Kutoka 15 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Wimbo wa Musa 1 Kisha, Musa pamoja na Waisraeli wakamwimbia Yawe wimbo huu: “Nitamwimbia Yawe, maana ameshinda kwa utukufu; farasi na mupanda-farasi wake amewatupa katika bahari. 2 Yawe ananijalia nguvu na uwezo, yeye mwenyewe ndiye anayeniokoa. Yeye ni Mungu wangu nami nitamusifu; ni Mungu wa baba yangu nami nitamutukuza. 3 Yawe ni shujaa kwa vita; Yawe ndilo jina lake. 4 “Magari na majeshi ya mufalme wa Misri ameyatumbukiza ndani ya bahari; majemadari wake wachaguliwa wamezama katika bahari Nyekundu. 5 Vilindi vya maji vimewafunika, wameporomoka katika bahari kama jiwe. 6 “Mukono wako wa kuume, ee Yawe, unatukuka kwa nguvu; kwa mukono wako wa kuume, ee Yawe, unawaponda waadui. 7 Kwa wingi wa ukubwa wako unawaangamiza wapinzani wako; unawapulizia kasirani yako nayo inawateketeza kama maganda. 8 Kwa pumzi ya pua yako maji yalilundikana, mawimbi yakasimama wima kama ukuta; vilindi katikati ya bahari vikagandamana. 9 Adui akajisemesha: ‘Nitawafuata na kuwakamata; nitagawanya vitu mpaka hamu yangu iishe. Tutafuta upanga wetu, tutawaangamiza kwa mukono wetu.’ 10 Lakini wewe uliuvumisha upepo wako, nayo bahari ikawafunika. Walizama ndani ya maji kama risasi. 11 “Ewe Yawe, ni nani kati ya miungu anayelingana nawe? Ni nani aliyekuwa kama wewe unayekuwa mutakatifu mukubwa, unayetisha kwa matendo matukufu, unayetenda mambo ya ajabu? 12 Ulinyoosha mukono wako wa kuume, nayo inchi ikawameza waadui zetu. 13 “Kwa wema wako mukubwa umewaongoza watu uliowakomboa, kwa nguvu yako umewaongoza kwenye makao yako matakatifu. 14 Watu wa mataifa wamesikia hayo wakatetemeka; Wafilistini wamepatwa na kitisho. 15 Wakubwa wa Edomu wamefazaishwa; viongozi wa Moabu wamepatwa na woga mukubwa; wakaaji wote wa Kanana wamevunjika moyo. 16 Kitisho na hofu vimewashika. Kwa sababu ya ukubwa wa nguvu zako, wao wamenyamaza kimya kama jiwe, mpaka watu wako, ee Yawe, wapite, mpaka watu wale uliowakomboa wamewapita. 17 Wewe utawaleta watu wako na kuwapanda juu ya mulima wako, pale ulipochagua, ee Yawe, kuwa makao yako, pahali patakatifu, ee Yawe, ulipojenga kwa mikono yako. 18 “Wewe, ee Yawe, unatawala milele na milele.” 19 Wakati farasi wa mufalme wa Misri na magari yake pamoja na wapanda-farasi wake walipoingia pahali pakavu katika bahari, Yawe aliyarudisha maji ya bahari yakawafunika. Lakini Waisraeli waliendelea kutembea pakavu katikati ya bahari. 20 Basi nabii Miriamu, dada ya Haruni, akatwaa ngoma katika mukono, na wanawake wengine wote wakamufuata wakiwa na ngoma zao ndogo wakicheza. 21 Miriamu akawaongoza kwa kuimba: “Mumwimbie Yawe maana ameshinda kwa utukufu. Farasi na mupanda-farasi wake amewatupa ndani ya bahari.” Maji machungu 22 Kisha, Musa akawaongoza Waisraeli kutoka bahari Nyekundu, wakaenda mpaka kwenye jangwa la Suri. Wakasafiri kwa muda wa siku tatu katika jangwa bila kuona maji yoyote. 23 Walipofika pahali panapoitwa Mara, hawakuweza kunywa maji ya Mara kwa sababu yalikuwa machungu. Kwa sababu hiyo pahali pale pakaitwa Mara, ni kusema “Uchungu”. 24 Basi, watu wote wakamunungunikia Musa wakisema: “Sasa tutakunywa nini?” 25 Halafu Musa akamulilia Yawe, naye akamwonyesha kipande cha muti, na Musa akakitumbukiza katika maji. Maji hayo yakakuwa mazuri. Kule Mungu aliwapa Waisraeli sharti na agizo, kusudi awapime, 26 akawaambia: “Ikiwa mutaisikiliza kwa uaminifu sauti yangu mimi Yawe, Mungu wenu, kutenda yale yanayokuwa sawa mbele yangu, na kuheshimu amri na masharti yangu yote, basi, mimi sitawaletea yale magonjwa niliyowaletea Wamisri. Kwa sababu, mimi ni Yawe ninayewaponya ninyi.” 27 Kisha Waisraeli wakafika kule Elimu ambako kulikuwa chemichemi kumi na mbili na mingazi makumi saba. Wakapiga kambi yao kule karibu na maji. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo