Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Luka 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yesu anaponyesha mutumishi wa mukubwa wa waaskari
( Mat 8.5-13 )

1 Yesu alipokwisha kusema maneno hayo yote kwa watu waliomusikiliza, akaenda Kapernaumu.

2 Kule kulikuwa mukubwa mumoja wa waaskari aliyekuwa na mutumishi wake mupendwa sana. Mutumishi yule alikuwa mugonjwa karibu kufa.

3 Yule mukubwa aliposikia habari ya Yesu, akatuma kwake wasimamizi wamoja wa Wayuda, kwa kumwomba akuje kumuponyesha mutumishi wake.

4 Wale wasimamizi walipofika kwa Yesu, wakamusihi sana, wakasema: “Umufanyie mutu huyu sawa anavyokuomba, kwa maana anastahili kutendewa vile.

5 Yeye anapenda taifa letu na ni yeye aliyetujengea nyumba yetu ya kuabudia.”

6 Halafu Yesu akaenda pamoja nao. Alipokuwa karibu na kwa yule mukubwa wa waaskari, yule mukubwa akawatuma warafiki zake kumwambia Yesu: “Bwana, usijisumbue, kwa maana mimi sistahili kukupokea ndani ya nyumba yangu.

7 Ndiyo sababu nilijiona kwamba sistahili kuja kwako. Lakini sema neno tu, na mutumishi wangu atapona.

8 Hata mimi vilevile ni mutu mwenye kuwa chini ya mamlaka ya wakubwa, na tena niko na waaskari wengine wanaokuwa chini yangu. Nami nikimwambia mumoja: ‘Kwenda!’ naye anakwenda! Nikimwambia mwingine: ‘Kuja!’ naye anakuja! Nami nikimwambia mutumishi wangu: ‘Fanya hivi!’ naye anafanya vile!”

9 Yesu aliposikia maneno haya, akashangaa sana na yule mukubwa, na kugeukia kundi la watu waliomufuata, na kusema: “Ninawaambia: katika inchi yote ya Israeli sijaona bado mutu anayekuwa na imani kubwa kama huyu.”

10 Halafu wale wasimamizi waliotumwa wakarudia kwenye nyumba, nao wakamukuta yule mutumishi amekwisha kupona.


Yesu anamufufua mwana wa mujane

11 Kesho yake nyuma ya maneno haya, Yesu akaenda katika muji Naina, nao wanafunzi wake na kundi kubwa la watu wakamufuata.

12 Alipokaribia kwenye mulango wa ukuta wa muji, kukatokea watu wanaobeba maiti ya kijana mumoja aliyekuwa mutoto wa pekee wa mama mumoja mujane. Nao watu wengi wa muji ule walikuwa wakimusindikiza yule mama.

13 Bwana alipomwona yule mama, akamusikilia huruma na kumwambia: “Usilie.”

14 Kisha akajongea, akagusa sanduku, nao watu waliokuwa wakilibeba wakasimama. Akasema: “Kijana, ninakuamuru, amuka!”

15 Halafu yule aliyekuwa maiti akaamuka, akaikaa na kuanza kusema. Na Yesu akamurudisha kwa mama yake.

16 Watu wote wakashikwa na woga, nao wakamutukuza Mungu, wakisema: “Nabii mukubwa ametokea tena kwetu! Mungu amekuja kuwasaidia watu wake.”

17 Na jambo hili Yesu alilolifanya likaenea katika Yudea yote na katika inchi zote zinazokuwa pembeni.


Wajumbe wa Yoane
( Mat 11.2-19 )

18 Wanafunzi wa Yoane wakamwelezea mambo hayo yote yaliyotokea. Kwa hiyo Yoane akawaita wawili kati yao

19 na kuwatuma kwa Bwana kumwuliza: “Wewe ndiwe yule aliyepaswa kuja kutuokoa au tumungojee mwingine?”

20 Wale wanafunzi walipofika kwa Yesu wakamwambia: “Yoane Mubatizaji ametutuma kwako kukuuliza ikiwa wewe ndiwe yule aliyepaswa kuja au tumungojee mwingine.”

21 Saa ile ile Yesu akawaponyesha watu wengi walioteswa na magonjwa na ulema mbalimbali pamoja na wenye pepo, na kuwaponyesha hata vipofu wengi.

22 Halafu Yesu akawajibu wale wajumbe: “Mwende kumwelezea Yoane mambo muliyoona na kusikia: vipofu wanapata kuona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanapata kusikia, wafu wanafufuliwa na Habari Njema inahubiriwa kwa wamasikini.

23 Heri mutu yule ambaye sitakuwa kikwazo kwake.”

24 Wale wajumbe wa Yoane walipokwisha kuondoka, Yesu akaanza kuwaambia makundi ya watu habari za Yoane akisema: “Mulienda katika jangwa kuangalia nini? Tete linalotikiswa na upepo? Hapana!

25 Basi mulienda kuangalia nini? Mutu aliyevaa nguo nzuri? Hapana! Wale wanaovaa nguo za bei kali na kuishi katika raha wanakaa katika nyumba za kifalme.

26 Basi mulienda kuangalia nini? Nabii? Ndiyo, ninawaambia ninyi kwamba yeye ni mukubwa kupita hata nabii.

27 Huyu ndiye maneno haya yameandikwa juu yake katika Maandiko Matakatifu: ‘Ninamutuma mujumbe wangu akutangulie, kusudi akutengenezee njia utakayopitia!’

28 Ninawaambia: kati ya watu wanaoishi katika dunia, hakuna anayekuwa mukubwa kuliko Yoane. Lakini yeyote anayehesabiwa kuwa mudogo katika Ufalme wa Mungu anahesabiwa kuwa mukubwa kuliko yeye.”

29 (Watu wote waliomusikiliza, na walipishaji wa kodi vilevile, wakakubali kwamba Mungu ni mwenye haki, hata wakabatizwa na Yoane.

30 Lakini Wafarisayo na walimu wakubwa wa Sheria walikataa mupango wa Mungu juu yao, na kukataa kubatizwa na Yoane.)

31 “Basi nitawafananisha watu wa kizazi hiki na nini? Wao ni watu wa namna gani?

32 Wanafanana na watoto wanaoikaa kwenye nafasi ya makutano wanaowaita wenzao, wakisema: ‘Tuliwapigia ngoma, lakini hamukucheza! Tuliimba wimbo wa kilio, lakini hamukulia!’

33 Ni hivi vilevile, Yoane Mubatizaji alikuja, yeye anafunga kula chakula na kunywa divai, nanyi munasema: ‘Yuko na pepo.’

34 Mwana wa Mutu alikuja, yeye anakula na kunywa, nanyi munasema: ‘Angalia huyu mulafi na mulevi, rafiki ya walipishaji wa kodi na watenda maovu.’

35 Lakini hekima ya Mungu ilihakikishwa kuwa ya haki na wote wanaoikubali.”


Yesu katika nyumba ya Simoni Mufarisayo

36 Siku moja Mufarisayo mumoja akamwalika Yesu kwake kuja kula chakula. Basi Yesu akaenda kwenye nyumba ya yule Mufarisayo, na kuikaa kula chakula.

37 Katika muji ule kulikuwa mwanamuke mumoja aliyejulikana kuwa mwenye mwenendo mubaya. Mwanamuke yule alipopata habari kama Yesu alikuwa akikula ndani ya nyumba ya yule Mufarisayo, akafika akileta chupa la jiwe linalojaa marasi ya bei kali.

38 Akakuja kuinama kwenye miguu ya Yesu, akilia. Machozi yake yakamwangika juu ya miguu ya Yesu, akaipanguza na nywele zake, akaibusu na kuipakaa marasi.

39 Yule Mufarisayo aliyemwalika Yesu alipoona vile, akajisemesha: “Kama mutu huyu angekuwa kweli nabii, angetambua mwanamuke huyu anayemugusa ni wa namna gani. Angetambua kwamba yeye ni mwenye mwenendo mubaya.”

40 Yesu akamwambia yule Mufarisayo: “Simoni, niko na neno la kukuuliza.” Simoni akajibu: “Mwalimu, sema.”

41 Yesu akasema: “Kulikuwa watu wawili waliokopesha feza kutoka kwa mutu mumoja. Mumoja alikuwa na deni ya vikoroti mia tano vya feza na mwingine vikoroti makumi tano.

42 Na kwa kuona wote wawili hawakukuwa na uwezo wa kulipa madeni yao, yule bwana akawasamehe. Sasa, uniambie, kati ya hawa wawili, ni nani atakayemupenda yule bwana zaidi?”

43 Simoni akajibu: “Ninazani kwamba ni yule aliyesamehewa deni kubwa zaidi.” Na Yesu akamwambia: “Umejibu vizuri.”

44 Halafu akamugeukia yule mwanamuke na kumwambia Simoni: “Unamwona mwanamuke huyu? Niliingia ndani ya nyumba yako, nawe haukunipa maji ya kunawa miguu yangu, lakini mwanamuke huyu amenawa miguu yangu na machozi yake na kuipanguza na nywele zake.

45 Wewe haukunibusu kwa kunisalimia, lakini mwanamuke huyu hakuacha kubusu miguu yangu tangu nilipoingia humu.

46 Wewe haukupakaa mafuta juu ya kichwa changu, lakini yeye amepakaa marasi juu ya miguu yangu.

47 Ni kwa sababu hii ninakuambia kwamba upendo ambao mwanamuke huyu alioonyesha unahakikisha kwamba Mungu amemusamehe zambi zake zinazokuwa nyingi. Lakini yule anayesamehewa kwa machache haonyeshi upendo zaidi.”

48 Kisha Yesu akamwambia yule mwanamuke: “Zambi zako zimesamehewa.”

49 Na waalikwa wengine waliokuwa wakikula pamoja na Yesu, wakaanza kujisemesha: “Ni mutu gani huyu anayesamehe zambi?”

50 Lakini Yesu akamwambia tena yule mwanamuke: “Kwenda na amani, imani yako imekuokoa.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan