Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Luka 19 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yesu na Zakayo

1 Yesu alipoingia katika muji Yeriko, akapita katikati yake.

2 Kule kulikuwa mutu mumoja jina lake Zakayo aliyekuwa mukubwa wa walipishaji wa kodi, naye alikuwa tajiri.

3 Alitaka kuona Yesu ni nani, lakini kwa vile alivyokuwa mutu mufupi, hakuweza kumwona kwa sababu watu walikuwa wengi.

4 Halafu akatangulia mbio na kupanda juu ya muti wa mukuyu apate kumwona Yesu, kwa sababu Yesu alipaswa kupitia kwenye njia ile.

5 Yesu alipofika kwenye nafasi ile akainua macho na kumwambia: “Zakayo, shuka mbio; kwa maana imenipasa kupanga ndani ya nyumba yako leo.”

6 Zakayo akashuka mbio na kumukaribisha kwa furaha.

7 Watu wote walioona hayo wakaanza kunungunika wakisema: “Amekwenda kupanga kwa mutenda maovu!”

8 Lakini Zakayo akasimama mbele ya Bwana na kumwambia: “Bwana! Ninawapa masikini nusu ya mali zangu, na kama nimetwaa kitu cha mutu kwa kumudanganya, nitamurudishia mara ine sawa na kitu kile.”

9 Yesu akamwambia: “Leo nyumba hii imeokolewa, kwa sababu mutu huyu vilevile ni wa uzao wa Abrahamu.

10 Kwa maana Mwana wa Mutu alikuja kutafuta na kuokoa yule aliyepotea.”


Mufano wa watumishi kumi
( Mat 25.14-30 )

11 Watu walipokuwa wakisikiliza maneno hayo, Yesu akaongeza kuwaambia mufano mumoja, kwa sababu alikuwa karibu na muji Yerusalema, na watu wale walizani kwamba siku za Ufalme wa Mungu zitafika saa ile ile.

12 Basi akasema: “Mutu mumoja mwenye heshima alifunga safari kwenda katika inchi ya mbali kusudi asimikwe kuwa mufalme na kisha arudie.

13 Mbele ya kuondoka kwake akawaita watu kumi kati ya watumishi wake, akamupatia kila mumoja furushi moja ya zahabu na kuwaambia: ‘Mufanye nazo uchuuzi mpaka nitakaporudia.’

14 Lakini wanainchi wenzake walimuchukia. Kwa hiyo wakatuma wajumbe kumufuata nyuma waende kusema: ‘Hatutaki mutu huyu kuwa mufalme wetu.’

15 “Lakini yule mutu mwenye heshima alisimikwa kuwa mufalme, na kurudia kwake. Halafu akaamuru wamwitie wale watumishi aliowapatia zahabu kusudi apate kujua kila mumoja amefaidia ngapi.

16 Mutumishi wa kwanza akakuja, akasema: ‘Bwana, furushi moja uliyonipatia imefaidia zingine kumi.’

17 Naye akamwambia: ‘Ni vizuri wewe mutumishi mwema. Kwa sababu ulikuwa mwaminifu katika jambo dogo, ninakupa utawala juu ya miji kumi.’

18 Mutumishi wa pili akakuja akasema: ‘Bwana, furushi moja uliyonipatia imefaidia zingine tano.’

19 Naye akamwambia: ‘Nawe vilevile ninakupa utawala juu ya miji mitano.’

20 Kisha mutumishi mwingine akakuja akasema: ‘Bwana, furushi yako ndiyo hii. Niliichunga vizuri nikiifunga ndani ya kitambaa,

21 kwa maana nilikuogopa kwa maana wewe ni mutu mugumu. Unatafutia nafasi usipowekea na kuvuna nafasi usipopanda.’

22 Yule bwana akamujibu: ‘Wewe mutumishi mubaya! Nitakuhukumu kufuatana na maneno yako. Ulijua kama mimi ni mutu mugumu, ninayetafutia nafasi nisipowekea na kuvuna nafasi nisipopanda.

23 Kwa nini basi haukuweka feza yangu katika banki, kusudi siku ya kurudia kwangu ningepata mali yangu pamoja na faida yake?’

24 Halafu akawaambia wale waliokuwa pale: ‘Mumunyanganye ile furushi moja na kuitoa kwa yule anayekuwa na furushi kumi.’

25 Wakamwambia: ‘Bwana, amekwisha kuwa na furushi kumi!’

26 Akawajibu: ‘Ninawaambia kwamba mutu anayekuwa na kitu ataongezewa kingine, lakini mutu asiyekuwa na kitu ataondolewa hata kidogo anachokuwa nacho.

27 Na sasa kwa ngambo ya wale waadui zangu walionikataa mimi kuwa mufalme wao, muwalete hapa na kuwaua mbele yangu.’ ”


Yesu anaingia Yerusalema
( Mat 21.1-11 ; Mk 11.1-11 ; Yn 12.12-19 )

28 Kisha kusema maneno hayo, Yesu akatembea mbele ya kundi la watu kwenda Yerusalema.

29 Alipokaribia kufika katika kijiji cha Betefage na cha Betania upande wa mulima wa Mizeituni, Yesu akawatuma wawili kati ya wanafunzi wake, akiwaambia:

30 “Mwende katika kijiji kinachokuwa mbele yenu. Mutakapofika kule, mutaona mwana-punda amefungwa, na hakuna mutu aliyekwisha kupanda juu yake. Mumufungue na kumuleta hapa.

31 Na kama mutu akiwauliza: ‘Kwa sababu gani munamufungua?’, mumwambie: ‘Bwana yuko na lazima ya kumutumia.’ ”

32 Basi wale waliotumwa wakaenda, wakakuta vyote kama vile Yesu alivyowaambia.

33 Walipokuwa wakimufungua, wenyeji wa mwana-punda yule wakawauliza: “Kwa nini munamufungua mwana-punda huyu?”

34 Wakajibu: “Bwana yuko na lazima ya kumutumia.”

35 Wakamuletea Yesu yule mwana-punda, wakatandika nguo zao juu yake na kumupandisha Yesu juu yake.

36 Alipokuwa akiendelea, watu walitandika nguo zao katika njia.

37 Alipokaribia Yerusalema kwenye mutelemuko wa mulima wa Mizeituni, kundi zima la wanafunzi wakafurahi na kuanza kumusifu Mungu kwa sauti kubwa kwa ajili ya miujiza yote waliyoiona.

38 Wakasema: “Abarikiwe mufalme anayekuja kwa jina la Bwana! Amani mbinguni na utukufu kwa Mungu anayekuwa juu!”

39 Kwa hiyo, wamoja kati ya Wafarisayo waliokuwa katika kundi la watu wakamwambia Yesu: “Mwalimu, uwakaripie wanafunzi wako!”

40 Yesu akawajibu: “Ninawaambia ninyi: kama watu hawa wakinyamaza, mawe yatalalamika.”


Yesu analilia Yerusalema

41 Yesu alipokaribia muji wa Yerusalema, na alipouona, akaulilia,

42 akisema: “Kama wewe vilevile ungejua leo hii kitu kinachoweza kukuletea amani! Lakini sasa kitu hicho kimefichwa, nawe hauwezi kukiona!

43 Kwa maana siku zitakufikia wakati waadui zako watakapokuzunguka kwa vita, watakapojenga ukuta wa kujikingia pembeni yako, na kukusonga pande zote.

44 Watakuharibu kabisa pamoja na wakaaji wako. Hawatakuachia hata jengo moja lisilobomolewa kwa sababu haukutambua wakati Mungu alipokuja kukuokoa.”


Yesu anatakasa hekalu
( Mat 21.12-17 ; Mk 11.15-19 ; Yn 2.13-22 )

45 Halafu Yesu akaingia katika hekalu, akaanza kufukuza wachuuzi

46 na kuwaambia: “Imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: ‘Nyumba yangu itakuwa nyumba ya maombi.’ Lakini ninyi munaigeuza kuwa nafasi ya kukutania ya wanyanganyi!”

47 Yesu alikuwa akifundisha kila siku ndani ya hekalu. Lakini wakubwa wa makuhani na walimu wa Sheria pamoja na wakubwa wa watu wakatafuta kumwua.

48 Lakini hawakupata namna ya kumwua, kwa sababu watu wote walimusikiliza kwa uangalifu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan