Kutoka 39 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Nguo za makuhani: kizibao ( Kut 28.1-14 ) 1 Kwa kutumia sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu walifuma nguo za kuvaa wakati wa kutumika katika Pahali Patakatifu. Walimushonea Haruni nguo takatifu kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. 2 Wakatengeneza kizibao kwa nyuzi za zahabu, kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kwa kitani safi iliyosokotwa. 3 Wakafua zahabu na kuikata katika nyuzi nyembamba kwa kuzifuma pamoja na sufu ya rangi ya samawi, ya zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa kwa ufundi. 4 Kizibao hicho kilivaliwa kwa kamba mbili juu ya mabega zilizoshonewa kwenye incha zake mbili. 5 Mukaba uliofumwa kwa ufundi juu yake kwa kuifunga ulikuwa kitu kimoja na kizibao hicho, na ulitengenezwa kwa vitu hivyohivyo: zahabu, sufu ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. 6 Kisha wakatayarisha mawe ya sardoniki na kuyapanga katika kingo za zahabu. Nayo yalichorwa, kama vile mutu anavyochora muhuri, majina kumi na mawili ya wana wa Israeli. 7 Wakaweka mawe yale juu ya mikaba ya mabega za kila kizibao kuwa ukumbusho wa makabila kumi na mawili ya Israeli, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Kifuko cha kifua ( Kut 28.15-30 ) 8 Wafundi walitengeneza kifuko cha kifua kama vile walivyotengeneza kile kizibao, kwa zahabu, kwa sufu ya rangi ya samawi, ya zambarau na ya nyekundu, na kwa kitani safi iliyosokotwa. 9 Kifuko hicho kilikuwa cha muraba, sentimetre makumi mbili na mbili kwa sentimetre makumi mbili na mbili nacho kilikunjwa. 10 Kifuko hicho kilipambwa kwa mistari mine ya mawe ya bei kali. Mustari wa kwanza ulikuwa wa akiki, topazi na almasi nyekundu. 11 Mustari wa pili ulikuwa wa zumaridi, yakuti-samawi na almasi. 12 Mustari wa tatu ulikuwa wa yasinto, akiki nyekundu na ametisto. 13 Mustari wa ine ulikuwa wa zabarajadi, shohamu na yaspi. Yote yalifungwa ndani ya kingo za zahabu. 14 Basi, kulikuwa mawe kumi na mawili yaliyochorwa juu yake majina kumi na mawili ya wana wa Israeli. Yalikuwa yamechorwa kama vile wanavyochora muhuri, juu ya kila moja kulichorwa jina kwa ukumbusho wa makabila kumi na mawili. 15 Walitengenezea kile kifuko cha kifua mikufu ya zahabu safi. 16 Wakatengeneza kingo mbili za zahabu safi na pete mbili za zahabu, na kutia pete hizo kwenye incha mbili za juu za kifuko hicho. 17 Mikufu hiyo miwili ya zahabu wakaifunga kwenye pete hizo za kifuko cha kifua. 18 Zile incha mbili za mikufu ya zahabu wakazitia kwenye zile kingo mbili wakazishikamanisha na vile vipande viwili vya mabega vya kizibao, upande wa mbele. 19 Wakatengeneza pete mbili za zahabu, wakazitia kwenye incha mbili za chini upande wa ndani wa kifuko hicho cha kifua karibu na kizibao. 20 Wakatengeneza pete zingine mbili za zahabu na kuzitia mbele katika incha za chini za vipande vya kizibao, pahali kinapoungana na ule mukaba uliofumwa kwa ufundi. 21 Wakafunga kifuko cha kifua kwenye kizibao kwa kufunganisha pete zake na kizibao kwa kamba ya rangi ya samawi, kusudi kifuko hicho kisiregee lakini kiikalie ule mukaba uliofumwa kwa ufundi, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Nguo zingine za kikuhani ( Kut 28.31-43 ) 22 Akatengeneza kanzu ya kuvaa ndani ya kizibao ya rangi ya samawi. 23 Koti hilo lilikuwa na nafasi ya kupitishia kichwa katikati, nalo lilizungushiwa utepe uliofumwa kusudi isichanike. 24 Kwenye upindo wa chini wa kanzu walifuma mapambo ya makomamanga ya rangi ya samawi, ya zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa. 25 Kisha walitengeneza kengele za zahabu na kisha kila komamanga walitia kengele kwenye upindo wa koti. 26 Hivyo, kengele na komamanga vilifuatana kuzunguka upindo wa koti hilo, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. 27 Kisha wakawafumia Haruni na wana wake vizibao vya kitani safi, 28 kitambaa cha kitani safi, kofia za kitani safi, makapitula za kitani safi iliyosokotwa, 29 na mikaba ya kitani safi iliyosokotwa kwa sufu ya rangi ya samawi, ya zambarau na nyekundu na kupambwa vizuri, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. 30 Kisha wakatengeneza pambo la zahabu safi kwa ajili ya taji takatifu na kuchora juu yake kama vile wanavyochora muhuri: Takatifu kwa Yawe. 31 Kisha wakalifunga mbele ya kile kitambaa kwa mukaba wa rangi ya samawi, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. Kukamilika kwa kazi ( Kut 35.10-19 ) 32 Basi, kazi yote ya hema la mukutano ikamalizika. Waisraeli walifanya yote kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. 33 Wakamuletea Musa hema takatifu pamoja na vyombo vyake vyote, vifungio vyake, mbao zake, miti yake, nguzo zake na vikalio vyake; 34 kifuniko cha ngozi za kondoo dume na mbuzi kilichotiwa rangi nyekundu, pazia la Pahali Patakatifu, 35 Sanduku la Agano, miti yake na kiti cha rehema; 36 meza na vyombo vyake vyote, mikate iliyotolewa kwa Mungu; 37 kinara cha taa cha zahabu safi, taa zake, vyombo vyake vyote pamoja na mafuta kwa ajili ya taa hizo; 38 mazabahu ya zahabu; mafuta ya kupakaa, ubani wenye harufu nzuri, na pazia la mulango wa hema; 39 mazabahu ya shaba na wavu wake wa shaba, miti yake na vyombo vyake vyote; bakuli, birika na tako lake; 40 mapazia ya upango, nguzo zake na vikalio vyake; pazia la mulango wa upango, kamba zake na misumari yake; vyombo vyote vilivyohitajika katika kazi ya hema takatifu, ni kusema hema la mukutano; 41 na nguo zote zilizofumwa vizuri kabisa kwa ajili ya kazi ya Pahali Patakatifu, ni kusema nguo takatifu za kuhani Haruni, na za wana wake kwa ajili ya kazi za ukuhani. 42 Waisraeli walifanya kila kitu kama vile Yawe alivyomwamuru Musa. 43 Musa akachunguza kila kitu, akaona kwamba walikuwa wamefanya kila kitu kama vile Yawe alivyoamuru. Hivyo Musa akawabariki. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo