Kutoka 16 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mana na kwale 1 Waisraeli wote wakasafiri toka Elimu na kufika katika jangwa la Sini kati ya Elimu na Sinai. Hii ilikuwa siku ya kumi na tano ya mwezi wa pili tangu walipoondoka inchi ya Misri. 2 Basi, Waisraeli wote pamoja wakamunungunikia Musa na Haruni kule katika jangwa. Wakasema hivi: 3 “Heri Yawe angelituua tulipokuwa katika inchi ya Misri ambako tulikaa, tukakula nyama na mikate hata tukashiba. Lakini ninyi mumetuleta huku katika jangwa kwa kuua jamii hii yote kwa njaa!” 4 Halafu Yawe akamwambia Musa: “Mimi nitawanyeshea mikate kutoka mbinguni. Kila siku watu watatoka na kukusanya chakula cha siku hiyo. Kwa njia hii nitawapima nione kama watafuata sheria zangu au hawatazifuata. 5 Lakini siku ya sita, wakati watakapotayarisha chakula walichokusanya, kipimo kile kitakuwa mara mbili ya chakula cha kila siku.” 6 Basi, Musa na Haruni wakawaambia watu wote wa Israeli: “Magaribi, mutatambua kwamba Yawe ndiye aliyewatoa katika inchi ya Misri! 7 Tena, kesho asubui mutaona utukufu wa Yawe maana ameyasikia manunguniko muliyomunungunikia. Sisi ni nani hata mutunungunikie?” 8 Tena Musa akasema: “Magaribi, Yawe atawapa nyama mupate kula na asubui atawapa mikate mupate kula na kushiba. Maana yeye ameyasikia manunguniko muliyomunungunikia. Sisi ni nani hata mutunungunikie? Musitunungunikie sisi lakini mumunungunikie Yawe.” 9 Kisha Musa akamwambia Haruni: “Uwaambie Waisraeli wote wakusanyike mbele ya Yawe, maana ameyasikia manunguniko yao.” 10 Wakati Haruni alipokuwa akizungumuza na Waisraeli wote pamoja, watu wote wakaangalia kule katika jangwa na mara moja utukufu wa Yawe ukaonekana katika mawingu. 11 Yawe akamwambia Musa: 12 “Nimesikia manunguniko ya Waisraeli. Basi, uwaambie kwamba wakati wa magaribi watakula nyama na asubui watakula mukate. Hapo ndipo mutakapotambua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wenu.” 13 Basi, kwa wakati wa magaribi kukakuja kwale wengi, wakafunika kambi ya Waisraeli. Asubui yake kukatokea umande, ukatanda kandokando ya kambi yao. 14 Umande ule ulipotoweka, kukabaki kule katika jangwa kitu kama mukate mwembamba na mwepesi. 15 Waisraeli walipoona kitu kile wakashangaa, wakaulizana: “Nini hii?” Hawakujua kilikuwa kitu gani. Basi, Musa akawaambia: “Huu ni mukate ambao Yawe amewapa mukule. 16 Yawe ameamuru mufanye hivi: kila mutu akusanye chakula kipimo anachoweza kula. Ataokota kipimo cha litre ine kwa kila mutu katika hema yake.” 17 Basi, Waisraeli wakafanya hivyo na ikakuwa kwamba wengine waliokota kwa wingi na wengine kidogo. 18 Lakini wote walipopima kiasi walichookota katika kipimo cha litre ine, walitambua kwamba aliyeokota kingi hakukuwa na cha zaidi na aliyeokota kidogo, hakupungukiwa. Kila mumoja alikuwa ameokota kiasi alichoweza kula. 19 Musa akawaambia watu: “Mutu yeyote asiache chakula hicho mpaka asubui.” 20 Lakini watu hawakumusikiliza Musa. Wamoja kati yao walijiwekea chakula mpaka asubui. Lakini asubui chakula hicho kikakuwa kimeoza na kuwa na vidudu. Musa akawakasirikia sana watu. 21 Basi, kila asubui walikusanya chakula kila mutu kipimo alichohitaji kula. Jua lilipopanda juu na kuwa kali, kile chakula kingine kiliyeyuka. 22 Katika siku ya sita, Waisraeli walikusanya chakula hicho mara mbili, vipimo viwili vya litre ine kwa kila mutu. Basi, wazee wote wa Waisraeli wakamwendea Musa, wakamwelezea jambo hilo. 23 Musa akawaambia: “Hii ndiyo amri ya Yawe. Kesho ni siku ya mapumziko. Ni Sabato takatifu ya Yawe. Basi, muende mupike au kuchemusha kile chakula munachohitaji leo na chakula kitakachobakia mukiweke mpaka kesho.” 24 Basi, wakafanya hivyo na kuacha chakula kingine mpaka kesho yake kama vile Musa alivyosema. Asubui yake waliona kwamba hakikuharibika wala kuwa na vidudu. 25 Basi, Musa akawaambia: “Mukule chakula hicho kilichobakia kwa sababu leo ni Sabato ya Yawe. Leo hamutapata chakula kule inje. 26 Kwa siku sita mutakuwa mukikusanya chakula hiki, lakini siku ya saba ambayo ni Sabato hakitakuwa.” 27 Kwa siku ya saba watu wamoja walitoka kwenda kutafuta chakula, lakini hawakukipata. 28 Hapo Yawe akamwambia Musa: “Mpaka wakati gani mutakataa kutii amri na sheria zangu? 29 Mufahamu kwamba mimi Yawe nimewapa siku ya Sabato, ndiyo maana nimewapa chakula cha siku mbili kwa siku ya sita. Basi, kila mutu apumzike ndani ya nyumba yake. Mutu yeyote asitoke katika siku ya saba.” 30 Kwa hiyo, watu walipumzika siku ya saba. 31 Waisraeli wakaita chakula hicho “Mana.” Kilikuwa kama mbegu za mutama mweupe na onjo yake ilikuwa kama mukate mwembamba uliotiwa asali. 32 Musa akawaambia: “Hili ndilo agizo la Yawe: Mutwae kipimo kimoja cha litre ine ya mana na kukiweka kwa ajili ya wazao wenu, kusudi waweze kuona chakula nilichowakulisha katika jangwa wakati nilipowatoa katika inchi ya Misri.” 33 Musa akamwambia Haruni: “Twaa kopo, utie ndani yake kipimo kimoja cha litre ine ya mana na kuiweka mbele ya Yawe, ikuwe kwa ajili ya wazao wenu.” 34 Basi, Haruni aliweka mana Pahali Patakatifu mbele ya Sunduku la Agano kusudi ilindwe kama vile Yawe alivyomwagiza Musa. 35 Waisraeli walikula mana kwa muda wa miaka makumi ine, mpaka walipofika katika inchi iliyofaa kwa kuishi, ni kusema mpaka walipovuka mupaka wa Kanana. 36 (Posho ya mana ilikuwa sehemu ya kumi ya kipimo cha kawaida kinachoitwa efa.) |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo