Kutoka 33 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu anamwamuru Musa waanze safari 1 Yawe akamwambia Musa: Anza safari uondoke hapa, wewe na watu hao uliowatoa katika inchi ya Misri. Muende katika inchi niliyowapia Abrahamu, Isaka na Yakobo, nikisema: Nitawapa wazao wenu inchi hii. 2 Nitamutuma malaika awaongoze. Nitawafukuza Wakanana, Waamori, Wahiti, Waperizi, Wahivi na Wayebusi. 3 Muende katika inchi hiyo inayotiririka maziwa na asali. Lakini kwa sababu ninyi ni wenye vichwa vigumu sitakwenda pamoja nanyi, nisiwaangamize katika njia. 4 Watu wakalia waliposikia habari hizi mbaya, wala hakuna aliyevaa mapambo yake. 5 Walifanya hivyo maana Yawe alikuwa amemwambia Musa: Uwaambie Waisraeli: Ninyi ni watu wenye vichwa vigumu. Nikienda pamoja nanyi kwa muda mufupi tu, nitawaangamiza. Hivyo muvue mapambo yenu kusudi nijue namna ya kuwatendea. 6 Basi, Waisraeli wakavua mapambo yao tangu walipoondoka kwenye mulima Horebu. Hema la mukutano 7 Musa alikuwa na desturi ya kuchukua lile hema na kulisimika inje ya kambi. Hema hilo alilipa jina, hema la mukutano. Mutu yeyote aliyetaka shauri kwa Yawe alikwenda kwenye hema la mukutano inje ya kambi. 8 Kila mara Musa alipotoka kwenda kwenye hema hilo, kila mutu alisimama kwenye mulango wa hema yake na kumwangalia Musa mpaka alipoingia ndani ya hilo hema. 9 Wakati Musa alipoingia ndani ya hilo hema, munara wa wingu ulitua kwenye mulango wa hema, na Yawe akaongea naye. 10 Watu wote walipouona ule munara wa wingu umesimama kwenye mulango wa hema, kila mumoja wao alisimama na kuabudu kwenye mulango wa hema lake. 11 Hivi ndivyo Yawe alivyokuwa akiongea na Musa uso kwa uso, kama mutu na rafiki yake. Kisha Musa alirudi tena katika kambi. Naye kijana Yoshua mwana wa Nuni ambaye alikuwa mutumishi wake hakuondoka ndani ya hema. Yawe anaahidi kuwa na watu wake 12 Musa akamwambia Yawe: Wewe unaniambia: Uwaongoze watu hawa, lakini haujanijulisha ni nani utakayemutuma anisaidie. Hata hivyo umesema kwamba unanijua kwa jina langu na vilevile kwamba nimepata kukubaliwa mbele yako. 13 Sasa basi, ninakusihi, kama nimepata kukubaliwa mbele yako, unionyeshe sasa njia zako, kusudi nipate kukujua na kupata kukubaliwa mbele yako. Ninaomba ukumbuke vilevile kwamba taifa hili ni watu wako. 14 Mungu akasema: Mimi mwenyewe nitakwenda pamoja nawe na nitakupa raha. 15 Musa akasema: Kama wewe peke yako hautakwenda pamoja nami, basi, usituondoe pahali hapa. 16 Maana namna gani itajulikana kwamba nimepata kukubaliwa mbele yako, mimi na watu wako kama usipokwenda pamoja nasi? Ukienda pamoja nasi itatufanya mimi na watu wako kuwa watu wa pekee kati ya watu wote katika dunia. 17 Yawe akamwambia Musa: Kwa sababu umepata kukubaliwa mbele yangu, nami ninakujua kwa jina lako, jambo hilihili ulilolisema nitalifanya. 18 Musa akasema: Ninakusihi unionyeshe utukufu wako. 19 Yawe akamujibu: Nitapita mbele yako na kukuonyesha uzuri wangu wote nikilitangaza jina langu, Yawe. Mimi nitamuhurumia yule ninayependa kumuhurumia; nitamurehemu yule ninayependa kumurehemu. 20 Lakini hautaweza kuniona uso maana hakuna mwanadamu yeyote atakayeniona na kuishi. 21 Kisha Yawe akamwambia Musa: Kuna pahali karibu nami ambapo utasimama juu ya jiwe. 22 Utukufu wangu utakapokuwa unapita, nitakutia katika pango chini ya jiwe na kukufunika kwa mukono wangu, mpaka nitakapokuwa nimepita. 23 Halafu nitaondoa mukono wangu nawe utaona mugongo wangu, lakini uso wangu hautauona. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo