Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Kutoka 19 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Waisraeli kwenye mulima Sinai

1 Siku ya kwanza ya mwezi wa tatu tangu walipotoka katika inchi ya Misri, watu wa Israeli wakafika katika jangwa la Sinai.

2 Walipoondoka Refidimu na kufika jangwa la Sinai, kule wakapiga kambi mbele ya mulima Sinai.

3 Basi, Musa akapanda juu kwenye mulima kwa Mungu. Halafu Yawe akamwita Musa kutoka kule juu ya mulima, akamwambia: “Hivi ndivyo utakavyowaambia wazao wa Yakobo, wale Waisraeli:

4 ‘Ninyi wenyewe mumeona jinsi nilivyowatendea Wamisri na jinsi nilivyowapeleka ninyi kama vile tai anavyopeleka watoto wake kwa mabawa, nikawaleta kwangu.

5 Sasa basi, kama mukitii sauti yangu na kushika agano langu, mutakuwa watu wangu wachaguliwa kati ya mataifa yote, maana dunia yote ni yangu.

6 Mutakuwa kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.’ Hayo ndiyo maneno utakayowaambia Waisraeli.”

7 Basi, Musa akarudi, akawakusanya pamoja wazee wa Waisraeli na kuwaambia maneno hayo aliyoamuriwa na Yawe.

8 Watu wote wakaitikia kwa pamoja wakisema: “Mambo yote Yawe aliyosema, tutayafanya.” Musa akamujulisha Yawe jibu lile la watu.

9 Yawe akamwambia Musa: “Basi, mimi nitakufikia katika wingu zito kusudi Waisraeli wapate kunisikia ninaposema nawe na kukuamini siku zote.” Kisha Musa akamwambia Mungu jinsi watu walivyosema.

10 Yawe akamwambia Musa: “Kwenda kwa watu uwatakase leo na kesho. Uwaambie wafue nguo zao

11 wakuwe tayari kwa kesho kutwa, maana siku hiyo ya tatu mimi Yawe nitashuka juu ya mulima Sinai mbele ya watu wote.

12 Tena wewe utawawekea watu mupaka kuzunguka mulima kuwaambia wajilinde sana wasipande juu kwenye mulima wala kugusa mupaka wake. Yeyote atakayegusa mulima, atauawa.

13 Mutu asimuguse mutu yule. Atauawa kwa kupigwa mawe au mushale. Akuwe ni mutu au ni nyama, hataishi. Wakati baragumu itakapopigwa mufululizo, watu wote watakaribia mulima.”

14 Basi, Musa akashuka toka juu ya mulima na kuwaendea watu, akawatakasa, nao wakafua nguo zao.

15 Kisha akawaambia watu wote: “Kesho kutwa mukuwe tayari na mwanaume yeyote asimukaribie mwanamuke.”

16 Basi, siku ya tatu asubui, kukatokea ngurumo na umeme na wingu zito juu ya mulima. Kukasikilika vilevile sauti kubwa ya baragumu ambayo iliwatetemesha watu wote katika kambi.

17 Kisha Musa akawaongoza watu wote kutoka katika kambi, wakaenda kukutana na Mungu. Wote walikwenda wakajipanga chini ya mulima.

18 Mulima wa Sinai ulikuwa umefunikwa na moshi kwa sababu Yawe alishuka juu yake katika moto. Moshi wa moto ule ulipanda juu kama moshi wa furu kubwa na mulima wote ukatetemeka kwa nguvu.

19 Sauti ya baragumu ikazidi kuongezeka na Musa akaongea na Mungu. Mungu naye akamujibu katika ngurumo.

20 Yawe akashuka juu ya mulima Sinai, akamwita Musa kutoka kule juu, naye Musa akapanda juu ya mulima.

21 Kisha Yawe akamwambia Musa: “Shuka chini uwaonye watu wote wasikuje kuniona. Kama sivyo wengi wao wataangamia.

22 Hata makuhani ambao wananikaribia wanapaswa kujitakasa, kama sivyo nitawaazibu.”

23 Musa akamwambia Yawe: “Watu hawa hawawezi kupanda juu ya mulima wa Sinai maana wewe mwenyewe ulituamuru tuweke mupaka kuzunguka mulima na kuutakasa.”

24 Yawe akasema: “Teremuka chini kisha urudi pamoja na Haruni. Lakini usiwaruhusu makuhani na watu wengine wapite mupaka na kuja kwangu, kama sivyo nitawaazibu.”

25 Basi, Musa akashuka na kuwaambia Waisraeli mambo yote aliyoagizwa.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan