Luka 9 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yesu anawatuma wale kumi na wawili ( Mat 10.5-15 ; Mk 6.7-13 ) 1 Yesu akawakusanya wanafunzi wake kumi na wawili na kuwapatia uwezo na mamlaka ya kufukuza pepo, na uwezo wa kuponyesha wagonjwa. 2 Halafu akawatuma kuhubiri habari za Ufalme wa Mungu na kuwaponyesha wagonjwa, 3 akiwaagiza: “Musibebe kitu chochote kwa safari yenu, hata ikiwa fimbo, mufuko, mukate wala feza na hata mumoja wenu asivae kanzu mbili. 4 Na nafasi yoyote watakapowakaribisha ndani ya nyumba mubakie mule mpaka mutakapotoka kule. 5 Na katika muji wowote watu watakapokataa kuwakaribisha, mutoke kule na mukungute mavumbi toka juu ya miguu yenu. Jambo hili litakuwa ushuhuda juu yao.” 6 Basi wanafunzi wakaondoka, wakapita katika vijiji mbalimbali, wakihubiri Habari Njema na kuponyesha watu kila fasi. Herode anafazaika juu ya habari za Yesu ( Mat 14.1-12 ; Mk 6.14-29 ) 7 Liwali Herode akasikia habari za mambo yote yaliyofanyika. Kwa hiyo akafazaika kwa sababu watu wamoja walikuwa wakisema kwamba Yoane Mubatizaji amefufuka. 8 Na wengine walikuwa wakisema kwamba Elia ametokea. Na wengine walisema kwamba mumoja wa manabii wa zamani amefufuka. 9 Lakini Herode alisema: “Mimi nimeamuru Yoane akatwe kichwa. Basi huyu ninayesikia habari zake ni nani?” Naye akatafuta namna ya kumwona Yesu. Yesu analisha watu elfu tano ( Mat 14.13-21 ; Mk 6.30-44 ; Yn 6.1-14 ) 10 Mitume waliporudia toka kuhubiri wakamwelezea Yesu mambo yote waliyofanya. Kisha akaondoka pamoja nao na kwenda kwenye nafasi ya upekee karibu na muji Betesaida. 11 Lakini makundi ya watu walipopata habari ile, wakamufuata mpaka kule. Yesu akawapokea na kuanza kusema nao juu ya Ufalme wa Mungu, na vilevile akawaponyesha wale waliohitaji kuponyeshwa. 12 Jua lilipoanza kushuka, wanafunzi kumi na wawili wa Yesu wakamufikia na kumwambia: “Hapa tunapokuwa ni katika pori. Uage makundi haya ya watu kusudi waende katika vijiji vinavyokuwa hapa karibu na kwenye nyumba kule katika mbuga kwa kujitafutia chakula na nafasi ya kulala.” 13 Lakini Yesu akawajibu: “Ninyi wenyewe muwape chakula!” Nao wakajibu: “Sisi tuko tu na mikate mitano na samaki mbili. Unataka sisi wenyewe tuende kuwanunulia watu hawa wote chakula?” 14 (Watu waliokuwa pale walikuwa yapata wanaume elfu tano.) Yesu akawaamuru wanafunzi wake wawaikalishe kwa makundi ya watu makumi tano tano. 15 Nao wanafunzi wakafanya vile, wakawaikalisha watu wote. 16 Kisha Yesu akatwaa ile mikate mitano na samaki mbili, akainua macho mbinguni, akamushukuru Mungu. Halafu akaimega, akawapa wanafunzi waigawanyie watu. 17 Wote wakakula na kushiba. Nao wanafunzi wakaokota vipande vilivyobaki, wakajaza vitunga kumi na viwili. Petro anajulisha kwamba Yesu ni Kristo ( Mat 16.13-19 ; Mk 8.27-29 ) 18 Siku moja Yesu alipokuwa akiomba kwenye nafasi ya upekee, nao wanafunzi wake wakiwa pale karibu naye, akawauliza: “Watu wanasema kwamba mimi ni nani?” 19 Nao wakajibu: “Wamoja wanasema kwamba wewe ni Yoane Mubatizaji, wengine wanasema kwamba wewe ni Elia, na wengine wanasema kwamba wewe ni mumoja wa manabii wa zamani aliyefufuka.” 20 Na halafu Yesu akawauliza: “Na ninyi munasema kwamba mimi ni nani?” Petro akamujibu: “Wewe ni Masiya wa Mungu.” Yesu anajulisha habari za kufa na kufufuka kwake ( Mat 16.20-28 ; Mk 8.30–9.1 ) 21 Halafu Yesu akawaagiza wanafunzi wake kwa nguvu wasimwambie mutu yeyote maneno hayo. 22 Naye akaongeza kuwaambia: “Sherti Mwana wa Mutu ateswe na kukataliwa na wasimamizi wa watu, pamoja na walimu wa Sheria. Atauawa na kwa siku ya tatu kisha kufa kwake, atafufuka.” 23 Kisha akawaambia wote: “Kama mutu akitaka kunifuata, asijishugulikie mwenyewe, lakini ajitolee kwa kubeba musalaba wake kila siku na kunifuata. 24 Kwa maana mutu anayetaka kulinda uzima wake ataupoteza; lakini yule atakayetoa uzima wake kwa ajili yangu ataulinda. 25 Ni faida gani kwa mutu kupata utajiri wote wa dunia, lakini anapoteza uzima wake mwenyewe au kujiangamiza? 26 Kwa hiyo mutu yeyote anayesikia haya juu yangu na juu ya mafundisho yangu, Mwana wa Mutu atasikia haya juu yake vilevile. Itakuwa vile atakapokuja katika utukufu wake, akitukuzwa na Baba yake pamoja na wamalaika wake watakatifu. 27 Kweli ninawaambia: wamoja kati ya watu wanaokuwa hapa hawatakufa mbele ya kuona Ufalme wa Mungu unasimama.” Yesu anageuzwa sura ( Mat 17.1-8 ; Mk 9.2-8 ) 28 Ilipotimia karibu siku nane nyuma ya pale Yesu aliposema maneno hayo, yeye akawatwaa Petro, Yakobo na Yoane, akapanda pamoja nao kwa mulima kwa kuomba. 29 Naye alipokuwa akiomba, sura yake ikageuka, nazo nguo zake zikageuka nyeupe sana na zenye kumetameta. 30-31 Watu wawili, Musa na Elia wakatokea, wakionekana katikati ya mwangaza wa utukufu kutoka mbingu. Walikuwa wakizungumuza na Yesu juu ya yale yatakayomutokea kule Yerusalema, kusudi atimize yaliyoandikwa juu yake. 32 Kwa wakati ule Petro na wenzake walikuwa wamewezwa sana na usingizi; lakini wakaamuka, wakaona ule utukufu wa Yesu na wale watu wawili waliokuwa wakisimama pamoja naye. 33 Watu wale walipokuwa wakiachana na Yesu, Petro akamwambia: “Bwana, ni vizuri kuona sisi tuko hapa. Tujenge vibanda vitatu, kimoja chako, kimoja cha Musa na kingine cha Elia.” (Naye alisema hayo bila kufikiri.) 34 Alipokuwa hajamaliza kusema, wingu likatokea na kuwafunika. Nao wanafunzi wale wakaogopa kwa kuona wamefunikwa na lile wingu. 35 Na sauti ikasikilika toka katikati ya lile wingu, ikisema: “Huyu ni Mwana wangu niliyemuchagua. Mumusikilize!” 36 Nyuma ya kusikilika kwa sauti ile, Yesu akaonekana amebaki peke yake. Wale wanafunzi wakachunga mambo hayo yote kwa siri wala hawakumwambia mutu neno katika siku zile. Yesu anaponyesha mutoto mwenye pepo ( Mat 17.14-18 ; Mk 9.14-27 ) 37 Kesho yake, Yesu na wale wanafunzi watatu waliposhuka toka kwa mulima, kundi kubwa la watu wakamufikia. 38 Na mutu mumoja kati ya kundi akalalamika, akisema: “Mwalimu, ninakusihi umwangalie mwana wangu, kwa maana yeye ni mutoto wa pekee! 39 Pepo anapomukamata, mara moja mutoto analalamika, na yule pepo anamutikisatikisa kwa nguvu hata pofu inamutoka. Huyo pepo hatoki ndani yake upesi, naye anamutesa sana. 40 Niliwasihi wanafunzi wako wamufukuze, lakini hawakuweza.” 41 Na Yesu akajibu: “Ee ninyi watu wa kizazi kisichoamini Mungu na chenye kupotoka! Nitakaa pamoja nanyi tena mpaka wakati gani? Nitawavumilia tena mpaka wakati gani? Umulete mutoto wako hapa.” 42 Yule mutoto alipokuwa akijongea karibu na Yesu, yule pepo akamutupa chini na kumutikisa kwa nguvu. Lakini Yesu akamukaripia yule pepo na kumuponyesha mutoto. Kisha akamurudisha kwa baba yake. 43 Na watu wote wakashangaa sana kwa kuona uwezo mukubwa wa Mungu. Nao wote walipokuwa wakishangaa juu ya mambo hayo yote Yesu aliyofanya, yeye akawaambia wanafunzi wake: Yesu anajulisha tena habari za kufa na kufufuka kwake ( Mat 17.22-23 ; Mk 9.30-32 ) 44 “Munitegee sikio vizuri: Mwana wa Mutu atatolewa katika mikono ya watu.” 45 Lakini wao hawakufahamu maana ya maneno hayo, kwa sababu yalikuwa yamefichwa kwao, kusudi wasipate kuyatambua. Nao waliogopa kumwuliza maana yake. Ni nani anayekuwa mukubwa katika Ufalme wa Mungu ( Mat 18.1-5 ; Mk 9.33-37 ) 46 Wanafunzi waliingiwa na wazo la kutafuta kujua nani anayekuwa mukubwa kati yao. 47 Yesu akatambua mawazo yao. Kwa hiyo akatwaa mutoto akamuweka karibu naye 48 na kuwaambia: “Anayemupokea mutoto mudogo kama huyu kwa jina langu, ananipokea mimi. Naye anayenipokea mimi, anamupokea yule aliyenituma. Kwa maana yule anayekuwa mudogo kati yenu ndiye anayekuwa mukubwa.” Asiyekuwa adui yenu ni wa upande wenu ( Mk 9.38-40 ) 49 Naye Yoane akasema: “Bwana, tulimwona mutu mumoja akifukuza pepo kwa jina lako, nasi tulimukataza, kwa sababu yeye si wa kundi letu.” 50 Lakini Yesu akamujibu: “Musimukataze, kwa maana yule asiyekuwa adui yenu ni wa upande wenu.” Wasamaria wanakataa kumukaribisha Yesu 51 Siku za Yesu za kunyanyuliwa mbinguni zikakaribia. Kwa hiyo akakusudia sana kwenda Yerusalema, 52 akawatuma wajumbe watangulie mbele yake. Wale wajumbe wakaondoka na kuingia katika kijiji kimoja cha Wasamaria kusudi wamutayarishie vitu vyote kule. 53 Lakini wale wakaaji wakakataa kumupokea Yesu kwao kwa sababu alikuwa katika safari kwenda Yerusalema. 54 Wanafunzi wake, Yakobo na Yoane walipoona mambo hayo, wakasema: “Bwana, unataka tuombe moto uwashukie toka mbinguni na kuwateketeza?” 55 Lakini Yesu akawageukia na kuwakaripia. 56 Kisha wakaondoka kwenda katika kijiji kingine. Namna ya kumufuata Yesu ( Mat 8.19-22 ) 57 Nao walipokuwa katika njia, mutu mumoja akamwambia Yesu: “Nitakufuata popote utakapokwenda.” 58 Yesu akamwambia: “Mbweha wako na makao yao ndani ya matundu nao ndege wako na chicha, lakini Mwana wa Mutu hana nafasi ya kulala.” 59 Naye Yesu akamwambia mutu mwingine: “Unifuate.” Lakini mutu yule akamujibu: “Bwana, unipe ruhusa niende kwanza kuzika baba yangu.” 60 Yesu akamwambia: “Uwaache hao wafu wazike wafu wao, lakini wewe uende kutangaza habari ya Ufalme wa Mungu.” 61 Mutu mwingine akasema: “Bwana, nitakufuata lakini unipe ruhusa niende kwanza kuaga jamaa yangu.” 62 Lakini Yesu akamujibu: “Mutu yeyote anayeanza kulima na kuanza tena kuangalia nyuma hafai kutumika katika Ufalme wa Mungu.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo