Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Luka 8 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Wanawake waliomusaidia Yesu katika kazi yake

1 Nyuma ya pale Yesu akapita katika miji na vijiji mbalimbali, akihubiri na kutangaza Habari Njema ya Ufalme wa Mungu. Wale wanafunzi wake kumi na wawili walienda naye

2 pamoja na wanawake wamoja ambao alikuwa ameondosha pepo ndani yao na magonjwa mengine. Kati ya wale wanawake kulikuwa Maria (aliyeitwa wa Magdala), aliyekuwa ameponyeshwa pepo saba;

3 na Yoana muke wa Kuza, huyo mume wake alikuwa musimamizi wa mali ya Herode, pamoja na Suzana na wengine wengi. Wanawake hawa walitumia mali yao kwa kuwasaidia Yesu na wanafunzi wake.


Mufano wa mupandaji wa mbegu
( Mat 13.1-9 ; Mk 4.1-9 )

4 Watu walikuwa wakimufikia Yesu toka miji mbalimbali, na kundi kubwa la watu walikusanyika. Halafu akawaambia mufano huu:

5 “Mupandaji mumoja alikwenda kupanda mbegu. Alipokuwa akipanda mbegu katika shamba lake, zimoja zikaanguka pembeni ya njia. Watu wakazikanyagakanyaga na ndege wakazikula.

6 Zingine zikaanguka kwenye udongo wenye mawe. Nazo zilipoota, mara moja zikakauka kwa sababu ya ukosefu wa maji.

7 Mbegu zingine zikaanguka katikati ya miiba. Ile miiba ikaota pamoja na mbegu, na kuzisonga.

8 Lakini mbegu zingine zikaanguka katika udongo muzuri; nazo zikaota na kutoa matunda, kila moja punje mia.” Yesu alipokwisha kuwaambia hayo yote, akasema: “Mwenye kuwa na masikio ya kusikia, asikie!”


Kusudi la kutumia mifano
( Mat 13.10-17 ; Mk 4.10-12 )

9 Halafu wanafunzi wa Yesu wakamwuliza maana ya mufano huo.

10 Akawajibu: “Ninyi mumefunuliwa kujua siri ya Ufalme wa Mungu, lakini kwa watu wengine si vile. Wao wanaambiwa maneno hayo kwa njia ya mifano, kusudi waangalie, lakini wasione kitu, nao wasikie, lakini wasifahamu kitu.”


Yesu anaeleza maana ya mufano wa mupandaji
( Mat 13.18-23 ; Mk 4.13-20 )

11 “Basi hii ndiyo maana ya ule mufano wa mupandaji: mbegu ni mufano wa neno la Mungu.

12 Nafasi ile mbegu zilipoanguka pembeni ya njia ni mufano wa watu wanaosikia neno la Mungu. Lakini Shetani anakuja na kuondoa lile neno katika mioyo yao kusudi wasiamini na kuokolewa.

13 Udongo wenye mawe pahali mbegu zilipoanguka ni mufano wa watu wanaosikia neno na kulipokea kwa furaha, lakini halizami ndani yao kama mizizi. Wanaliaminia kwa muda mufupi tu, nayo majaribu yanapowafikia, wanaliacha.

14 Na mbegu zilizoanguka katika miiba ni mufano wa wale wanaosikia, lakini masumbuko, utajiri na raha ya dunia vinawasonga hata wanashindwa kutoa matunda yanayokomaa.

15 Nao udongo muzuri walimopanda mbegu, ni mufano wa watu wanaosikia neno la Mungu na kulishika kwa moyo mwema na kwa uhaki. Ndio wale wanaovumulia hata wanatoa matunda mazuri.


Mufano wa taa
( Mk 4.21-25 )

16 “Hakuna mutu anayewakisha taa na kuifunika na chombo fulani au kuiweka chini ya kitanda. Lakini anaiweka juu ya kinara kusudi wanaoingia ndani wapate kuona mwangaza.

17 Na ni hivi hakuna chochote kinachofichwa kitakachokosa kuonekana wazi, wala hakuna siri itakayokosa kufunuliwa waziwazi.

18 “Basi mufanye angalisho na jinsi munavyosikia maneno. Kwa maana mutu anayekuwa na kitu, ataongezewa kingine, lakini mutu asiyekuwa na kitu, atanyanganywa kile anachozania kuwa nacho.”


Mama na wandugu za Yesu
( Mat 12.46-50 ; Mk 3.31-35 )

19 Mama na wandugu za Yesu wakakuja kumwona, lakini hawakuweza kufika karibu naye kwa ajili ya kundi kubwa la watu.

20 Halafu watu wakamwambia Yesu: “Mama yako na wandugu zako wanasimama inje, wanataka kukuona.”

21 Lakini Yesu akawajibu: “Mama yangu na wandugu zangu ni wale wanaosikia neno la Mungu na kulishika.”


Yesu anatuliza zoruba
( Mat 8.23-27 ; Mk 4.35-41 )

22 Siku moja Yesu akaingia ndani ya chombo pamoja na wanafunzi wake. Naye akawaambia: “Tuvuke ngambo ya ziwa.” Basi wakaondoka.

23 Nao walipokuwa wakivuka ziwa, Yesu akalala usingizi. Mara moja zoruba kali ikaanza kuvuma, hata maji yakaanza kuingia ndani ya chombo, nao wakakuwa katika hatari.

24 Basi wanafunzi wake wakamujongelea, wakamwamusha wakisema: “Bwana, Bwana, tunakufa!” Yesu alipoamuka, akakaripia zoruba, nayo ikakoma na maji yakatulia.

25 Halafu akawaambia wanafunzi wake: “Imani yenu iko wapi?” Nao wakaogopa na kushangaa, wakiulizana: “Huyu ni mutu gani? Anaamuru hata zoruba na ziwa, navyo vinamutii!”


Yesu anaponyesha mutu mwenye pepo
( Mat 8.28-34 ; Mk 5.1-20 )

26 Yesu na wanafunzi wake wakaezeka chombo katika inchi ya Wagerasi, kuelekea Galilaya.

27 Yesu alipotoka ndani ya chombo, akakutana na mutu mumoja kule katika muji aliyeshikwa na pepo. Mutu yule hakuvaa nguo tangu siku nyingi, wala hakuishi ndani ya nyumba, lakini aliishi kwenye makaburi.

28 Wakati alipomwona Yesu, akalalamika na kuanguka mbele yake, na kusema kwa nguvu: “Yesu, Mwana wa Mungu Mukubwa, kuna neno kati yako na mimi? Ninakusihi, usinitese!”

29 Alisema vile kwa sababu Yesu alikuwa amemwamuru huyo pepo, atoke ndani ya yule mutu. Huyo pepo alimukamata mutu yule mara nyingi, na ijapokuwa watu walimufunga na minyororo na vifungo vya chuma kusudi asitoroke, yeye alivikata. Na yule pepo alimusukuma kwenda katika jangwa.

30 Yesu akamwuliza: “Jina lako nani?” Naye akamujibu: “Jina langu ni ‘Jeshi.’ ” Alisema vile kwa sababu ndani ya mutu yule mulikuwa pepo wengi.

31 Nao wale pepo walimusihi Yesu kwamba atakapowafukuza asiwaamuru kutumbukia ndani ya shimo lisilokuwa na mwisho.

32 Na karibu na pale kulikuwa kundi la nguruwe wengi waliokuwa wakijitafutia chakula kwenye mulima. Wale pepo wakamusihi Yesu awaruhusu kuingia ndani ya wale nguruwe. Naye akawaruhusu.

33 Basi pepo wakamutoka mutu yule na kuingia ndani ya wale nguruwe. Kundi zima la nguruwe wakatelemuka mbio kwenye mulima na kutumbukia ndani ya maji, nao wakazama.

34 Wachungaji wa nguruwe walipoona jambo lililotokea, wakaenda mbio kupasha habari katika muji na katika vijiji.

35 Watu wakakuja kusudi waone jambo lile. Walipofika kwa Yesu, wakamukuta yule mutu aliyetokwa na pepo akiikaa mbele ya Yesu, akiwa amevaa nguo, nayo akili yake ikiwa sawa. Basi watu wale wakaogopa.

36 Wale walioona yale yaliyotendeka wakawaelezea watu namna yule aliyekuwa na pepo alivyoponyeshwa.

37 Halafu watu wote wa inchi ya Wagerasi wakashikwa na woga mukubwa, kwa hiyo wakamwomba Yesu aondoke kwao. Basi Yesu akaingia ndani ya chombo, kusudi apate kuondoka kule.

38 Mutu yule aliyeponyeshwa pepo akamusihi Yesu aende pamoja naye, lakini akamukatalia, akimwambia:

39 “Rudia kwako na ueleze mambo yote Mungu aliyokutendea.” Basi yule mutu akajiendea, na kutangaza fasi zote katika muji wake mambo Yesu aliyomutendea.


Binti ya Yairo na mwanamuke aliyegusa nguo ya Yesu
( Mat 9.18-26 ; Mk 5.21-43 )

40 Yesu alipovuka kurudia ngambo ingine ya ziwa, watu wengi wakamupokea kwa furaha, kwa sababu wote walikuwa wakimungojea.

41 Mukubwa mumoja wa nyumba ya kuabudia aliyeitwa Yairo akafika. Alijitupa mbele ya Yesu na kumusihi afike kwake,

42 kwa sababu alikuwa na mutoto mumoja binti wa pekee mwenye umri wa miaka yapata kumi na miwili, na aliyekuwa karibu kufa. Yesu alipokuwa akienda kule, kundi kubwa la watu walimusongasonga.

43 Kati yao kulikuwa mwanamuke mumoja mwenye ugonjwa wa kutokwa na damu kwa muda wa miaka kumi na miwili. Alikuwa ametumia mali yake yote kwa kulipa waganga, lakini hakuna hata mumoja wao ambaye aliweza kumuponyesha.

44 Mwanamuke huyu akakuja nyuma ya Yesu na kugusa upindo wa nguo yake. Na mara moja akapona ule ugonjwa wa kutokwa na damu.

45 Yesu akauliza: “Ni nani aliyenigusa?” Watu wote wakakana, lakini Petro akasema: “Bwana, hauoni kwamba watu wengi wanakuzunguka na kukusonga?”

46 Lakini Yesu akasema: “Kuna mutu aliyenigusa kwa maana nimejisikia kwamba nguvu zimenitoka.”

47 Yule mwanamuke alipoona kwamba ametambulikana, akakuja akitetemeka kwa woga na kujitupa mbele ya Yesu. Na pale mbele ya watu wote, akaeleza sababu gani alimugusa na namna alivyoponyeshwa mara moja.

48 Na Yesu akamwambia: “Binti yangu, imani yako imekuponyesha. Ujiendee na amani.”

49 Yesu alipokuwa hajamaliza kusema maneno hayo, mujumbe mumoja akafika toka kwa yule mukubwa Yairo wa nyumba ya kuabudia na kumwambia: “Binti yako amekwisha kufa. Usiendelee kumusumbua Mwalimu.”

50 Lakini Yesu aliposikia vile, akamwambia Yairo: “Usiogope, amini tu, atapona.”

51 Yesu alipofika ndani ya nyumba ya Yairo, hakuruhusu mutu kuingia pamoja naye isipokuwa Petro, Yoane, Yakobo, baba na mama wa mutoto.

52 Watu wote walikuwa wakilia na kusikitika sana kwa ajili ya kifo cha mutoto. Lakini Yesu akasema: “Musilie, kwa maana hakufi, lakini analala tu!”

53 Nao wakamuchekelea kwa sababu walijua kwamba amekwisha kufa.

54 Lakini Yesu akamushika mukono na kumwambia kwa sauti kubwa: “Mutoto, simama!”

55 Naye akakuwa tena muzima, na mara moja akasimama. Yesu akawaamuru wamupe chakula.

56 Wazazi wake wakashangaa sana na Yesu akawaagiza wasimwambie mutu yeyote yale yaliyotokea.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan