Luka 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Utangulizi 1-3 Muheshimiwa Teofilo: Watu wengi wamejaribu kuandika juu ya mambo yale yaliyotendeka katikati yetu. Wameyaandika sawa vile tulivyoelezwa na wale walioona mambo yale tangu mwanzo, na waliotangaza ujumbe ule. Inafaa nami vilevile kisha kuchunguza kwa uangalifu mambo yote tangu mwanzo, nikuandikie kwa utaratibu, 4 kusudi upate kujua ukweli juu ya mambo uliyofundishwa. Malaika anatangaza habari ya kuzaliwa kwa Yoane Mubatizaji 5 Katika siku Herode alipokuwa mufalme wa Yudea, kulikuwa kuhani mumoja, aliyeitwa Zakaria, wa kundi la makuhani wa ukoo wa Abiya. Muke wake Elizabeti alikuwa vilevile wa uzao wa Kuhani Mukubwa Haruni. 6 Wote wawili walikuwa wenye haki mbele ya Mungu, walishika kwa ukamilifu amri na maagizo yote ya Bwana. 7 Lakini hawakukuwa na mutoto, kwa maana Elizabeti alikuwa tasa, tena wote wawili walikuwa wazee sana. 8 Siku moja, Zakaria alikuwa akimutumikia Mungu, akifanya kazi yake ya ukuhani kwa maana ilikuwa zamu ya kundi lake. 9 Na kama ilivyokuwa desturi ya makuhani, yeye alichaguliwa kwa njia ya kupiga kura kwa kuingia ndani ya hekalu la Bwana, kusudi achome ubani. 10 Kundi kubwa la watu walikuwa inje wakiomba saa ile Zakaria alipokuwa akichoma ubani. 11 Halafu malaika wa Bwana akamutokea Zakaria, akisimama upande wa kuume wa mazabahu ya kuchomea ubani. 12 Wakati Zakaria alipomwona, akahangaika na kushikwa na woga. 13 Lakini yule malaika akamwambia: “Zakaria, usiogope, kwa maana Mungu amesikia maombi yako. Muke wako Elizabeti atakuzalia mutoto mwanaume, nawe utamwita jina lake Yoane. 14 Utakuwa na furaha na shangwe kwa ajili yake, na watu wengi watafurahia kuzaliwa kwake, 15 kwa maana atahesabiwa kuwa mutu mukubwa mbele ya Bwana. Hatakunywa divai wala kinywaji kikali, na atajazwa na Roho Mutakatifu tangu kuzaliwa kwake. 16 Atawageuza Waisraeli wengi kwa kumurudilia Bwana Mungu wao. 17 Atatangulia mbele ya kufika kwa Bwana, akiwa na roho na uwezo kama nabii Elia, kwa kuwapatanisha tena baba na watoto wao, na kuwageuza waasi wapate kuwa na hekima kama vile wenye haki. Hivi atamutayarishia Bwana watu wanaokuwa tayari kwa kumupokea.” 18 Zakaria akamwuliza yule malaika: “Kitu gani kitakachonijulisha kwamba maneno hayo ni ya kweli? Mimi ni muzee, na muke wangu amekwisha kuzeeka sana.” 19 Malaika akamujibu: “Mimi ni Gabrieli, anayebaki karibu na Mungu! Nimetumwa kusema nawe, kwa kukuletea habari hii njema. 20 Maneno yale yatatimia kwa wakati wake uliopangwa, lakini kwa sababu haukuyasadiki, utakuwa bubu. Hautaweza kusema mpaka siku ile mambo hayo yatakapotimia.” 21 Kwa muda wote watu wale walipokuwa inje, wakimungojea Zakaria, wakashangaa kwa kuona anakawia ndani ya hekalu. 22 Alipotoka inje, hakuweza kusema nao, na watu wakatambua kwamba amepata maono ndani ya hekalu. Lakini alikuwa akifanya alama kwa mikono, kwa sababu alibaki bubu. 23 Wakati Zakaria alipotimiza siku zake za kazi, akarudia kwenye nyumba yake. 24 Halafu nyuma ya siku zile, muke wake Elizabeti akapata mimba. Hakutokatoka ndani ya nyumba kwa muda wa miezi mitano, akisema: 25 “Sasa Bwana amenifanyia mema kwa kunitendea hivi; ameniondolea haya ya kutokuzaa niliyokuwa nayo mbele ya watu.” Malaika anatangaza habari ya kuzaliwa kwa Yesu 26 Mimba ya Elizabeti ilipotimiza miezi sita, Mungu akamutuma malaika Gabrieli katika muji mumoja wa Galilaya, unaoitwa Nazareti. 27 Alimutuma kwa binti mumoja aliyekuwa muchumba wa mutu mumoja wa ukoo wa mufalme Daudi, aliyeitwa Yosefu. Jina la yule binti liliitwa Maria. 28 Malaika akamufikia kwenye nyumba yao na kumwambia: “Salamu kwako, wewe uliyejaliwa neema kutoka kwa Mungu! Bwana yuko pamoja nawe.” 29 Wakati Maria aliposikia maneno haya, akahangaika sana na kujiuliza: “Maana ya salamu hii ni nini?” 30 Halafu malaika akamwambia: “Maria, usiogope, kwa maana Mungu amekujalia neema. 31 Utapata mimba, utazaa mutoto mwanaume, na utamwita jina lake Yesu. 32 Yeye atakuwa mwenye mamlaka, na ataitwa Mwana wa Mungu Mukubwa. Bwana Mungu atamuweka kuwa mutawala wa ufalme wa babu yake Daudi. 33 Yeye atatawala taifa la Israeli hata milele, nao ufalme wake hautakuwa na mwisho.” 34 Maria akamwuliza malaika: “Jambo hili litawezekana namna gani kwa maana mimi ningali bikira?” 35 Malaika akamujibu: “Roho Mutakatifu atakufikia, na uwezo wa Mungu Mukubwa utakufunika kama vile kivuli. Kwa sababu hii mutoto yule atakayezaliwa ataitwa Mutakatifu na Mwana wa Mungu. 36 Hata Elizabeti wa jamaa yako, amepata mimba, naye atazaa mutoto mwanaume, ijapokuwa yeye ni muzee. Yeye aliyekuwa akiitwa tasa, sasa huu ni mwezi wa sita wa mimba yake. 37 Kwa maana hakuna kisichowezekana kwa Mungu.” 38 Basi Maria akasema: “Mimi ni mujakazi wa Bwana; ifanyike kwangu sawa ulivyosema.” Kisha malaika akajiendea. Maria anamutembelea Elizabeti 39 Katika siku zile, Maria akafunga safari, akaenda kwa haraka katika muji mumoja uliokuwa katika vilima vya Yudea. 40 Akafika kwenye nyumba ya Zakaria, akaingia ndani yake na kumusalimia Elizabeti. 41 Elizabeti aliposikia salamu ya Maria, mutoto akajitingiza ndani ya tumbo lake. Elizabeti akajazwa na Roho Mutakatifu, 42 akasema kwa sauti kubwa: “Wewe umebarikiwa kuliko wanawake wote, na mutoto utakayemuzaa amebarikiwa! 43 Namna gani nimepata bahati hii ya kutembelewa na mama ya Bwana wangu? 44 Kwa maana mara moja niliposikia salamu yako, mutoto akajitingiza kwa furaha ndani ya tumbo langu. 45 Heri kwako wewe uliyesadiki kwamba maneno yale uliyoambiwa kutoka kwa Bwana yatatimizwa!” Wimbo wa Maria 46 Halafu Maria akasema: “Moyo wangu unamutukuza Bwana, 47 roho yangu inamufurahia Mungu, Mwokozi wangu; 48 kwa maana ameniangalia kwa huruma, mimi mujakazi wake munyenyekevu. Tangu sasa watu wote wataniita mwenye heri, 49 sababu Mungu Mwenye Uwezo, amenitendea maajabu. Jina lake ni takatifu. 50 Yeye anawasikilia wale wanaomwogopa huruma kwa vizazi vyote. 51 Ametenda kwa uwezo wake mukubwa, amewasambaza wale wanaofanya mipango kwa kiburi. 52 Amewashusha wafalme wenye uwezo, lakini amewainua wanyenyekevu. 53 Anawatajirisha wenye njaa, lakini amewaacha watajiri mikono mitupu. 54 Amesaidia Israeli mutumishi wake, akikumbuka huruma yake, 55 sawa alivyoahidi babu zetu, Abrahamu na wazao wake kwa milele.” 56 Maria akakaa na Elizabeti kadiri ya miezi mitatu. Kisha akarudia kwenye nyumba yao. Kuzaliwa kwa Yoane Mubatizaji 57 Wakati wa kuzaa kwa Elizabeti ulipotimia, akazaa mutoto mwanaume. 58 Wajirani zake na wandugu zake wa jamaa waliposikia jinsi Bwana amemusikilia huruma sana, wakafurahi wote pamoja naye. 59 Ilipotimia siku nane tangu mutoto alipozaliwa, wakaenda kumutahiri, nao wakataka kumupa jina la baba yake Zakaria. 60 Lakini mama yake akakataa na kuwaambia kwamba jina lake litaitwa Yoane. 61 Wakamwambia: “Mbona hakuna mutu katika jamaa yako anayeitwa kwa jina hili?” 62 Halafu wakamwuliza baba ya mutoto kwa njia ya kufanya alama jina gani analotaka wamupe. 63 Zakaria akaomba wamuletee kibao, naye akaandika maneno haya juu yake: “Jina lake ni Yoane.” Wote wakashangaa. 64 Na pale pale ulimi wa Zakaria ukafunguka, akaanza tena kusema, akasifu Mungu. 65 Basi watu wote waliokaa karibu naye wakashikwa na woga, na habari ya mambo haya yote ikaenea fasi zote katika inchi ya vilima vya Yudea. 66 Na wote waliosikia habari ile wakafikiri juu yake na kujiuliza: “Mutoto huyu atakuwa mutu gani?” Maana hakika nguvu ya Bwana ilikuwa pamoja naye. Wimbo wa Zakaria 67 Baba yake Zakaria akajazwa na Roho Mutakatifu, na kuanza kutabiri, akisema: 68 “Asifiwe Bwana, Mungu wa Waisraeli, maana amewasaidia watu wake na kuwakomboa. 69 Ametuletea Mwokozi mwenye uwezo, toka ukoo wa mutumishi wake Daudi. 70 Ni sawa alivyosema zamani kwa njia ya manabii wake watakatifu. 71 Aliahidi kutuokoa toka mikono ya waadui zetu, ndio wale wanaotuchukia. 72 Aliahidi kuwasikilia babu zetu huruma; na kukumbuka agano lake takatifu, 73 sawa alivyomwapia babu yetu Abrahamu. 74 Alimwahidi kutuokoa toka mikono ya waadui zetu, kusudi tumutumikie pasipo woga, 75 katika hali ya utakatifu na haki mbele yake siku zote za maisha yetu. 76 Na wewe, mutoto wangu, utaitwa nabii wa Mungu Mukubwa, maana utatangulia mbele ya kufika kwa Bwana, kusudi umutengenezee njia. 77 Upate kuwajulisha watu wake kwamba atawaokoa akisamehe zambi zao. 78 Kutokana na huruma kubwa ya Mungu wetu, atatutumia mwangaza kutoka juu. 79 Atawaangazia wale wanaoishi katika giza na wanaokaa katika kivuli cha kifo, kusudi atuongoze tupate kufuata njia ya amani.” 80 Mutoto yule akakomaa na kuzidi kuwa na nguvu katika roho. Akakaa katika nafasi za jangwa mpaka siku alipojionyesha waziwazi mbele ya Waisraeli. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo