Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Luka 23 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yesu mbele ya liwali Pilato
( Mat 27.1-2 , 11-14 ; Mk 15.1-5 ; Yn 18.28-38 )

1 Kisha watu wote wa Baraza Kubwa wakasimama, wakamupeleka Yesu mbele ya Pilato.

2 Wakaanza kumushitaki, wakisema: “Tulimukuta mutu huyu akiwashawishi watu wa taifa letu kufanya uasi. Yeye alikuwa akiwaambia kwamba wasilipe kodi kwa Mufalme wa Roma. Na zaidi ya hii anasema kwamba yeye ndiye Kristo, Mufalme aliyengojewa.”

3 Basi Pilato akamwuliza Yesu: “Wewe ndiwe mufalme wa Wayuda?” Yesu akamujibu: “Ni wewe ndiwe umesema.”

4 Halafu Pilato akawaambia wakubwa wa makuhani na kundi la watu: “Mimi sioni hata sababu moja ya kumuhukumu mutu huyu.”

5 Lakini wakazidi kusema kwa nguvu: “Kwa njia ya mafundisho yake anawashawishi watu kufanya uasi katika Yudea yote. Alianzia Galilaya na sasa amefika hapa.”


Yesu mbele ya mufalme Herode

6 Wakati Pilato aliposikia maneno hayo, akauliza: “Mutu huyu ni wa Galilaya?”

7 Naye alipojua kwamba Yesu alikuwa mutu wa jimbo lililokuwa chini ya utawala wa Herode, akamutuma kwa Herode, kwa maana alikuwa Yerusalema siku zile.

8 Herode alipomwona Yesu, akafurahi sana. Tangu siku nyingi alitamani kumwona kwa sababu alikuwa amesikia habari zake, naye alitumaini kuona kitambulisho kutoka kwake.

9 Akamwuliza Yesu maneno mengi, lakini yeye hakumujibu neno.

10 Wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria waliokuwa pale wakatoa mashitaki makubwa sana juu ya Yesu.

11 Basi Herode na waaskari wake wakamuchekelea Yesu na kumuzarau. Wakamuvalisha nguo zinazokuwa sawa za mufalme na kumurudisha kwa Pilato.

12 Siku ile Herode na Pilato waliokuwa waadui tangu zamani, wakageuka kuwa warafiki.


Yesu anahukumiwa kufa
( Mat 27.15-26 ; Mk 15.6-15 ; Yn 18.39–19.16 )

13 Basi Pilato akafanya mukutano wa wakubwa wa makuhani, nao wasimamizi wa watu pamoja na watu wao.

14 Akawaambia: “Mumeniletea mutu huyu mukisema kwamba anashawishi watu kufanya uasi. Basi nimemwuliza mbele yenu juu ya maneno yale, lakini sikumwona na kosa lolote ninyi munalomushitakia.

15 Hata Herode vilevile hakumwona na kosa; na ni kwa sababu hii amemurudisha kwetu. Mutu huyu hakufanya hata kosa moja linalomustahili kuhukumiwa kufa.

16 Basi nitaamuru apigwe fimbo, na kisha nitamufungua.” [

17 Kila sikukuu ya Pasaka, Pilato alipaswa kuwafungulia watu mufungwa mumoja.]

18 Lakini wote pamoja wakapiga kelele wakisema: “Umwue mutu huyu na utufungulie Baraba!”

19 (Baraba alikuwa amefungwa kwa ajili ya fujo iliyofanyika katika muji na kwa ajili ya kuua watu.)

20 Kufuatana na vile Pilato alivyotaka kumufungua Yesu, yeye akasema tena na watu.

21 Lakini wakapiga tena kelele, wakisema: “Umutundike juu ya musalaba! Umutundike juu ya musalaba!”

22 Pilato akawaambia kwa mara ya tatu: “Alifanya ubaya gani? Mimi sikumwona na hata kosa moja linalomustahili kuhukumiwa kufa. Nitaamuru apigwe fimbo, na kisha nitamufungua.”

23 Lakini wakaendelea kupiga kelele kubwa wakiomba Yesu atundikwe juu ya musalaba. Na kwa mwisho akashindwa kwa sababu ya makelele yao.

24 Halafu akakata shauri la kuwatendea sawa walivyotaka.

25 Akamufungua yule mutu waliyetaka, aliyefungwa kwa ajili ya kuleta fujo na kuua watu, na kumutoa Yesu kwao kusudi wamutendee vile walivyotaka.


Yesu anatundikwa juu ya musalaba
( Mat 27.32-44 ; Mk 15.21-32 ; Yn 19.17-27 )

26 Nao walipokuwa wakimupeleka Yesu kwenda kutundikwa, wakakutana na mutu mumoja aliyeitwa Simoni, wa inchi ya Kurene, aliyekuwa akitoka kwenye vijiji. Wakamulazimisha abebe musalaba wa Yesu na kumufuata nyuma.

27 Kundi kubwa la watu walimufuata. Kati yao kulikuwa wanawake waliokuwa wakijipigapiga kwenye kifua kwa huzuni na kumulilia.

28 Yesu akawageukia na kuwaambia: “Ninyi wanawake wa Yerusalema, musinililie mimi, lakini mujililie ninyi wenyewe pamoja na watoto wenu.

29 Kwa maana siku zitakuja wakati watu watakaposema: ‘Heri wanawake wanaokuwa tasa, wale waliokosa kuzaa na kunyonyesha!’

30 Wakati ule watu wataanza kuiambia milima ‘Mutuangukie’, navyo vilima ‘Mutufunike!’

31 Kwa maana wakifanya hivi kwangu mimi ninayekuwa kama muti mubichi, basi watafanya nini kwenu munaokuwa kama muti unaokauka?”

32 Kulikuwa watu wengine wawili, watenda maovu; walipelekwa pamoja na Yesu kwa kutundikwa.

33 Walipowafikisha kwenye pahali palipoitwa “Kilima cha Mufupa wa Kichwa,” wakamutundika Yesu juu ya musalaba. Vilevile walitundika wale watenda maovu, mumoja kwa upande wa kuume wa Yesu na mwingine kwa upande wa kushoto.

34 Halafu Yesu akasema: “Baba uwasamehe, kwa maana hawajui jambo wanalofanya.” Waaskari wakagawanya nguo zake kwa kuzipigia kura.

35 Watu walisimama pale wakiangalia. Nao wakubwa wa Wayuda walimusimanga Yesu, wakisema: “Aliokoa watu wengine, sasa ajiokoe yeye mwenyewe ikiwa yeye ndiye Masiya, yule aliyechaguliwa na Mungu.”

36 Waaskari vilevile walimuzarau, wakamupelekea divai yenye kuchacha

37 na kumwambia: “Kama wewe ni mufalme wa Wayuda, ujiokoe wewe mwenyewe!”

38 Na mashitaki haya yalikuwa yameandikwa juu ya musalaba wake: “Huyu ndiye Mufalme wa Wayuda.”

39 Mumoja wa wale watenda maovu wawili waliotundikwa juu ya musalaba alimutukana, akisema: “Si wewe ndiwe Kristo? Basi ujiokoe wewe mwenyewe na kutuokoa sisi vilevile.”

40 Lakini mwenzake akamukaripia, akisema: “Wewe haumwogopi Mungu hata kidogo ingawa unapata azabu ile ile?

41 Sisi tunahukumiwa kwa haki, kwa maana tunaazibiwa kufuatana na matendo yetu mabaya. Lakini mutu huyu hakufanya ubaya wowote.”

42 Na akaongeza kusema: “Ee Yesu, usinisahau wakati utakapokuja katika ufalme wako!”

43 Yesu akamujibu: “Kweli ninakuambia wewe: leo hii utakuwa pamoja nami katika Paradizo.”


Kufa kwa Yesu
( Mat 27.45-56 ; Mk 15.33-41 ; Yn 19.28-30 )

44-45 Ilikuwa karibu na saa sita ya muchana, jua likafifia, kukakuwa giza katika inchi yote mpaka saa tisa. Pazia la hekalu likapasuka katikati.

46 Yesu akalalamika kwa sauti kubwa akisema: “Baba, ninatoa uzima wangu kwako.” Kisha kusema maneno haya, akakata roho.

47 Mukubwa wa waaskari alipoona mambo yale yaliyotokea, akamusifu Mungu, akisema: “Hakika mutu huyu alikuwa mwenye haki!”

48 Nalo kundi la watu waliofika kuangalia mambo yale, wakaona yote yaliyotokea. Kwa hiyo, wakarudia wakijipigapiga kwenye kifua kwa huzuni.

49 Na wote waliojuana sana naye, na hata wanawake waliomufuata tangia Galilaya, walisimama kwa mbali wakiangalia mambo hayo.


Kuzikwa kwa Yesu
( Mat 27.56-61 ; Mk 15.42-47 ; Yn 19.38-42 )

50-51 Kulikuwa mutu mumoja muzaliwa wa Arimatea, katika jimbo la Yuda, jina lake lilikuwa Yosefu. Mutu huyu alikuwa mwema na mwenye haki, naye alikuwa akitazamia Ufalme wa Mungu. Yeye alikuwa mumoja wa washauri wa Baraza Kubwa, lakini hakukubali shauri na matendo ya wenzake.

52 Yosefu alienda kwa Pilato kwa kumwomba maiti ya Yesu.

53 Alipokwisha kuishusha toka juu ya musalaba, akaifungafunga na vitambaa na kuiweka ndani ya kaburi lililochimbwa katika jiwe. (Ndani ya kaburi lile mulikuwa bado hamujazikwa mutu.)

54 Siku ile ilikuwa ya matayarisho ya siku ya Sabato iliyokuwa karibu kuanza.

55 Wale wanawake waliokuja na Yesu tangia Galilaya walimufuata Yosefu, wakaona kaburi na namna maiti ya Yesu ilivyowekwa mule.

56 Kisha wakarudia kwao kutengeneza mafuta na marasi ya kupakaa maiti. Siku ya Sabato wakapumzika kama Sheria ilivyoamuru.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan