Luka 10 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yesu anawatuma wanafunzi makumi saba 1 Nyuma ya maneno hayo, Bwana akawachagua watu wengine makumi saba. Naye akawatuma wawili wawili wamutangulie kupita katika kila muji na kila nafasi yeye mwenyewe alipokuwa amekusudia kwenda. 2 Akawaambia: “Mavuno ni mengi, lakini watumishi ni wachache. Basi muombe Bwana wa mavuno atume watumishi kwa kuyavuna. 3 Muende! Muangalie, ninawatuma kama wana-kondoo katikati ya imbwa wa pori. 4 Musibebe feza, wala mufuko, wala viatu, na musimusalimie mutu katika njia. 5 Na katika nyumba yoyote mutakapoingia, mutoe kwanza salamu mukisema: ‘Amani ikuwe katika nyumba hii!’ 6 Kama mule mukiwa mutu anayekuwa tayari kupokea amani, atakaa na amani ile muliyomutakia. Kama si vile, amani ile itawarudilia. 7 Mukae ndani ya nyumba ile, nanyi mukule na kunywa chochote watakachowapa, kwa maana mutumishi anastahili kupewa mushahara wake. Musihame nyumba kwa nyumba. 8 Na katika muji wowote mutakamoingia, watu wakiwakaribisha, mukule na kunywa kile watakachowapa. 9 Muponyeshe wagonjwa wanaokuwa mule na kuwaambia wakaaji: ‘Ufalme wa Mungu umewakaribia ninyi.’ 10 Lakini katika muji wowote mutakamoingia, nao wakaaji wake wasipowakaribisha, muende kwenye viwanja vyake vya makutano na kusema: 11 ‘Tunawakungutia ninyi hata mavumbi ya muji wenu toka juu ya miguu yetu kuwa ushuhuda juu yenu. Na hata hivi mujue vizuri kwamba Ufalme wa Mungu umewakaribia.’ 12 Ninawaambia hakika kwamba kwa Siku ya hukumu muji ule utaazibiwa vikali zaidi kuliko muji Sodoma.” Azabu ya miji iliyokataa kuamini Yesu ( Mat 11.20-24 ) 13 Yesu akaendelea kusema: “Ole kwako muji Korazini! Ole kwako muji Betesaida! Kwa maana kama miujiza iliyofanyika ndani yenu ingefanyika katika muji wa Tiro na wa Sidona, wakaaji wa kule wangekwisha zamani kuonyesha masikitiko yao kwa kuvaa magunia na kujipakaa majivu, na kugeuka toka zambi zao. 14 Kwa hiyo, Siku ile ya hukumu, mutaazibiwa vikali zaidi kuliko Tiro na Sidona. 15 Nawe muji Kapernaumu, unafikiri kwamba utapandishwa mpaka mbinguni? Utashushwa mpaka chini katika kuzimu.” 16 Yesu akaongeza kuwaambia wanafunzi wake: “Yule anayewasikiliza ninyi, ananisikiliza mimi; yule asiyewapokea ninyi, hanipokei mimi, na yule asiyenipokea mimi, hamupokei yule aliyenituma.” Kurudia kwa wale wanafunzi makumi saba 17 Wale wanafunzi makumi saba wakarudia wakijazwa na furaha, nao wakasema: “Bwana, hata pepo wanatutii tunapowaamuru kwa jina lako!” 18 Naye Yesu akamwambia: “Nilimwona Shetani akianguka kama umeme toka mbinguni. 19 Muangalie, nimewapa uwezo wa kukanyaga nyoka na nge na mamlaka ya kumushinda yule adui Shetani; wala hakuna kitu chochote kitakachowazuru. 20 Hata hivi musifurahi kwa sababu pepo wanawatii, lakini mufurahi kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.” Yesu anafurahi ( Mat 11.25-27 ; 13.16-17 ) 21 Saa ile ile, Yesu akajazwa na furaha kwa uwezo wa Roho Mutakatifu, naye akasema: “Ee Baba, Bwana wa mbingu na dunia, ninakushukuru kwa maana mambo uliyoyaficha kwa watu wenye hekima na elimu, umeyafunua kwa wanaokuwa wadogo. Ndiyo Baba, hayo yote ni kutokana na mapenzi yako. 22 “Baba yangu, umeweka vitu vyote katika mikono yangu. Hakuna mutu anayemujua Mwana isipokuwa Baba, wala hakuna anayemujua Baba isipokuwa Mwana na yeyote ambaye Mwana anataka kumujulisha kwake.” 23 Kisha Yesu akawageukia wanafunzi wake wakiwa peke yao, akawaambia: “Heri watu wanaoona mambo yale munayoona! 24 Kwa maana ninawaambia: manabii wengi na wafalme walitamani kuona mambo munayoyaona, lakini hawakuyaona, na kusikia maneno munayoyasikia, lakini hawakuyasikia.” Mufano wa Musamaria mwema 25 Halafu mwalimu mumoja wa Sheria akasimama na kumwuliza Yesu kwa kumupima: “Mwalimu, nifanye nini kusudi nipate uzima wa milele?” 26 Yesu akamujibu: “Imeandikwa namna gani katika Sheria? Unaielewa namna gani unapoisoma?” 27 Mutu yule akamujibu kwa maneno haya: “ ‘Umupende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa roho yako yote, kwa nguvu yako yote na kwa akili yako yote.’ Vilevile, ‘Umupende mwenzako kama vile unavyojipenda mwenyewe.’ ” 28 Basi Yesu akamwambia: “Umejibu vizuri. Fanya sawa vile unavyosema, nawe utaishi milele.” 29 Lakini kwa kutaka kujipatia haki, yeye akamwuliza Yesu: “Mwenzangu ni nani?” 30 Yesu akajibu akimwelezea: “Mutu mumoja alitoka Yerusalema akishuka kwenda Yeriko. Alipokuwa katika njia, akashambuliwa na wanyanganyi, wakamuvua nguo, wakamupigapiga, wakajiendea, wakimwacha karibu kufa. 31 Kukatokea kuhani mumoja akishuka katika njia ile ile. Wakati alipomwona yule mutu, akapita pembeni na kujiendea. 32 Vilevile Mulawi mumoja akafika kwenye nafasi ile, naye alipomwona mutu yule, akapita pembeni na kujiendea. 33 Lakini Musamaria mumoja, alikuwa akisafiri vilevile katika njia ile, akafika kwenye nafasi ile yule mutu alipokuwa. Wakati alipomwona, akamusikilia huruma. 34 Akajongea karibu naye, akamutunza vidonda, akivimwangia divai na kuvimimia mafuta na kuvifunga na vitambaa. Kisha akamupandisha juu ya punda wake, na kumupeleka kwenye nyumba ya kupangisha wageni na kumuchunga. 35 Kesho yake akatwaa vikoroti viwili vya feza, na kuvitoa kwa mwenye nyumba, akimwambia: ‘Umuchunge mutu huyu, na feza zingine utakazotumia zaidi ya hizi kwa matunzo yake, nitazilipa kwako nitakaporudia.’ ” 36 Halafu Yesu akamwuliza yule mwalimu wa Sheria: “Kati ya hawa watatu ni nani aliyemutendea yule mutu aliyeshambuliwa na wanyanganyi kama vile mwenzake?” 37 Naye akajibu: “Ni yule aliyemusikilia huruma.” Halafu Yesu akamwambia: “Kwenda, nawe ufanye sawa sawa.” Yesu katika nyumba ya Marta na Maria 38 Yesu na wanafunzi wake walipokuwa wakisafiri, wakaingia katika kijiji kimoja. Kule mwanamuke mumoja aliyeitwa Marta akamukaribisha ndani ya nyumba yake. 39 Marta alikuwa na dada yake mudogo aliyeitwa Maria. Huyo aliikaa mbele ya Bwana, akisikiliza mafundisho yake. 40 Lakini Marta alikuwa anafungwa na kazi nyingi za nyumba. Kwa hiyo akamwendea Yesu na kumwambia: “Bwana, haikuhangaishi kitu kuona jinsi dada yangu anavyoniachilia kutumika mimi peke? Umwambie anisaidie.” 41 Bwana akamujibu: “Marta! Marta! Kwa nini unahangaika na kusumbuka kwa ajili ya vitu vingi? 42 Kuna kitu kimoja tu cha lazima. Maria amechagua kitu kinachokuwa kizuri zaidi ambacho hakuna mutu atakayekiondoa kwake.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo