale munapoichafua mazabahu yangu, na chakula munachotoa juu yake munakizarau. 13 Munasema: Mambo haya yametuchokesha sana na munanizarau. Munaniletea sadaka za nyama muliopata kwa njia ya kunyanganya, au wanaokua vilema au wagonjwa. Basi, nipokee sadaka hizo toka katika mikono yenu? 14 Alaaniwe mutu yeyote anayenidanganya, ambaye anaahidi kwa kiapo kunitolea sadaka ya nyama safi kutoka kundi lake, lakini ananitolea sadaka ya nyama mwenye kilema. Mimi ni mufalme mukubwa, na watu wa mataifa yote wananiogopa. –Ni Yawe wa majeshi anayesema hivyo. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo