Kutoka 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu anaamuru Musa na Haruni 1 Yawe akamwambia Musa: “Mimi ninakufanya kuwa kama mungu kwa mufalme wa Misri, naye ndugu yako Haruni atakuwa nabii wako. 2 Utamwambia ndugu yako Haruni mambo yote nitakayokujulisha. Naye Haruni ndugu yako, atamwambia mufalme wa Misri awaache Waisraeli watoke katika inchi yake. 3 Lakini nitafanya moyo wa mufalme kuwa mugumu. Na hata kama nitazidisha vitambulisho na maajabu yangu katika inchi ya Misri, 4 Mufalme wa Misri hatakusikiliza. Na hapo nitanyoosha mukono wangu wenye nguvu na kuazibu vikali inchi ya Misri na kuwatoa watu wangu, makabila ya Israeli, kutoka Misri. Nitafanya hivyo kwa matendo makubwa ya hukumu juu ya Misri, 5 wakati nitakaponyoosha mukono wangu juu ya inchi ya Misri na kuwatoa Waisraeli kati yao. Halafu Wamisri watatambua kwamba mimi ni Yawe.” 6 Basi, Musa na Haruni wakafanya hivyo. Hakika, walifanya kama vile Yawe alivyowaamuru. 7 Musa alikuwa na umri wa miaka makumi nane, na Haruni alikuwa na umri wa miaka makumi nane na mitatu wakati ule walipoongea na mufalme wa Misri. Fimbo ya Haruni 8 Yawe akamwambia Musa na Haruni: 9 “Mufalme wa Misri atakapowaambia muhakikishe jambo lile kwa kutenda miujiza, wewe utamwambia Haruni atwae fimbo yake, aitupe mbele ya mufalme, nayo itakuwa nyoka.” 10 Basi, Musa na Haruni wakamwendea mufalme wa Misri na kufanya kama vile walivyoamuriwa na Yawe. Haruni akatupa fimbo yake chini mbele ya mufalme na wakubwa wake, nayo ikakuwa nyoka. 11 Lakini, mufalme wa Misri akawaita wenye hekima wake na wachawi. Wale wachawi wa Misri wakafanya vile vile kwa uchawi wao. 12 Kila mumoja akatupa fimbo yake chini, ikakuwa nyoka. Lakini fimbo ya Haruni ikameza fimbo zao. 13 Hata hivyo, moyo wa mufalme ulibaki tu kuwa mugumu, wala hakuwasikiliza. Ikakuwa kama vile Yawe alivyosema. MAPIGO KUMI Pigo la kwanza: Damu 14 Kisha Yawe akamwambia Musa: “Moyo wa mufalme wa Misri umekuwa mugumu. Anakataa kuwaacha Waisraeli waondoke. 15 Basi, kwenda ukutane naye kesho asubui, wakati anapokwenda kwenye muto Nili. Umungojee kando ya muto. Utwae katika mukono wako ile fimbo iliyogeuka kuwa nyoka. 16 Kisha umwambie hivi: Yawe, Mungu wa Waebrania, amenituma kwako, naye anasema hivi: ‘Uwaache watu wangu waende zao kusudi wanitumikie katika jangwa. Lakini mpaka sasa wewe haupendi kutii. 17 Basi, Yawe anasema kwamba sasa utamutambua yeye ni nani. Nitayapiga maji ya muto Nili kwa fimbo hii na maji yote yatageuka kuwa damu. 18 Samaki wanaokuwa ndani ya muto Nili watakufa, muto wote utanuka vibaya, na Wamisri watachukia kabisa kunywa maji yake.’ ” 19 Yawe akamwambia Musa: “Umwambie Haruni atwae fimbo yake na kuiinua juu ya maji ya Misri, juu ya mito yote, mifereji, visima na maji yao yote, nayo yatakuwa damu. Kutakuwa damu katika inchi yote, na hata katika vyombo vyote vya muti na vya mawe.” 20 Musa na Haruni wakafanya kama vile Yawe alivyowaamuru. Haruni akainua fimbo yake juu mbele ya mufalme wa Misri na wakubwa wake, akayapiga maji ya muto Nili, na maji yote katika muto yakageuka kuwa damu. 21 Samaki wakakufa, muto ukanuka vibaya sana hata Wamisri hawakuweza kunywa maji yake. Inchi nzima ikajaa damu. 22 Lakini wachawi wa Misri kwa kutumia uchawi wao wakafanya vivyo hivyo. Kwa hiyo moyo wa mufalme wa Misri ukabaki kuwa mugumu, naye hakuwasikiliza Musa na Haruni. Ikakuwa kama vile Yawe alivyokuwa amesema. 23 Basi, mufalme wa Misri akarudi katika nyumba yake na hata yale yaliyotokea hakuyajali. 24 Wamisri wote wakachimbachimba kandokando ya muto Nili kusudi wapate maji ya kunywa, maana hawakuweza kunywa maji ya muto ule. 25 Pigo hilo la muto Nili lilidumu siku saba. Pigo la pili: Vyura 26 Kisha Yawe akamwambia Musa: “Kwenda kwa mufalme wa Misri umwambie Yawe anasema hivi: Uwaache watu wangu waondoke kusudi wanitumikie. 27 Lakini ukikataa kuwaacha waondoke, basi, nitapiga inchi yako yote kwa kuiletea vyura. 28 Muto Nili utajaa vyura, nao wataingia mpaka ndani ya nyumba yako, chumba chako cha kulala, juu ya kitanda chako, na katika nyumba za watumishi wako na watu wako. Vyura hao wataingia katika mafika yenu na vyombo vyenu vya kufinyangia unga. 29 Vyura watapanda juu ya mwili wako, miili ya watu wako na watumishi wenu!” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo