Luka 21 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Sadaka ya mujane masikini ( Mk 12.41-44 ) 1 Yesu alipoinua macho, akawaona watajiri wakitia sadaka ndani ya sanduku ya sadaka za hekalu. 2 Akaona vilevile mujane mumoja masikini akitia ndani ya ile sanduku vikoroti viwili vidogo sana. 3 Basi akasema: “Kweli ninawaambia kwamba mujane huyu masikini ametoa mingi zaidi kuliko watu wote wengine. 4 Kwa maana hawa wengine wote walitoa sehemu ya mali wasiyokuwa nayo lazima. Lakini yeye ametoa kwa umasikini wake mali yote aliyokuwa nayo kwa kuishi.” Yesu anatangaza uharibifu wa hekalu ( Mat 24.1-2 ; Mk 13.1-2 ) 5 Wamoja kati ya wanafunzi wa Yesu walikuwa wakizungumuza juu ya hekalu, wakisema juu ya majengo yake mazuri ya mawe na juu ya vitu vingine vizuri watu walivyovitoa sadaka kwa Mungu. Lakini Yesu akasema: 6 “Kutakuwa siku vitu hivi munavyoona vitabomolewa, wala hakutabaki hata jiwe moja juu ya lingine.” Mateso yatakayokuwa mbele ya wakati wa mwisho ( Mat 24.3-14 ; Mk 13.3-13 ) 7 Halafu wakamwuliza: “Mwalimu, mambo hayo unayotoka kusema yatakuwa wakati gani? Na ni kitambulisho gani kitakachoonyesha kwamba yanataka kutimia?” 8 Yesu akawajibu: “Muangalie vizuri, musidanganywe. Watu wengi watakuja wakijiita kwa jina langu, wakisema kwamba wao ndio Kristo, nao wakati umetimia. Ingawa vile, musiwafuate. 9 Musiogope wakati mutakaposikia habari za vita na za mapinduzi. Sherti mambo hayo yatukie kwanza, lakini haionyeshi kwamba mwisho wa dunia unatimia palepale.” 10 Kisha Yesu akaongeza kusema: “Taifa litapigana na taifa, nao ufalme utapigana na ufalme. 11 Kutakuwa tetemeko kubwa la inchi. Vilevile kutakuwa njaa na magonjwa makali kwenye nafasi mbalimbali. Zaidi ya ile kutakuwa mambo ya kuogopesha na vitambulisho vya ajabu toka mbinguni. 12 Lakini mbele mambo hayo yote yatokee, mutakamatwa na kuteswa. Watawapeleka kwenda kuhukumiwa katika nyumba za kuabudia na kuwatia katika vifungo. Vilevile mutapelekwa mbele ya wafalme na ya wakubwa kwa ajili ya jina langu, 13 kusudi mutoe ushuhuda wangu mbele yao. 14 Basi mukusudie ndani ya moyo kwamba hamutajihangaisha mbele ya wakati kwa kutafuta kujua namna mutakavyojitetea. 15 Kwa maana mimi mwenyewe nitawapa masemi na hekima hata waadui zenu hawataweza kuyapinga wala kuyakataa. 16 Mutatolewa hata na wazazi wenu, wandugu zenu, na watu wa jamaa zenu pamoja na warafiki zenu. Nao watawaua wamoja kati yenu. 17 Watu wote watawachukia kwa ajili ya jina langu. 18 Lakini hata unywele mumoja wa kichwa chenu hautapotea. 19 Lakini muendelee kuvumilia, maana kwa njia ile mutaokoa uzima wenu.” Yesu anajulisha habari za uharibifu wa Yerusalema ( Mat 24.15-21 ; Mk 13.14-19 ) 20 “Wakati mutakapoona muji wa Yerusalema umezungukwa na waaskari, mujue kwamba uharibifu wake unakaribia. 21 Basi wale watakaokuwa Yudea, wakimbilie kwa milima, na wale watakaokuwa Yerusalema watoke ndani yake, nao wale watakaokutiwa katika mashamba wasiingie ndani ya muji. 22 Kwa maana siku zile zitakuwa siku za azabu ya Mungu, kusudi mambo yote yaliyoandikwa katika Maandiko Matakatifu yatimie. 23 Wanawake wenye mimba na wenye kunyonyesha watapata hasara katika siku zile! Kwa maana kutakuwa taabu kubwa katika inchi, na Mungu ataonyesha kasirani yake juu ya watu wa taifa hili. 24 Wamoja watauawa kwa vita na watapelekwa kuwa wafungwa katika inchi za mataifa yote. Vilevile mataifa mengine yatautawala Yerusalema mpaka nyakati zao za kuutawala zitakapokwisha.” Kuja kwa Mwana wa Mutu ( Mat 24.29-31 ; Mk 13.24-27 ) 25 “Vitambulisho vitaonekana katika jua, mwezi na nyota. Na hapa katika dunia mataifa yatakuwa na uchungu, na kushikwa na wasiwasi kwa ajili ya mungurumo na musukosuko wa bahari. 26 Watu watazimia kwa ajili ya hofu, wakingojea mambo yatakayotokea katika dunia, kwa maana vyote vyenye nguvu katika mbingu vitatikiswa. 27 Halafu wakati ule Mwana wa Mutu ataonekana akikuja katikati ya mawingu, kwa uwezo mwingi na kwa utukufu. 28 Mambo hayo yatakapoanza kutokea, muinue kichwa na kusimama na nguvu, kwa sababu wakati wa kukombolewa kwenu umekaribia.” Mafundisho toka muti wa tini ( Mat 24.32-35 ; Mk 13.28-31 ) 29 Kisha Yesu akawaambia wanafunzi wake mufano huu: “Muchunguze vizuri muti wa tini na miti yote mingine. 30 Munapoona kwamba majani yao yanaanza kuchipuka, munatambua wenyewe kwamba wakati wa jua kali unakaribia. 31 Vilevile wakati mutakapoona mambo hayo niliyotoka kutaja yanatokea, mujue kwamba Ufalme wa Mungu unakaribia. 32 “Kweli ninawaambia: hiki kizazi hakitapita mbele ya kutimia kwa mambo yote. 33 Mbingu na dunia vitatoweka, lakini maneno yangu hayatabadilika hata kidogo. Kukesha 34 “Mujilinde vizuri, kusudi musilemewe na kutafuta kula ulafi, kulewa na kusumbukia maisha. Kama si vile, Siku ile ya kurudia kwa Kristo itawafikia kwa rafla 35 sawa mutego. Kwa maana Siku ile itawafikia watu wote wa dunia. 36 Basi mukeshe na kuomba kila wakati, kusudi mupate nguvu ya kuepuka mambo hayo yote yatakayotokea, nanyi mupate kuweza kusimama mbele ya Mwana wa Mutu.” 37 Yesu alikuwa akipitisha muchana katika hekalu akihubiri, na usiku alikuwa akienda kulala kwenye mulima wa Mizeituni. 38 Watu wote walikuwa wakimufikia asubui mapema katika hekalu, kusudi wamusikilize. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo