Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Kutoka 13 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Kutakaswa kwa wazaliwa wa kwanza

1 Yawe alimwambia Musa:

2 “Unitakasie wazaliwa wote wa kwanza, maana wazaliwa wote wa kwanza wa Waisraeli ni wangu, ikuwe wanaume au wanyama.”


Sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu

3 Musa akawaambia watu: “Mukumbuke siku hii muliyotoka inchi ya Misri ambako mulikuwa watumwa. Hii ndiyo siku Yawe alipowatoa humo kwa mukono wake wenye nguvu. Katika siku hii, musikule mukate uliotiwa chachu.

4 Siku hii, mwezi wa kwanza wa Abibu, mutaondoka katika inchi ya Misri.

5 Na wakati Yawe atakapowafikisha katika inchi ya Wakanana, Wahiti, Waamori, Wahivi, na Wayebusi, inchi ambayo aliwaapia babu zenu kwamba atawapa ninyi, inchi inayotiririka maziwa na asali, munapaswa kushika sikukuu hii kila mwaka katika mwezi huu wa kwanza.

6 Kwa muda wa siku saba mutakula mikate isiyotiwa chachu, na katika siku ya saba mutafanya sikukuu kwa heshima ya Yawe.

7 Kwa muda ule wa siku saba mutakula mikate isiyotiwa chachu. Kusikuwe mikate iliyotiwa chachu, wala chachu yoyote kati yenu na katika inchi yenu yote.

8 Siku hiyo mutawaambia watoto wenu kwamba munafanya hivyo kwa sababu ya jambo Yawe alilowafanyia mulipoondoka katika inchi ya Misri.

9 Na mambo haya yatakuwa ukumbusho, kama vile kitambulisho katika mikono yenu au katika paji la nyuso zenu; kusudi kiwakumbushe siku zote sheria ya Yawe. Maana, Yawe amewatoa katika inchi ya Misri kwa mukono wenye nguvu.

10 Kwa hiyo, mutashika sikukuu hii kwa wakati uliopangwa, kila mwaka.”


Maelezo juu ya wazaliwa wa kwanza

11 Musa akaendelea kuwaambia watu: “Vilevile, wakati Yawe atakapowafikisha katika inchi ya Wakanana na kuwapa inchi ile kama vile alivyowaapia ninyi na babu zenu,

12 munapaswa kumuwekea Yawe kila muzaliwa wenu wa kwanza mwanaume. Kila muzaliwa wa kwanza dume wa mifugo yenu atakuwa wa Yawe.

13 Lakini muzaliwa wa kwanza dume wa punda utamukomboa kwa kulipa mwana-kondoo; kama sivyo, utamwua kwa kumuvunja shingo. Kila muzaliwa wa kwanza wa kiume wa mwanadamu utamukomboa.

14 Kama kisha mwana wako akiuliza maana ya jambo hili, utamwambia: ‘Kwa nguvu ya mukono wake, Yawe alitutoa katika inchi ya Misri ambako tulikuwa watumwa.

15 Mufalme wa Misri kwa ugumu wake alikataa kutuachilia tuondoke. Kwa hiyo Yawe akamwua kila muzaliwa wa kwanza katika inchi ya Misri, muzaliwa wa kwanza wa mwanadamu na wa nyama. Basi, mimi ninamutolea Yawe sadaka kila muzaliwa wa kwanza dume wa mifugo yangu. Lakini kila muzaliwa wa kwanza wa wana wangu ninamukomboa.’

16 Jambo hili litakuwa kama kitambulisho katika mukono wako au utepe katika paji la uso wako, kwamba Yawe alitutoa katika inchi ya Misri kwa mukono wenye nguvu.”


Munara wa wingu na wa moto

17 Wakati mufalme wa Misri alipowaachilia Waisraeli wajiendee, Mungu hakuwapitisha katika inchi ya Wafilistini, ingawa njia hiyo ilikuwa ya karibu. Mungu alisema: “Sipendi watu hawa wabadilishe nia na kurudi Misri wakijua kama itawapasa kupigana vita.”

18 Pahali pake, Mungu akawapitisha Waisraeli katika njia ya muzunguko kupitia katika jangwa, kuelekea bahari Nyekundu. Waisraeli wakaondoka katika inchi ya Misri wakiwa wamejitayarisha kwa vita.

19 Musa alipeleka mifupa ya Yosefu kama vile Yosefu alivyoagiza mbele ya kufa kwake. Alikuwa amewaapisha Waisraeli akisema: “Mungu atakapowafikia kuwatoa katika inchi hii, munapaswa kupeleka mifupa yangu kutoka hapa pamoja nanyi.”

20 Basi, Waisraeli wakaondoka Sukoti, wakapiga kambi kule Etamu, kwenye ukingo wa jangwa.

21 Muchana, Yawe aliwatangulia katika munara wa wingu kwa kuwaonyesha njia. Na usiku aliwatangulia katika munara wa moto kuwaangazia, kusudi waweze kusafiri muchana na usiku.

22 Munara wa wingu wakati wa muchana na munara wa moto wakati wa usiku haikukosekana kuwatangulia Waisraeli.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan